Tuesday, April 24, 2012

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

WATANZANIA KUCHEZESHA AFRIKA KUSINI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limewateua waamuzi wane wa Tanzania kuchezesha mechi ya marudiano ya 16 bora ya Kombe la Shirikisho kati ya Black Leopards ya Afrika Kusini na Warri Wolves ya Nigeria itakayochezwa nchini Afrika Kusini kati ya Mei 4, 5 na 6 mwaka huu. Waamuzi hao ni Waziri Sheha atakayepuliza filimbi wakati wasaidizi wake watakuwa John Kanyenye na Erasmo Jesse. Mwamuzi wa akiba (fourth official) atakuwa Israel Mujuni. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Aurelio Mathias wa Msumbiji. Mechi ya kwanza kati ya timu hizo itachezwa Jumapili (Aprili 29 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Warri City ulioko Jimbo la Delta nchini Nigeria na itachezeshwa na waamuzi kutoka Senegal wakati Kamishna atakuwa Inyangi Bokinda wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

1,635 WASHUHUDIA MECHI YA YANGA, POLISI DODOMA
Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Yanga na Polisi Dodoma iliyochezwa (Aprili 22 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ilishuhudiwa na watazamaji 1,635 na kuingiza sh. 5,666,000. Baada ya kuondoa gharama za awali za mchezo na asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ni sh. 864,305.08 kila klabu ilipata sh. 193,858.47, uwanja sh. 26,469.49. Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 26,469.49, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 108,687.80. Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 13,234.75, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) sh. 2,646.95 na asilimia 10 ya gharama za mechi ni sh. 26,469.49. Gharama za awali za mechi zilikuwa nauli ya ndani kwa waamuzi sh. 10,000, nauli ya ndani kwa kamishna wa mchezo sh. 10,000. Mwamuzi wa akiba sh. 30,000, posho ya kujikimu kwa kamishna na waamuzi sh. 160,000, gharama ya tiketi sh. 1,500,000, usafi na ulinzi kwa uwanja sh. 1,500,000 na Wachina (Beijing Construction) sh. 1,000,000. Kutokana na mechi hiyo kuingiza kiasi kidogo baadhi ya gharama zililipwa nusu au kutolipwa kabisa na kuacha madeni. Madeni hayo ni tiketi sh. 1,500,000, maandalizi ya uwanja (pitch marking) sh. 400,000, umeme sh. 300,000, usafi na ulinzi kwa uwanja sh. 850,000 na Wachina sh. 1,000,000.

POLISI MORO, MGAMBO, PRISONS ZAPANDA VPL
Fainali ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) iliyoshirikisha timu tisa imemalizika jana (Aprili 23 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro huku tatu zikifuzu kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu wa 2012/2013 utakaonza Agosti mwaka huu. Timu hizo ni Polisi Morogoro iliyofikisha pointi 20 ikifuatiwa na Mgambo Shooting ya Tanga (15) na Tanzania Prisons ya Mbeya iliyomaliza katika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 14. Nyingine zilizofuatia na pointi zao kwenye mabano ni Polisi Dar es Salaam (13), Mbeya City Council (11), Rhino Rangers ya Tabora (8), Mlale JKT ya Ruvuma (8), Polisi Tabora (6) na Transit Camp ya Dar es Salaam (2).

SIMBA, MORO UNITED ZAINGIZA MIL 28/-
Pambano la Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Moro United lililochezwa jana (Aprili 23 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeingiza sh. 28,688,000. Jumla ya watazamaji 7,945 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa viingilio vya sh. 3,000, sh. 5,000, sh. 10,000 na sh. 15,000. Watazamaji 6,946 kati ya hao walishuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 3,000. Baada ya kuondoa gharama za awali za mchezo na asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ni sh. 4,376,135.59 kila klabu ilipata sh. 4,919,009.32, uwanja sh. 1,454,286.44. Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 1,454,286.44, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,058,414.58, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 727,143.22, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) sh. 145,428.64 na asilimia 10 ya gharama za mechi ni sh. 1,454,286.44. Gharama za awali za mechi zilikuwa nauli ya ndani kwa waamuzi sh. 10,000, nauli ya ndani kwa kamishna wa mchezo sh. 10,000, mwamuzi wa akiba sh. 30,000, posho ya kujikimu kwa kamishna na waamuzi sh. 80,000, gharama ya tiketi sh. 3,000,000, maandalizi ya uwanja (pitch) sh. 400,000, umeme sh. 300,000, usafi na ulinzi kwa uwanja sh. 2,350,000 na Wachina (Beijing Construction) sh. 2,000,000. Nayo mechi kati ya Villa Squad na African Lyon iliyochezwa Aprili 22 mwaka huu kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam iliingiza sh. 496,000 ambapo kila klabu ilipata sh. 68,061.70 wakati watazamaji walioshuhudia mechi hiyo ni 469. Vilevile mechi kati ya Tanzania (Ngorongoro Heroes) na Sudan iliyochezwa Aprili 21 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam iliingiza sh. 9,717,000 kutokana na washabiki 2,562.

MECHI ZA LIGI KUU WIKIENDI HII
Ligi Kuu ya Vodacom imeingia raundi ya 25 ambapo kesho (Aprili 25 mwaka huu) Oljoro JKT itaikaribisha Yanga kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha wakati JKT Ruvu itakuwa mwenyeji wa Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Raundi hiyo itakamilika kwa mechi nne; Aprili 28 mwaka huu Coastal Union itakuwa mwenyeji wa Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga huku Mtibwa Sugar ikiwa mgeni wa African Lyon kwenye Uwanja wa Chamazi. Azam na Toto African zitacheza Chamazi, Aprili 30 mwaka huu wakati Mei 1 mwaka huu Villa Squad itaumana na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Chamazi. Ligi hiyo itafunga msimu wa 2011/2012, Mei 5 mwaka huu ambapo timu zote 14 zitakuwa uwanjani. Simba vs Yanga (Uwanja wa Taifa), Oljoro JKT vs Polisi Dodoma (Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha) na Ruvu Shooting vs Villa Squad (Mabatini, Mlandizi). Mechi nyingine zitakuwa kati ya Coastal Union vs Toto African (Mkwakwani, Tanga), African Lyon vs JKT Ruvu (Manungu, Morogoro), Azam vs Kagera Sugar (Chamazi, Dar es Salaam) na Moro United vs Mtibwa Sugar (Jamhuri, Morogoro).

No comments:

Post a Comment