Friday, March 31, 2017

CONTE AMKOMALIA HAZARD.

MENEJA wa Chelsea, Antonio Conte amesisitiza Eden Hazard anafurahi kuwepo Stamford Bridge lakini amekubali tetesi za kuhitajika na klabu zingine zinaweza kuwaweka katika wakati mgumu wachezaji. Tetesi za hivi karibuni zinamuhusisha Hazard kuwaniwa na Real Madrid kwa kitita cha paundi milioni 100 majira ya kiangazi, ingawa nyota huyo wa kimataifa wa Ubelgiji amesisitiza kuwa yeye na familia wanafurahia maisha ya London. Conte amesema hafahamu kama maofisa wa Chelsea watakubali ofa rasmi ya usajili kwa Hazard lakini anadhani mazungumzo yanayoendelea pembani kuhusiana kuhusiana na mkataba wake yanaweza kufanya akili ya mchezaji isitulie. Conte aliendelea kudai kuwa anachofahamu hivi sasa ni kuwa Hazard bado ni mali ya Chelsea na anafurahia kuwepo hapo.

SCHNNEIDERLIN KUIKOSA LIVERPOOL.


KIUNGO wa Everton, Morgan Schneiderlin anatarajiwa kuukosa mchezo wa derby ya kesho dhidi ya Liverpool na pia safari ya kwenda kucheza na Manchester United wiki ijayo. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 27 amekuwa akisumbuliwa na majeruhi ya kigimbi aliyopata kwneye mchezo dhidi ya Hull City machi 18 mwaka huu lakini mapema wiki hii alionekana akifanya mazoezi mepesi gym. Hata hivyo, meneja wa Everton Ronaldo Koeman amesema Schneiderlin hataweza kucheza mechi hiyo ya kesho huku pia akiongeza anaweza asiwe fiti kwenye mchezo ujao dhidi ya United Jumanne ijayo. Koeman aliendelea kudai kuwa pamoja na nyota huyo kuanza mazoezi mepesi lakini hadhani kama atakuwepo kwenye mechi wala ile ya Jumanne ila anamtegemea atakuwa fiti kwa ajili ya mechi dhidi ya Leicester City. Taarifa hizo ni pigo kubwa kwa Everton wenye matumaini ya kushinda derby yao ya kwanza katika Ligi Kuu toka mwaka 2010.

WENGER AWEZA WAZI MIKAKATI YAKE.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amesisitiza wataendelea na kanuni yao la kushambulia pamoja na kukosolewa kuwa ndio imechangia kupoteza mechi zao nyingi. Arsenal wamepoteza mechi sita kati ya tisa zilizopita kwenye mashindano yote huku wakiporomoka mpaka nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu. Hatua hiyo imepelekea meneja huyo kuwa katika shinikizo kubwa huku mashabiki wakimtaka kuachia ngazi. Akizungumza na luninga ya Sky Sports, Wenger amesema kwasasa wamebakisha mechi 11 hivyo itakuwa sio busara kubadili kabisa aina yao ya uchezaji. Meneja huyo aliendelea kudai kuwa wachezaji hao hao ndio walioshinda mechi na hao hao pia ndio waliopoteza hivyo anadhani kwasasa wataendelea na aina yao ileile ya kushambuliaji.

KLOPP AMLILIA LALLANA.

MENEJA wa Liverpool, Jurgen Klopp hamlaumu kocha wa timu ya taifa ya Uingereza Gareth Southgate kwa kuumia kwa Adam Lallana lakini hajafurahishwa kwa mshambuliaji huyo kuchezeshwa mechi mbili za kimataifa. Lallana mwenye umri wa miaka 28, aliumia msulu wakati wa mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Lithuania Jumapili iliyopita baada ya kucheza ya kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Ujerumani Machi 22. Nyota huyo anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa muda wa mwezi mzima akianza kwa kukosa mchezo wa derby ya Merseyside kesho. Akizungumza na wanahabari, Klopp amesema hakufurahishwa na Lallana kuchezeshwa mchezo wa Jumatano iliyopita lakini sio kwamb anamlaumu Southgate. Klopp aliendelea kudai kuwa ingekuwa vyema kama waifanya kazi pamoja na kuulizana hili na lile wa manufaa ya pande zote mbili.

CHUNG KUKATA RUFANI CAS.

MAKAMU wa rais wa wa zamani wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA Chung Mong-joon anatarajia kukata rufani kwenye Mahakama ya Michezo ya Kimataifa-CAS kupinga adhabu ya kufungiwa miaka mitano aliyopewa. Chung raia wa Korea Kusini ambaye alikuwa makamu wa rais wa FIFA kuanzia mwaka 1994 mpaka 2011, alikutwa na hatia mwaka 2015 ya kukiuka maadili ya shirikisho hilo wakati Korea Kusini ikitafuta nafasi ya uenyeji wa Kombe la Dunia 2022 miaka saba iliyopita, ambapo Qatar ndio waliopewa uenyeji. Chung anatarajiwa kuzungumzia uamuzi wake huo wa kukata rufani CAS Alhamisi ijayo jijini Seoul. Mapema kamati ya rufani ya FIFA ilipunguza adhabu ya Chung kutoka miaka sita aliyofungiwa awali mpaka mitano, wakitoa sababu kuwa hakukua na ushahidi wa kutosha wa kuvunjwa kwa kanuni hiyo. Mbali na adhabu hiyo ya kufungiwa kujishughulisha na masuala ya michezo, Chung pia alilimwa faini ya dola 49, 940.

PSG KUWAKOSA MARQUINHOS NA KRYCHOWIAK.

BEKI wa kimataifa wa Brazil, Marquinhos na kiungo wa kimataifa wa Poland Grzegorz Krychowiak wanatarajiwa kukosa mchezo wa fainali ya Kombe la Ufaransa ambapo Paris Saint-Germain-PSG watacheza dhidi ya Monaco kesho. PSG walibainisha taarifa hizo mapema leo baada ya kutowajumuisha nyota hao katika orodha ya wachezaji watakaokuwepo kwenye mchezo huo utakaofanyika jijini Lyon. Marquinhos alitolewa wakati wa mapumziko katika ushindi wa mabao 3-0 waliopata Brazil dhidi ya Paraguay baada ya kuzumbuliwa na majeruhi ya nyonga. Krychowiak ambaye pia alikuwa kwenye majukumu ya kimataifa katikati ya wiki, naye aliondoka katika kambi ya Poland kufuatia kuumia mbavu.

Wednesday, March 29, 2017

BARCELONA WASHTUSHWA NA ADHABU ALIYOPEWA MESSI.

KLABU ya Barcelona imetoa taarifa wakidai kushtushwa kwa adhabu ya kufungiwa mechi nne za kimataifa nyota wao Lionel Messi. Messi amelimwa adhabu hiyo kufuatia kumtolea maneno machfu mwamuzi wakati Argentina iliposhinda bao 1-0 katika mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Chile wiki iliyopita. Adhabu hiyo ilitangazwa saa chache kabla ya mchezo wao dhidi ya Bolivia jijini La Paz jana. Kukosekana kwa Messi kumepelekea Argentina kutandikwa mabao 2-0 na kuwafanya kushuka mpaka nafasi ya tano katika msimamo wa nchi za Amerika Kusini-CONMEBOL. Kaika taarifa yake Barcelona wamedai kushtushwa na taarifa hiyo ilitolewa na Kamati ya Nidhamu ya FIFA na kuona haikuwa haki na kuongeza kuwa wanamuunga mkono nyota wao kwenye kipindi hiki.

TEKNOLOGIA YA VIDEO KUMSAIDIA MWAMUZI YAANZA KUONYESHA MATUMAINI.

MFUMO wa teknologia ya video umetumika jana kusahihisha baadhi ya maamuzi katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki ambao Hispania ilifanikiwa kuifunga Ufaransa jijini Paris. Mshambuliaji wa Ufaransa Antoine Griezmann bao lake lilikataliwa kufuatia picha za video za kumsaidia mwamuzi kuamua kwamba alikuwa ameotea. Mfumo huo pia ulikubali bao la pili la Hispania lililofungwa na Gerard Deulofeu baada ya mwamuzi wa pembeni kunyoosha kibendera kuwa alikuwa ameotea. David Silva ndiye aliyefunga bao la kuongoza kwa Hispania kwa penati baada ya Laurent Koscielny kumfanyai madhambi Deulofeu. Teknologia ya kutumia picha za video kumsaidia mwamuzi kwasasa iko katika majaribio, huku rais wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA Gianni Infantino akitaka teknologia hiyo kutumika katika michuano ya Kombe la Dunia nchini Urusi mwakani.

BRAZIL YAWA NCHI YA KWANZA KUFUZU KOMBE LA DUNIA.

BRAZIL imekuwa nchi ya kwanza kufuzu michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2018 jana kufuatia ushindi wa mabao 3-0 waliopata dhidi ya Paraguay. Kikosi cha Brazil kinachonolewa na kocha Tite sasa kinaungana na wenyeji Urusi kuwa timu pekee ambazo mpaka ndizo zenye nafasi ya kushiriki michuano hiyo. Ushindi wa Brazil ulikuwa hautoshelezi kuwapa nafasi hiyo lakini kufungwa kwa Uruguay mabao 2-1 na Peru ndio iliyowapa rasmi nafasi hiyo. Brazil ilipoteza mechi yake ya kwanza ya kufuzu nchi za Amerika Kusini kwa Chile, lakini toka wakati huo wamecheza mechi 13 bila kupoteza na kuwafanya kukaa kileleni wakiwa na alama 33 baada ya kucheza mechi 14, wakishinda 10, sare tatu na kupoteza moja.

Tuesday, March 28, 2017

MESSI AFUNGIWA MECHI NNE.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Argentina, Lionel Messi anatarajiwa kukosa mchezo wa kufuzu michuano ya Kombe la Dunia dhidi ya Bolivia baadae leo baada ya kulimwa adhabu ya kufungiwa mechi nne kwa kumtolea maneno machafu mwamuzi. Uamuzi huo umepelekwa Chama cha Soka cha Argentina saa chache kabla ya kuanza kwa mchezo dhidi ya Bolivia huko jijini La Paz. Hatua hiyo imekuja kufuatia Messi kudaiwa kutumia lugha chafu dhidi ya mwamuzi msaidizi kwenye mchezo wao walioshinda bao 1-0 dhidi ya Chile Ijumaa iliyopita. Nyota huyo wa Barcelona pia ametozwa faini ya paundi 8,100 na anatarajiwa kukosa mechi za kufuzu dhidi ya Uruguay, Venezuela na Peru kabla ya kurejea kwenye mchezo wa mwisho dhidi ya Ecuador. Katika taarifa yake Shirikisho la Soka Duniani-FIFA limedai kuwa kamati yake ya nidhamu ndio ilifikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha na tuhuma zilizotolewa.

RONALDO AMZIDI MESSI KWA KIPATO.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Ureno na klabu ya Real Madrid, Cristiano Ronaldo ndiye mwanasoka anayelipwa zaidi kwa msimu huu wa 2016-2017, akikunja kitita cha euro milioni 87 na kumzidi hasimu wake nyota wa Argentina na Barcelona Lionel Messi anayepata euro milioni 76.5. Kwa mujibu wa taarifa hizo zilizotolewa na jarida maarufu la France Football, Neymar ndiye anayefuatia kwenye nafasi ya tatu akikunja kitita cha euro milioni 55.5 mbele ya nyota wa Wales na Real Madrid Gareth Bale anayepata euro milioni 41. Anayefuatia kwenye orodha hiyo ni nyota mwingine wa kimataifa wa Argentina Ezequial Lavezzi anayepokea kitita cha euro milioni 28.5 katika klabu ya Hebei Fortune ya China. Meneja wa Manchester United Jose Mourinho ndiye meneja anayelipwa zaidi akikunja kitita cha euro milioni 28 kwa mwaka ambapo kiwango hicho kinajumuisha mshahara, marupurupu na kipato cha matangazo mwaka msimu huu.

MAN CITY WALIMWA ADHABU.

KLABU ya Manchester City imelimwa faini ya paundi 35,000 na Chama cha Soka cha Uingereza-FA kwa kushindwa kuwadhibiti wachezaji wake kwenye mchezo wa Liverpool mwezi huu. City walikubali kosa wiki iliyopita baada ya wachezaji kadhaa kupingwa penati waliyopewa Liverpool kwenye mchezo huo uliofanyika Machi 19. Wachezaji hao waliendelea kulalamika hata baada ya James Milner kufunga penati hiyo kwa Liverpool iliyowapa uongozi kwenye mchezo huo uliomalizika kwa sare ya bao 1-1. Katika taarifa yake FA ilidai baada ya tume huru ya kisheria kusikiliza kesi hiyo iliamua kutoa uamuzi wa kuilima faini kufuatia klabu hiyo kukiri kufanya makosa hayo.

UWANJA WA KINA TEVEZ WAWAKA MOTO.

UWANJA wa klabu ya Shanghai Shenhua inayoshiriki Ligi Kuu ya China wa Hongkou umeharibiwa vibaya kufuatia kuungua moto. Hakuna majeruhi wowote walioripotiwa kufuatia tukio hilo lililotokea mapema leo asubuhi. Taarifa zaidi kuhusiana na tukio hilo zinadai kuwa moto haukuathiri majukwaa au sehemu ya kuchezea na uchunguzi unaendelea kufanyika kubaini chanzo chake. Klabu hiyo inayonolewa na Gus Poyet, ilimsajili mshambuliaji wa zamani wa Manchester City Carlos Tevez mwaka jana kwa kitita cha paundi milioni 40. Pia kikosi cha timu hiyo kinajumuisha nyota wengine wa zamani wa Ligi Kuu ya Uingereza akiwemo Demba ban a Obafemi Martin. Ligi Kuu ya China imeanza rasmi mapema mwezi huu huku Shenhua ikitarajiwa kucheza mechi yake inayofuata nyumbani dhidi ya Changhun Yatai Jumapili ya Aprili 16 mwaka huu.

LIVERPOOL KUWAKODIA NDEGE COUTINHO NA FIRMINO.


KLABU ya Liverpool inadaiwa kwa mara nyingine itakodi ndege ili kuwarejesha nyota wake Philippe Coutinho na Roberto Firmino kutoka katika majukumu ya kimataifa. Nyota hao wa kimataifa wa Brazil wanatarajiwa kucheza mechi ya kufuzu michuano ya Kombe la Dunia dhidi ya Paraguay jijini Sao Paulo Alfajiri ya kuamkia kesho hivyo kufanya kuwa na siku mbili pekee za kujiandaa kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu dhidi ya Everton Jumamosi hii. Kama kila kitu kikienda kama kilivyopangwa, Coutinho na Firmino wanatarajiwa kurejea Liverpool kesho kabla ya kuripoti mazoezi Alhamisi hii. Liverpool imeshakodi ndege mara kadhaa msimu huu ili kuhakikisha baadhi ya nyota wake wanaripoti klabuni kwa wakati. Mapema mwezi mwaka huu Sadio Mane alitumiwa ndege ya kukodi kutoka katika michuano ya Mataifa ya Afrika muda mfupi baada ya Senegal kuenguliwa katika michuano hiyo. Novemba mwaka jana taarifa zinadai kuwa Liverpool iligawana gharama za ndege ya kukodi na Manchester City, Chelsea na Paris Saint-Germain ili waweze kuwarejesha nyota wao wa

MECHI YA IVORY COAST NA SENEGAL YAVUNJIKA KUFUATIA VURUGU.

MCHEZO wa kirafiki wa kimataifa wa kati ya Ivory Coast na Senegal ulilazimika kusitishwa kufuatia mashabiki kuvamia uwanjani jijini Paris. Timu hizo zilikuwa zimetoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1 kwenye dakika ya 88 wakati kundi la mashabiki liliporuka uzio na kuingia sehemu ya kuchezea huku shabiki mmoja akionekana kumrukia nyota wa Senegal Lamine Gassama. Wachezaji walilazimikia kukimbia nje ya uwanja na mwamuzi Tony Chapron aliamua kusitisha mchezo huo huku zikiwa zimebaki dakika mbili mpira kumalizika. Bao la Senegal lilifungwa na nyota wa Liverpool Sadio Mane kwa penati huku lile la Ivory Coast likifungwa na Bi Gohi Cyriac. Mmoja wa mashuhuda wa mchezo huo amesema watu hao waliovamia uwanja hawakuwa na nia mbaya bali walitaka kuwa karibu na wachezaji ikiwemo kupiga nao picha lakini ni suala linalotakiwa kutizamwa kwa umakini kwani lolote linaweza kutokea.

Monday, March 27, 2017

ARDA TURAN AUMIA AKIWA KWENYE MAJUKUMU YA KIMATAIFA.

SHIRIKISHO la Soka la Uturuki-TFF limethibitisha kuwa nahodha wa timu ya taifa ya nchi hiyo Arda Turan amepata majeruhi ya nyonga na anatarajiwa kukosa mchezo w kirafiki wa kimataifa dhidi ya Moldova baadae leo. TFF walithibitsiha taarifa kufuatia nyota huyo mwenye umri wa miaka 30 kuachwa katika kikosi cha nchi hiyo baada ya kushindwa kupona kwa wakati. Awali ilikuwa imeripotiwa kuwa majeruhi aliyopata Turan hayakuwa makubwa sana na kulikuwa na uwezekano wa kucheza mchezo wa Jumapili hii wa klabu yake ya Barcelona dhidi ya Granada. Hata hivyo, baada ya kufanyiwa vipimo imegundulika kuwa hataweza kucheza mechi hiyo ya leo ingawa anaweza kupona kwa wakati kwa ajili ya mchezo huo wa La Liga Jumapili.

WENGER HAWEZI KUNIFANYIA HIVI - OZIL.

KIUNGO wa Arsenal, Mesut Ozil amesema haamini kama kuna ukweli wowote juu ya taarifa kuwa meneja Arsene Wenger anataka kumuuza. Gazeti la Daily Express liliripoti wiki iliyopita kuwa Ozil na Alexis sanchez wanaweza kuuzwa na Wenger kufuatia nyota hao kuwa bado hawajaongeza mikataba ambayo inatarajiwa kumalizika mwaka 2018. Akizungumza na wanahabari kuhusiana na suala hilo, Ozil amesema hadhani kama taarifa hizo zina ukweli wowote kwani Wenger asingeweza kusema taarifa hizo bila kumshirikisha. Nyota huyo wa zamani wa Real Madrid aliendelea kudai kuwa bado anafurahia kuwepo Arsenal lakini kwasasa kuna kitu hakiendi sawa kwa timu ndio maana wamekuwa hawapati matokeo mazuri. Hata hivyo, Ozil anaamini upepo huo mbaya utapita na watarejea katika makali yao hivi karibuni.

KATIBU MKUU WA CAF ABWAGA MANYANGA.

KATIBU mkuu wa Shirikisho la Soka la Afrika-CAF, Hicham El Amrani amejiuzulu wadhifa wake huo jana, ikiwa imepita wiki moja baada ya rais aliyedumu kwa kipindi kirefu Issa Hayatou kushindwa kwenye uchaguzi na Ahmad Ahmad wa Madagascar. Katika barua yake ya kujiuzulu kwa CAF, El Amrani amesema ataondoka rasmi leo lakini hajatoa sababu zozote kwa uamuzi wake huo. El Amrani mwenye umri wa miaka 37 raia wa Morocco amekuwa katibu mkuu wa shirikisho hilo kwa kipindi cha miaka sita iliyopita. Hayatou aliondolewa kwenye nafasi ya urais wa CAF siku 10 zilizopita katika uchaguzi uliofanyika huko Ethiopia, ambapo wajumbe sita wa kamati ya utendaji waliokuwa wakimuunga mkono kwenye uchaguzi huo nao pia walipoteza naafsi zao. Hayatou mwenye umri wa miaka 70 ameingoza CAF kwa kipindi cha miaka 29.

NIMETIMIZA NDOTO ZANGU KWA KUFUNDISHWA NA BABA - DALEY BLIND.

BEKI wa kimataifa wa Uholanzi na Manchester United, Daley Blind amesema kucheza chini ya baba yake Danny ilikuwa ni moja ya ndoto zake pamoja na kocha huyo wa timu ya taifa ya nchi hiyo kutimuliwa. Uholanzi chini Danny Blind ilijikuta ikitandikwa mabao 2-0 na Bulgaria Jumamosi iliyopita na kuiacha nchi hiyo kwenye hatari ya kutofuzu michuano mikubwa kwa mara ya pili mfululizo. Blind mwenye umri wa miaka 55 alichukua nafasi ya Guus Hiddink mwaka 2015 lakini alishindwa kuiwezesha nchi hiyo kufuzu michuano ya Ulaya iliyofanyika nchini Ufaransa kiangazi mwaka jana. Fred Grim ndio anatarajiwa kuchukua mikoba ya muda wakati Uholanzi itakapovaana na Italia kesho. Akizungumza na wanahabari kuhusu kutimuliwa kwa baba yake, Daley amesema kufanya kazi naye katika viwango vya juu ilikuwa ndoto yake kubwa na imetimia hivyo anajivunia.

Friday, March 24, 2017

POLISI WAKAMATA COCAINE ILIYOKUWA IMEWEKEWA PICHA YA MESSI.

POLISI nchini Peru wamekamata kilo 1,417 za cocaine jana, nyingi kati ya hizo zikiwa zimefungwa na kuwekwa picha ya mshabuliaji nyota wa kimataifa wa Argentina na klabu ya Barcelona Lionel Messi. Mzigo huyo wa madawa ya kulevywa unaokadiriwa kuwa thamani ya dola milioni 85, ulikamatwa ukiwa umefungwa kwenye vishurushi ambavyo juu yake waliweka picha ya Messi akiwa na jezi ya Barcelona. Polisi nchini humo wamedai kuwa madawa hayo yalikuwa yakisafirishwa kupelekwa nchini Ubelgiji. Hii ni mara ya pili kwa shehena kubwa ya madawa ya kulevya kukamatwa nchini Peru ya kwanza ikiwa ni Januari wakati polisi walipokamata madawa yenye zaidi ya thamani ya dola milioni 174.

NAJUTA KUTOCHEZA NA RONALDO - TOTTI.

NGULI wa soka wa AS Roma, Francesco Totti amebainisha kuwa utambulisho wake wa kuwa mtu wa klabu moja uliingia katika tishio wakati Real Madrid walipomuwania na anajuta kutocheza sambamba na nguli wa Brazil Ronaldo De Lima. Totti mwenye umri wa miaka 40 ametumia kipindi cake chote cha soka kucheza kwenye klabu hiyo inayotoka katika mji mkuu wa Italia Rome, akicheza karibu mechi 800 kwa kipindi chote. Hata hivyo, aliwahi kupata nafasi ya kwenda kutafuta changamoto nyingine mpya wakati wakiwa kwenye kiwango juu huku Madrid ikiwa timu mojawapo iliyomuwania. Akizungumza wakati wa mahojiano nchini Italia, Totti amesema miaka mingi iliyopita alikaribia kujiunga na Madrid lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na heshima kubwa aliyokuwa nayo kwa mashabiki wa Roma. Totti aliendelea kudai kuwa kikubwa anachojutia ni kushindwa kucheza na Ronaldo pamoja na kutotwaa taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa na Roma.

DELE ALLI AFUNGIWA MECHI TATU NA UEFA.

KIUNGO wa Tottenham Hotspurs, Dele Alli amefungiwa mechi tatu na Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA baada ya kupewa kadi nyekundu katika mchezo wa Europa League dhidi ya Gent. Kiungo huyo wa kimataifa wa Uingereza, alitolewa nje kwa kosa la kumkwatua Brercht Dejaegere wakati wa kipindi cha kwanza cha mchezo huo wa hatua ya 32 bora dhidi ya klabu hiyo ya Ubelgiji. Wakati timu hizo zikiwa sare ya bao 1-1, Alli alimkwatua mwenye goti Dejaegere na kumuacha mwamuzi wa mchezo huo Manuel de Sousa bila chaguo zaidi ya kumpa kadi nyekundu. Mchezo huo ulimalizika kwa sare ya mabao 2-2 na kuwafanya Spurs kutolewa nje ya mashindano hayo kwa jumla ya mabao 3-2. Pamoja na kutolewa Alli atalazimika kuitumikia adhabu yake ya kutocheza mechi katika michuano ijayo ya Ulaya ya vilabu kama Spurs wakifanikiwa kufuzu.

RUNGU LA UEFA LAINGUKIA ARSENAL NA BAYERN.

KLABU za Arsenal na Bayern Munich zimelimwa adhabu na Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA kufuatia mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baina ya timu hizo uliochezwa mwanzoni mwa mwezi huu. Arsenal wakiwa nyuma ya mabao 5-1 waliyofungwa katika mchezo wa mkondo wa kwanza nchini Ujerumani, walipokea kipigo kingine kama hicho kwenye Uwanja wa Emirates Machi 7 mwaka huu na kutolewa nje ya michuano hiyo. Klabu zote mbili zimelimwa adhabu na UEFA kwa matukio mawili tofauti ambapo Arsenal wao wametozwa faini ya euro 5,000 baada ya mashabiki kadhaa kuvamia uwanjani wakati Bayern wao wametozwa faini ya euro 3,000 kufuatia vitu vilivyorushwa na mashabiki wao uwanjani. Kipigo hicho cha Arsenal kwenye mchezo huo kiliongeza shinikizo kwa mashabiki wake kumtaka meneja Arsene Wenger kuondoka kufuatia kutofanya vyema kwenye mechi zao kadhaa huku wakitolewa katika hatua ya 16 ya michuano hiyo kwa mara ya saba mfululizo.

BECKENBAUER AWEKWA MTU KATI USWISI.

NGULI wa soka wa Ujerumani, Franz Beckenbauer amehojiwa na waendesha mashitaka nchini Uswisi juu ya tuhuma za ufisadi katika Kombe la Dunia mwaka 2006. Beckenbauer amekuwa akichunguzwa sambamba na wajumbe watatu wengine waliokuwepo katika kamati ya maandalizi ya michuano hiyo. Wanne hao wanatuhumiwa kwa udanganyifu, usimamizi mbaya wa kijinai, kutakatisha fedha na ubadhilifu. Beckernbauer ambaye aliongoza kamati hiyo mwaka 2000 amekanusha tuhuma zozote za rushwa katika kinyanyiro hicho cha kutafuta uenyeji wa michuano hiyo.

Tuesday, March 21, 2017

YANGA WAPANGWA NA WAARABU SHIRIKISHO.

MABINGWA wa soka Tanzania Bara, Yanga wamepangwa kucheza na klabu ya MC Alger ya Algeria katika hatua ya mtoano ya timu 32 za bora katika michuano ya Kombe la Shirikisho katika ratiba iliyopangwa Makao Makuu ya Shirikisho la Soka la Afrika, Cairo, Misri. Ratiba hiyo ilijumuisha timu 16 zilizovuka hatua ya mtoano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya timu 16 zilizotolewa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika. Yanga iliangukia katika michuano hiyo kufuatia kutolewa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kufuatia sare ya bila kufungana na Zanaco ya Zambia mwishoni mwa wiki iliyopita na kuwafanya kutolewa kwa bao la ugenini kufuatia sare ya bao 1-1 waliyopata katika mchezo wa awali uliofanyika jijini Dar es Salaam. Katika hatua hiyo Yanga inatarajiwa kuanza mchezo wake wa mkondo wa kwanza nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku mchezo wa marudiano ukitarajiwa kuchezwa wiki moja baadae huko Algeria. Kwa mujibu wa ratiba iliyotoka leo mechi za mkondo wa kwanza zinatarajiwa kuchezwa kati ya Aprili 7 na 9 huku zile za marudiano zikichezwa kati Aprili 14 na 16.

RAIS MPYA CAF AANZA KUPUNGUZA VYEO ANAVYOSHIKILIA ILI KUKIDHI MASHARTI.

RAIS mpya wa Shirikisho la Soka la Afrika-CAF, Ahmad Ahmad amejizulu wadhifa wake kama makamu wa rais wa baraza la seneti nchini Madagascar. Ahmad ambaye pia ni rais wa Shirikisho la Soka la Madagascar-MFF, aliachia wadhifa huo mapema jana baada ya kudumu toka Februari mwaka 2016. Ahmad mwenye umri wa miaka 57 na kocha wa zamani wa klabu ya AC Sotema, alipokelewa rasmi na maofisa wa MFF na jamii ya Kiislamu katika hoteli ya Carlton jijini Antananarivo ambako alihutubia waliohudhuria. Alhamisi iliyopita Ahmad alichaguliwa kuwa rais mpya wa CAF kwa kupata kura 34 dhidi ya 20 za rais aliyemaliza muda wake Issa Hayatou ambaye alikaa madarakani kwa kipindi cha miaka 29. Ahmad ambaye pia amewahi kushikilia nafasi ya uwaziri kwa vipindi viwili tofauti nchini kwake, pia anategemewa kuachia nafasi yake kama rais wa MFF kama sheria za CAF zinavyotaka.

RONALDO ATWAA TUZO NYINGINE.

MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwaka 2016 wa Ureno baada ya kuiongoza nchi yake kutwaa taji lao la kwanza la michuano ya Ulaya akiangazi mwaka jana. Ronaldo aliwashinda mchezaji mwenzake wa Madrid Pepe na kipa wa Sporting Lisbon Rui Patricio katika kinyang’anyiro hicho. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 32 aliiongoza Madrid kushinda taji lake la 11 la michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya Mei mwaka jana kwa kufunga penati ya ushindi dhidi ya mahasimu wao Atletico Madrid huku akimaliza kama mfungaji bora kwa mabao yake 16. Ingawa Ronaldo aliumia mapema katika mchezo wa fainali ya michuano ya Ulata dhidi ya wenyeji Ufaransa, Ureno ilijitutumua na kushinda mchezo huo kwenye dakika za nyongeza na kutwaa taji lao la kwanza kubwa katika historia. Akizungumza na wanahabari, Ronaldo amesema umekuwa mwaka mzuri na muhimu kwasababu michuano ya Ulaya ndio ilikuwa pekee ambayo hajawahi kushinda.

VARDY ADAI KUPOKEA VITISHO VYA KUUAWA.

MSHAMBULIAJI wa Leicester City, Jamie Vardy amesema amekuwa akipokea vitisho vya kuuawa na familia yake ikilengwa toka meneja Claudio Ranieri alipotimuliwa. Nyota huyo mwneye umri wa miaka 30 analaumu tuhuma mbaya na za uongo kuwa ndiye aliyelazimisha klabu hiyo kufikia uamuzi wa kumtimua meneja huyo raia wa Italia. Ranmieri aliondoka Febrauri, miezi tisa baada ya kushinda taji la Ligi Kuu, huku klabu ikiw nafasi ya 17 katika msimamo ambapo nafasi yake ilishikiliwa na msaidizi wake Craig Shakespeare. Akizungumza na wahabari, Vardy amesema ni jambo linalotisha kwani alisoma habari moja kuwa alikuwepo katika mkutano baada ya mechi dhidi ya Sevilla na kushinikiza kutimuliwa kwa Ranieri. Vardy aliendelea kudai kuwa anasikitika kwasababu hakuwepo katika kikao hicho na hakuhusika na chochote katika uamuzi wa klabu uliochukua.

SCHWEINSTEIGER ATIMKIA MAREKANI.

KLABU ya Manchester United, imekubali kumuacha Bastian Schweinsteiger kujiunga na timu ya Chicago Fire inayoshiriki Ligi Kuu ya Soka ya Marekani-MLS. Kiungo huyo wa kimataifa wa Ujerumani mwenye umri wa miaka 32, amesaini mkataba wa mwaka mmoja na klabu hiyo. Katika taarifa yake, Schweinsteiger amesema siku zote amekuwa akiangalia nafasi ambayo anaweza kufanya kitu cha kusaidia na kutengeneza kitu kikubwa ndio maana ameamua kwenda Chicago Fire. Nahodha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Ujerumani na mshindi wa Kombe la Dunia alikuwa akifanya mazoezi mwenyewe na kikosi cha vijana chini ya umri wa miaka 23 akiwa United baada ya Jose Mourinho kuchukua mikoba ya kuinoa timu hiyo kiangazi mwaka jana. Hata hivyo, alirejea katika kikosi cha kwanza kabla ya mchezo wa Europa League dhidi ya Fenernahce Novemba mwaka jana na kucheza mechi yake ya kwanza kweney mchezo wa Kombe la EFL dhidi ya West Ham United.

Friday, March 17, 2017

GENK YA SAMATTA KUCHEZA NA CELTA VIGO EUROPA LEAGUE.

KLABU ya Genk ya Ubelgiji anayocheza nyota wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta imepangwa kucheza na Celta Vigo katika hatua ya robo fainali ya michuano ya Europa League. Genk ilitinga hatua hiyo kwa kishindo baada ya kuwagaragaza Wabelgiji wenzao Gent kwa jumla ya mabao 6-3, huku Samatta akifunga mabao mawili katika mchezo wa mkondo wa kwanza walioshinda mabao 5-2. Katika hatua nyingine Manchester United wanaopewa nafasi kubwa ya kutwaa taji hilo wao wamepangwa kucheza na Anderlecht ya Ubelgiji huku Olympique Lyon wakicheza na Besiktas na Ajax Amsterdam wakipepetana na Schalke 04. Mechi za mkondo wa kwanza zinatarajiwa kuchezwa Aprili 13 huku zile za marudiano zikifuatia wiki moja baadae.

MADRID KUWAVAA WABABE WA ARSENAL ULAYA.

MABINGWA watetezi Real Madrid wanatarajia kupambana na Bayen Munich, wakati Barcelona wakipangwa kucheza na Juventus katika ratiba ya robo fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Kwa upande mwingine mabingwa wa Ligi Kuu Uingereza Leicester City wao wamepangwa kuchuana na Atletico Madrid huku Borussia Dortmund wakipepetana na AS Monaco waliotinga hatua hiyo baada ya kuitoa Manchester City katika 16 bora. Madrid ambao walitinga hatua hiyo baada ya kuitoa AS Napoli watakabiliwa na kibarua kizito mbele ya Bayern iliyoifurumusha Arsenal kwa jumla ya mabao 10-2 katika mechi mbili walizokutana. Kwa upande wa Barcelona wanaweza mwaka hu unaweza kuwa mzuri kwao kwani walitinga hatua hiyo kwa kuweka historia ya kipekee ya kutoka nyuma wakiwa wamefungwa mabao 4-0 na kutinga hatua hiyo kufuatia ushindi wa mabao 6-1. Juventus kwa upande wao waliitoa FC Porto kwa jumla ya mabao 3-0 wakati Leicester walijiwekea historia ya kutinga hatua hiyo kwa kuiondosha Sevilla. Mechi za mkondo wa kwanza zinatarajiwa kuchezwa Aprili 11 na 12 huku zile za marudiano zikipangwa Aprili 18 na 19.

YAYA TOURE ANOGEWA MAN CITY.

KIUNGO wa Manchester City, Yaya Toure amesema Pep Guardiola ni sababu kubwa ya yeye kufanikiwa kurejea katika kiwnago chake na anataka kuendelea kubaki Etihad baada ya msimu huu. Nyota huyo aliachwa katika mipango ya City mwanzoni mwa msimu baada ya kutokea msuguano baina yake na Guardiola hali ambayo ilitishia mustakabali wake. Hata hivyo, Toure aliejeshwa katika kikos cha kwanza baada ya kuomba radhi kwa meneja huyo na sasa anataka kuendelea kubakia klabuni hapo baada ya mkataba wake wa sasa kumalizika. Akizungumza na wanahabari, Toure amesema anaipenda City na bado anapenda kuendelea kuitumikia mpaka pale atakapohisi mwili wake umefikia ukingoni.

FIFA YAIPIGA KUFULI MALI.

CHAMA cha Soka cha Mali-Femafoot kimesimamishwa na Shirikisho la Soka Duniani-FIFA mpaka itakapoamuliwa vinginevyo kufuatia serikali ya nchi hiyo kuingilia masuala ya soka. FIFA imechukua hatua hiyo baada ya Waziri wa Michezo wa Mali Housseini Amion Guindo kuvunja kamati ya utendaji ya Femafoot. Guindo pia aliteua kamati ya muda iliyopewa mamlaka ya kuongoza Femafoot mpaka uchaguzi mwingine utakapofanyika ndani ya miezi 12. Katika taarifa yake FIFA imedai kuwa marufuku hiyo itaondoshwa wakati bodi ya Femafoot iliyokuwepo awali itakaporejeshwa madarakani. FIFA iliendelea kudai hakuna timu yeyote kutoka Mali zikiwemo klabu zitakazoruhusiwa kushiriki michuano ya kimataifa kuanzia leo.

Thursday, March 16, 2017

AHMAD AHMAD RAIS MPYA CAF, ZANZIBAR WAUKWAA UANACHAMA.

RAIS wa Shirikisho la Soka la Madagascar, Ahmad Ahmad amefanikiwa kuchaguliwa kuwa rais mpya wa Shirikisho la Soka la Afrika-CAF akimshinda mpinzani wake Issa Hayatou wa Cameroon. Ahmad alishinda uchaguzi huo kwa kuzoa jumla ya kura 34 kati ya kura 54 za wajumbe huku mpinzani wake Hayatou ambaye ameiongoza CAF toka mwaka 1988 akiambulia kura 20. Uchaguzi huo umefanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia ambapo pamoja na mambo mengine Chama cha Soka cha Zanzibar-ZFA hatimaye nacho kimefanikiwa kupata uanachama rasmi CAF. ZFA ilikuwa imetuma maombi ya kutambuliwa kama mwanachama rasmi wa CAF na baada ya jopo la wajumbe wa mkutano huo kukutana walipitisha kwa kauli moja kulikubali ombi hilo la Zanzibar. Sasa CAF ambayo ilikuwa na wanachama 54 hapo awali kabla ya mkutano, itakuwa na jumla ya wanachama 55 huku Zanzibar wakiwa wanachama wapya.

Wednesday, March 15, 2017

CAF YAMFUNGULIA MASHITAKA YA KINIDHAMU CHIYANGWA.

SHIRIKISHO la Soka la Afrika-CAF linatarajia kumfungulia mashitaka ya kinidhamu dhidi ya rais wa Baraza la Soka la Nchi za Kusini mwa Afrika-Cosafa, Phillip Chiyangwa. Chiyangwa amekuwa akimponda Issa Hayatou na kujinasibu kuwa yeye ndiye kampeni meneja wa rais wa shirikisho la Soka la Madagascar, Ahmad Ahmad ambaye anashindana na Hayatou katika uchaguzi mkuu wa kesho. CAF imedai kuwa hatua za hivi karibuni zilizofanywa na Chiyangwa na kauli zinaonyesha kulikosea heshima shirikisho hilo, rais wake na wajumbe wa kamati ya utendaji. CAF imeamua kufungua kesi dhidi ya Chiyangwa mabaye ni rais wa Shirikisho la Soka la Zimbabwe katika kikao chao cha kamati ya utendaji kilichokutana jijini Addis Ababa, Ethiopia jana ikiwa zimebaki siku mbili kabla ya uchaguzi.

FIFA YAMPIGA KITANZI CHABUR.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA limemuengua rais wa zamani wa Shirikisho la Soka la Sudan Kusini Chabur Alei kugombea nafasi ya ujumbe katika baraza la shirikisho katika uchaguzi utakaofanyika Machi 16 mwaka huu jijini Addis Ababa. Akuzungumza na wanahabari, Chabur amesema Shirikisho la Soka la Afrika-CAF lilimuarifu kuhusu uamuzi huo wa FIFA ingawa hajapokea nyaraka yeyote ya maandishi. Hata hivyo, Chabur aliendelea kudai kuwa amekubaliana na maamuzi hayo na kama binadamu anafahamu utakuwepo wakati mwingine atakaopata nafasi nyingine. Chini ya sheria mpya za FIFA, mtu yeyote ambaye anashikilia au anataka kushikilia nafasi katika shirikisho hilo anatakiwa kufaulu uchunguzi wa kimaadili kabla ya uchaguzi.

UWANJA ALIOULALAMIKIA MOURINHO WAFUNGIWA.

WIKI moja baada ya Jose Mourinho kuponda sehemu ya kuchezea, Ligi Kuu ya Urusi imeufungia uwanja wa FC Rostov kutumika katika mechi zake za ligi kufuatia nyasi zake kuharibika. Manchester United ilitoka sare ya bao 1-1 katika Uwanja wa Olimp-2 katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa Europa League hatua ya 16 bora Alhamisi iliyopita. Akizungumza na wanahabari kabla ya mchezo huo, Mourinho alidai ni vigumu kwake kuamini atakwenda kuwa wanakwenda kucheza katika uwanja kama ule. Rostov sasa wamepewa mpaka Machi 24 kuuboresha uwanja wao huo kabla ya kuruhusiwa kuutumia tena kwa ajili ya mechi zao za ligi. United itavaana na United katika mchezo wa mkondo wa pili wa Europa League utakaofanyika Uwanja wa Old Trafford.

GOTZE NJE MSIMU WOTE.

KLABU ya Borussia Dortmund imethibitisha kuwa maradhi ya Mario Gotze yatamuweka nje ya uwanja mpaka mapema msimu ujao. Mapema Februari ilitangazwa kuwa nyota huyo wa kimataifa wa Ujerumani, ambaye alifunga bao la ushindi katika fainali ya Kombe la Dunia mwaka 2014, angekuwa nje ya uwanja kwa muda uziojulikana kutokana na maradhi yanayomsumbua. Lakini Dortmund ambao wiki iliyopita walifuzu hatua ya robo fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, sasa wamebainisha kuwa nyota huyo mwenye umri wa miaka 24 hataweza kurejea tena msimu huu. Katika taarifa yake, Dortmund wamesema lengo lao kubwa ni kwa mchezaji huyo kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya msimu ujao.

MBIVU NA MBICHI KWA HAYATOU KUJULIKANA KESHO.

RAIS wa Shirikisho la Soka la AFrika-CAF, Issa Hayatou anatarajiwa kukabiliwa na upinzani mkubwa wakati akitafuta nafasi ya kuongoza kwa kipindi cha nane shirikisho hilo katika Mkutano Mkuu utakaofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia kesho. Ahmad waziri wa serikali ya Madagascar ambaye anatumia jina moja ndio anatarajiwa kutoa upinzani kwa Hayatou katika uchaguzi akiwa ni mgombea wa tatu kushindana naye toka achaguliwe kuingoza CAF kwa mara ya kwanza mwaka 1988. Wagombea wengine waliowahi kugombea na Hayatou ni pamoja na Armando Machado wa Angola mwaka 2000 na Ismail Bhamjee wa Botswana mwaka 2004. Hata hivyo, Ahmad anakuwa mgombea wa kwanza kuungwa mkono na idadi kubwa ya wajumbe wa CAF likiwemo Baraza la Soka la nchi za Kusini mwa Afrika-COSAFA lenye wajumbe 14 pamoja na Nigeria.

Tuesday, March 14, 2017

HASSAN KABUNDA NDIO MCHEZAJI BORA WA MWEZI FEBRUARI.

KIUNGO mshambuliaji wa Mwadui FC, Hassan Salum Kabunda amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa mwezi Februari, mwaka huu. Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas Mapunda amesema leo katika Mkutano na Waandishi wa Habari mjini Dar es Salaam kwamba, Kabunda amewapiku washambuliaji wa Simba, Mrundi Laudit Mavugo na mzalendo Ibrahim Hajibu baada ya mechi tatu za Februari kushinda tuzo hiyo. Hassan Salum Kabunda ndiye Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa mwezi Februari, mwaka huu “Kabunda amecheza dakika 270 katika mechi tatu ambazo Mwadui wameshinda mbili na kupoteza mechi moja, hivyo kujikusanyia pointi 6 na kupanda kutoka nafasi ya nane hadi ya sita,”amesema Mapunda. Lucas amesema mtoto huyo wa beki wa zamani wa Yanga na timu ya taifa, Taifa Stars, Salum Kabunda enzi zake akiitwa Ninja au Msudan, katika mechi hizo tatu alifunga mabao manne kati ya sita ambayo Mwadui ilifunga. Na kwa ushindi huo, Kabunda atazawadia Sh. Milioni 1 na wadhamini wa Ligi Kuu, kampuni ya Vodacom.

MWENYEKITI WA BAYERN AFUTA NDOTO ZA MAN CITY.

MWENYEKITI wa Bayern Munich, Karl-Heinz Rummenigge ameondoa uwezekano wa kumuuza Joshua Kimmich kwenda Manchester City. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 22 alikuwa akipata nafasi kwenye kikosi cha kwanza chini ya Pep Guardiola alipokuwa Allianz Arena msimu uliopita lakini hivi sasa amekuwa akipaa nafasi chache toka Carlo Ancelotti apewe mikoba. Kimmich alikuwa benchi katika mchezo wa Bundesliga walioshinda 3-0 dhidi ya Entracht Frankfurt mwishoni mwa wiki iliyopita na baadae kukiri suala la kukosa nafasi linaanza kumyima raha. Kufuatia hali tetesi zimekuwa zikiibuka kuwa Guardiola anaweza kumpeleka Etihad msimu ujao lakini Rummenigge amesisitiza kuwa wana mipango mikubwa na beki huyo hivyo hawataweza kumuuza kwasasa. Rummenigge amesema wana mipango mikubwa ya baadae kwa Kimmich kwani wanataka achukue nafasi ya Philipp Lahm anayetarajiwa kutundika daruga zake mwishoni mwa msimu huu.

JUVENTUS KUMCHUKUA SPALLETTI KAMA ALLEGRI AKIAMUA KUONDOKA.

KLABU ya Juventus bado inaendelea na jitihada kumshawishi Massimiliano Alegri kuendelea kubakia jijini Turin lakini wanaweza kumchukua Luciano Spalletti kama meneja huyo wa sasa akiamua kuondoka mwishoni mwa msimu. Mkataba wa Allegri unamalizika Juni 30 mwaka 2018 na Juventus wamekuwa wakifurahishwa na meneja huyo wa zamani wa AC Milan ambaye amefanikiw kushinda mataji mawili mfululizo ya Serie A toka achukue mikoba kiangazi 2014. Pande zote mbili zimeendelea kuwa na mahusiano mazuri ya kikazi na bodi ya Juventus bado ina matumaini ya kumbakisha meneja huyo katika klabu hiyo. Hata hivyo, Allegri bado ana wazo la kujaribu bahati yake nje ya Italia kutokana na kuwa tayari ameshinda mataji matatu la Serie A akiwa na Milan na Juventus. Hivi karibuni kumekuwa na tetesi kuwa Arsenal inaweza kumuwania kufuatia meneja wake Arsene Wenger kuwa katika shinikizo kubwa hivi sasa.

TORRES KUREJEA UWANJANI KESHO.

MSHAMBULIAJI nyota wa Atletico Madrid, Fernando Torres anategemewa kurejea ikiwa zimepita wiki mbili pekee baada ya kuzimia kufuatia kugongwa kichwani, wakati kikosi chao kikijaribu kutafuta nafasi ya kutinga hatua ya robo fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kesho. Atletico wanapewa nafasi kubwa ya kusonga mbele kwa mwaka wan ne mfululizo kufuatia kushinda mabao 4-2 katika mchezo wao wa mkondo wa kwanza dhidi ya Bayer Leverkusen wiki tatu zilizopita. Torres amerejea mazoezini kwa mara ya kwanza Jumatatu toka alipozimia kufuatia kugongana na Alex Bergantinos wa Deportivo La Coruna. Akizungumza na wanahabari, Diego Simeone amesema wana imani Torres atakuwa fiti kwa ajili ya mchezo huo.

ARSENAL KURUDIANA NA BAYERN NCHINI CHINA.

KLABU ya Arsenal imethibitisha kuwa watacheza mchezo wa kirafiki na Bayern Munich nchini China Julai mwaka huu. Arsenal watavaana na wababe wao hao waliowatoa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya jijini Shanghai Julai 19 kabla ya kuja kukutana na Chelsea siku tatu baadae jijini Beijing katika Uwanja wa Bird’s Nest. Mpambano huo unaweza kuwa nafasi kwa Arsenal kulipa kisasi kufuatia kufungwa jumla ya mabao 10-2 na mabingwa hao wa Ujerumani katika mechi za mikondo miwili za michuano ya Ulaya. Ofisa mkuu wa Arsenal, Ivan Gazidis amesema mchezo huo utakuwa maalumu kwa ajili ya mashabiki wao wa China. Gazidis aliendelea kudai kuwa kumekuwa na mashabiki wengi nchini humo ndio maana wameamua kwenda kucheza mechi hizo mbili za kirafiki huko ili kuwazogezea burudani wanayoikosa.

MOURINHO AWAJIBU MASHABIKI WA CHELSEA BAADA YA KUMZOMEA.

MENEJA wa Manchester United, Jose Mourinho amewaambia mashabiki wa Chelsea kuwa bado yeye ni namba moja baada ya kuzomewa wakati wa mchezo wao wa Kombe la FA katika Uwanja wa Stamford Bridge. Mourinho aliyetimuliwa mara mbili Chelsea, aliitwa Yuda wakimaanisha msaliti na mashabiki wakati United ilipotandikwa bao 1-0, na yeye kujibu kwa kuonyesha vidole vitatu akimaanisha mataji matatu aliyoshinda. Mourinho amesema mpaka wana meneja mmoja aliyewasaidia kushinda mataji manne ya Ligi Kuu hivyo bado yeye namba moja. Meneja huyo aliendelea kudai kuwa mpaka hapo itakavyobadilika vinginevyo, Yuda ataendelea kuwa namba moja.

RATIBA NUSU FAINALI FA CUP.

KLABU ya Chelsea mepangwa kucheza na mahasimu wao kutoka London Tottenham Hotspurs katika hatua ya nusu fainali ya michuano ya Kombe la FA. Arsenal ambao wanatarajia kuweka rekodi kwa kucheza nusu fainali yao ya 29 ya michuano hiyo, wao watapambana na Manchester City. Mechi zote mbili za nusu fainali zitachezwa katika Uwanja wa Wembley mwishoni mwa wiki inayoangukia Aprili 22 na 23 mwaka huu. Chelsea waliwang’oa Manchester United kwa kuifunga bao 1-0 jana, huku Spurs wakiitoa timu ya daraja la kwanza ya Millwall Jumapili iliyopita. Arsenal wao ambao ni mabingwa wa mwaka 2014 na 2015 katika michuano hiyo, waliwatoa Loncoln City Jumamosi iliyopita huku City nao wakiingia hatua hiyo kwa mara ya kwanza baada ya kupita miaka minne kwa kuichapa Middlesbrough mabao 2-0.

Friday, March 10, 2017

KANE NDIO MCHEZAJI BORA WA FEBRUARI.

MSHAMBULIAJI wa Tottenham Hotspurs, Harry Kane ameteuliwa kuwa mchezaji bora wa mwezi Februari wa Ligi Kuu baada ya kufunga mabao manne katika mechi tatu alizocheza. Kane ndio anaongoza kwa ufungaji katika ligi akiwa na mabao 19, akimzidi bao moja Romelu Lukaku wa Everton na mabao yake yameisaidia Spurs kukaa kwenye nafasi ya pili katika msimamo wa ligi nyuma ya vinara Chelsea. Akizungumza na wanahabari, Kane amesema ni heshima kubwa kutwaa tuzo hiyo na umekuwa mwezi mzuri kwake pamoja na timu yake. Kwa upande mwingine meneja wa Manchester City, Pep Guardiola ametwaa tuzo ya kocha bora wa mwezi kufuatia kuisaidia timu yake kushinda mechi tatu mwezi uliopita, ikiwemo ile ya mabao 4-0 dhidi ya West ham United, mabao 2-1 dhidi ya Swansea City na mabao 2-0 dhidi ya Bournemouth. Naye mshambuliaji wa Chelsea Eden Hazard ametwaa tuzo ya bao bora la mwezi ambalo alifunga katika mchezo walioshinda mabao 3-0 dhidi ya Arsenal.

CAF CHAMPIONS LEAGUE: YANGA KUIVAA ZANACO.

MABINGWA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga baadae leo wanatarajiwa kujitupa uwanjani kukwaana na Zanaco FC ya Zambia katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika utakaofanyika katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Yanga wamepata nafasi hiyo baada ya kuiondosha Ngaya de Mbe ya Comoro katika mzunguko wa awali na sasa wanacheza na Zanaco kutafuta nafasi ya kutinga hatua ya makundi ya michuano hiyo mikubwa kabisa Afrika. Mchezo huo wa leo ambao utakuwa wa mkondo wa kwanza kabla ya ule wa marudiano utakaofanyika jijini Lusaka, unatarajiwa kuwa wa aina yake haswa kutokana na kocha wa Yanga George Lwandamina kuwa raia wa Zambia. Mbali na uraia lakini pia kocha huyo kabla ya kutua Yanga alikuwa akiinoa klabu ya Zesco United inayoshiriki Ligi Kuu ya Zambia hivyo kumfanya kuwafahamu zaidi Zanaco.

SAMATTA AWA GUMZO ULAYA.

KLABU ya Genk bado wana hofu na Gent kuelekea katika mchezo wao wa mkondo wa pili hatua ya 16 bora ya Europa League pamoja na ushindi mnono wa mabao 5-2 waliopata jana. Katika mchezo huo, mshambuliaji nyota wa kimataifa wa Tanzania Mbwana Samatta alifunga mabao mawili katika dakika ya 41 na 72 na kuipa Genk ushindi huo mnono wa mkondo wa kwanza. Hata hivyo, meneja wa Genk Albert Stuivenberg amesema pamoja na ushindi huo lakini hawapaswi kubweteka kwani wapinzani wao Gent bado wanaweza kubadili matokeo hayo na kutolewa mfano Barcelona. Barcelona walitinga hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya juzi kufuatia kuifunga Paris Saint-Germain kwa mabao 6-1 katika mchezo wa marudiano uliofanyika Camp Nou baada ya kupoteza mchezo wa kwanza kwa mabao 4-0 kule Ufaransa. Stuivenberg amesema waliona kitu cha kipekee kwa Barcelona, lakini kinaweza kutokea tena katika soka hivyo lazima wajindae kikamilifu kuhakikisha wanalinda ushindi wao kwenye mchezo wa marudiano.

RAKITIC AONGEZWA MKATABA BARCELONA.

KIUNGO wa Barcelona Ivan Rakitic ameongeza mkataba mwingine wa kuitumikia klabu hiyo ambao utamalizika mwaka 2021. Rakitic mwenye umri wa miaka 28, alianza katika mchezo wa juzi ambao Barcelona walitoka nyuma wakiwa wamefungwa mabao 4-0 kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kabla ya kupindua matokeo na kushinda mabao 6-1 dhidi ya Paris saint-Germain. Taarifa za kuongezwa mkataba Rakitic zilithibitishwa katika tovuti ya Barcelona huku mkataba wake ukiwa umewekwa kitenzi cha euro milioni 125 kwa klabu itakayomuhitaji kabla ya mkatab wake kumalizika. Rakitic ameshinda mataji nane toka ajiunge na Barcelona akitokea Sevilla mwaka 2014.