Tuesday, December 29, 2015

UNITED YATENGA PAUNDI MILIONI 33 KWA KIUNGO WA LAZIO.

KLABU ya Manchester United imedaiwa kujipanga kutoa ofa ya paundi milioni 33 kwa ajili ya kiungo wa kushambulia wa Lazio, Felipe Anderson. Kwa mujibu wa taarifa zilizozagaa United walikuwa wamemuweka kiungo wa Real Madrid James Rodriguez katika rada zao lakini baada ya kuona uwezekano huo utakuwa mgumu kumsajili katikati ya msimu wameamua kugeuzia nguvu zao kwa Anderson. United wamejipanga kuongeza nguvu katika kikosi chao pindi dirisha dogo la usajili litakapofunguliwa mwishoni mwa wiki hii. Meneja wa United Louis van Gaal ambaye yuko katika shinikizo anataka kufanya mabadiliko ya haraka ili kikosi hicho kirejee katika hali ya ushindani kama walivyoanza msimu.

IBE AIPA LIVERPOOL AHUENI.

MENEJA wa Liverpool, Jurgen Klopp amesema kiungo Jordon Ibe anaweza kurejea tena baada ya kupona katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Sunderland kesho. Hata hivyo, Klopp aliendelea kudai kudai kuwa pamoja na ahueni hiyo ya kurejea kwa Ibe lakini itabidi wasubiri wiki moja zaidi ili James Milner naye aweze kupona tayari kwa kurejea uwanjani. Ibe amekuwa benchi katika mechi mbili za ligi zilizopita za Liverpool akiokosa pia mchezo dhidi ya vinara Leicester City ambao walishinda kwa bao 1-0 Jumamosi iliyopita. Milner naye ameendelea kukaa nje kufuatia kupata majeruhi ya nyonga mapema mwezi huu. Akihojiwa Klopp amesema Ibe tayari ameshaanza mazoezi toka jana baada ya kuumwa kwa karibu wiki nzima, hivyo kuna uwezekano akawepo katika mchezo wa kesho.

SARE YAMRIDHISHA HIDDINK.

MENEJA wa muda wa Chelsea, Guus Hiddink ameridhishwa na sare ya bila kufungana waliyopata dhidi ya Manchester United jana, haswa kutokana na mabingwa hao wa Ligi Kuu kucheza bila mshambuliaji wa kueleweka. Diego Costa anatumikia adhabu baada ya kulimwa kadi Jumamosi iliyopita wakati walipotoa sare ya mabao 2-2 dhidi ya Watford wakati Loic Remy na Radamel falcao wakiwa nje kutokana na majeruhi na kumlazimisha winga Eden Hazard kucheza katika nafasi asiyoizoea. Akihojiwa Hiddink amesema kiufundi walikuwa sawa na hata safu yao ya ulinzi ilikuwa imejipanga vyema. Hiddink aliendelea kudai kuwa hawakuwa na nguvu za kutosha kuiumiza United kwakuwa walikuwa na matatiz kidogo katika safu ya ushambuliaji kutokana na adhabu na majeruhi ya nyota wao.

RUFANI YA MADRID YATUPILIWA MBALI.

KLABU ya Real Madrid, imeshindwa rufani yake ya kupinga kuenguliwa katika michuano ya Kombe la Mfalme kwa kuchezesha mchezaji asiyeruhusiwa. Mabingwa hao mara 19 wa michuano hiyo walienguliwa kwa kumchezesha winga Denis Cheryshev katika mchezo dhidi ya Cadiz uliochezwa Desemba 2 mwaka huu. Cheryshev alipaswa kutumikia adhabu yake kutocheza mechi moja ambayo aliipata wakati akicheza kwa mkopo Villarreal msimu uliopita. Mahakama ya Michezo ya Hispania ilitupilia rufani ya Madrid baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote kuhusiana na sakata hilo. Madrid kwasasa wanashikilia nafasi ya tatu katika msimamo wa La Liga nyuma ya mahasimu wao Barcelona na Atletico Madrid.

OZIL NDIO MCHEZAJI BORA LIGI KUU - WENGER.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amemsifia Mesut Ozil kama mchezaji bora wa Ligi Kuu na kumfananisha na nguli wa klabu hiyo Dennis Bergkamp kufuatia kiwango kikubwa alichoonyesha katika ushindi wa mabao 2-0 waliopata dhidi ya Bournemouth jana. Kiungo huyo wa kimataifa wa Ujerumani, alitengeza bao moja na kufunga lingine katika mchezo huo uliofanyika katika Uwanja wa Emirates na kufanya timu hiyo kukwea kileleni mwa msimamo wa ligi. Mpaka sasa Ozil ameshatoa pasi za mwisho 16 na kufunga mabao matano katika ligi na kumfanya kukaribia rekodi ya pasi za mwisho 20 ambayo iliwekwa na nguli mwingine wa Arsenal Thierry Henry. Akihojiwa Wenger amesema ukitizama kiwango na idadi ya pasi za mwisho alizotoa msimu huu hakuna shaka kuwa ndio mchezaji bora kwasasa nchini Uingereza. Meneja huyo aliendelea kudai kuwa kiungo huyo kwasasa anakaribia kufanana na Bergkamp kwani pamoja na kutoa pasi lakini pia amekuwa akifunga mabao muhimu.

RONALDO AMPIGIA CHAPUO MESSI KUTWAA BALLON D'OR.

NGULI wa soka wa Brazil, Ronaldo amesema nyota wa Barcelona, Lionel Messi ni mchezaji aliyekamilika zaidi ya mshambuliaji wa Real Madrid Cristiano Ronaldo. Wawili wapo katika orodha ya mwisho ya tuzo za Ballon d’Or sambamba na Neymar zawadi ambayo wamekuwa wakipokezana kwa miaka saba iliyopita huku Messi akishinda mara nne na Ronaldo mara tatu. Mjadala wa mchezaji gani ana kipaji zaidi ya mwenzake umekuwa ukitawala kwa kipindi kirefu, lakini Ronaldo ambaye naye ameshawahi kunyakuwa tuzo hiyo mara tatu amesema Messi ndio chaguo lake kati ya wawili hao. Ronaldo amesema amemchagua Messi kwasababu anamuona ni mchezaji aliyekamilika zaidi kuliko Ronaldo kwani anafanya vitu vyake kwa upekee.

GUARDIOLA AKANUSHA KUTUMA UJUMBE WA CHUKI.

MSHAMBULIAJI aliyetimuliwa mara baada ya kusajiliwa na Barcelona, Sergi Guardiola amekanusha kutuma ujumbe katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa twitter uliopelekea mkataba wake kusitishwa. Guardiola mwenye umri wa miaka 24 ni mmoja kati ya wachezaji watatu waliosajiliwa katika kikosi B cha Barcelona lakini ndoto zake za kuwachezea mabingwa hao wa Ulaya haraka zilizimika wakati ujumbe wa kuiponda klabu na kuhusu Catalonia ulipoonekana katika twitter yake. Katika taarifa rasmi, masaa machache baada ya kutangaza ujio wake, Barcelona walithibitisha kuwa wamebadili mawazo na kusitisha mkataba wake. Akihojiwa Guardiola amesema ameuelewa uamuzi wa klabu hiyo lakini amedai kuwa sio yeye aliyetuma ujumbe huo. Guardiola alianza kwa kuwaomba radhi Barcelona na Catalonia na kuendelea kudai kuwa ujumbe huo hakutumwa naye kwani kipindi cha mwaka 2013 ambacho ndio ujumbe unadaiwa kutumwa alikuwa hajui hata masuala hayo ya mitandao.

VAN GAAL ADAI HANA SABABU YA KUJIUZULU.

MENEJA wa Manchester United, Louis van Gaal amesema haoni sababu ya kujiuzulu baada ya kikosi chake kutoka sare ya bila kufungana na Chelsea jana. United sasa wameshindwa kupata ushindi katika mechi nane za mashindano yote walizocheza ikiwa ni mara ya kwanza kutokea hivyo toka mwaka 1990 na wako nyuma kwa alama tano kufikia nafasi ya nne. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo Van Gaal amesema kama wachezaji wanaweza kucheza kwa kiwango kile wakiwa katika shinikizo hakuna sababu ya yeye kujiuzulu. Sare hiyo imeifanya United kuendelea kubaki katika nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu ambayo inaendelea baadae leo kwa kuzikutanisha timu za Leicester City na Manchester City.

Monday, December 28, 2015

MAN CITY YATAKA KUFANYA KUFURU KWA MESSI.

KLABU ya Manchester City inadaiwa kutenga kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kumng’oa Lionel Messi kutoka Barcelona. Taarifa za gazeti la Sport zimedai wawakilishi wa Messi wamemuahidi kuwa atavuna kiasi cha paundi milioni 20 kwa msimu kama akitua City kiasi ambacho kinazidi kile anachopewa na mabingwa hao wa Hispania. Wakati Barcelona wakiwa hawana mpango wa kufanya mazungumzo ya mkataba mpya mpaka msimu ujao, klabu hiyo ina uhakika Messi ataikacha ofa hiyo kama alivyofanya wakati alipofuatwa na Paris Saint-Germain na Chelsea huko nyuma. Kwasasa City hawataweza rasmi ofa yao kwa Barcelona mpaka watakapoona dalili kwa Messi kuwa yuko tayari kukubali ofa yao.

MESSI AENDELEA KUZOA TUZO.

KLABU ya Barcelona na nyota wa Lionel Messi wameibuka washindi tena katika tuzo za Globe Soccer zilizofanyika huko Dubai jana, kwa kuondoka na zawadi ya timu na mchezaji bora. Messi alisafiri kutoka Argentina kwenda kuhudhuria sherehe hizo. Akihojiwa Messi amesema ni jambo zuri kupokea tuzo hiyo lakini kama asemavyo siku zote timu nzima ndio inafanya hilo kuwezekana. 
Barcelona imefanikiwa kushinda mataji matano mwaka 2015 ambayo ni La Liga, Kombe la Mfalme, Ligi ya Mabingwa Ulaya, Super Cup ya Ulaya na Klabu Bingwa ya Dunia. Taji pekee ambalo wamelikosa kwa mwaka huu ni Super Cup ya Hispania ambalo lilikwenda kwa Athletic Bilbao. 
Kocha wa timu ya taifa ya Ubelgiji Marc Wilmots ametajwa kama kocha bora wa mwaka huku Benfica ya Ureno wao wakichukua tuzo ya kuwa na shule bora ya soka. Viungo Andres Pirlo wa Italia na Frank Lampard wa Uingereza wao wamepewa tuzo kutokana na kucheza soka kwa kipindi kirefu zaidi.

RONALDO ATASTAAFU AKIWA NA UMRI WA MIAKA 40 - MENDES.

WAKALA wa mshambuliaji wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo amedai kuwa nyota huyo bado ataendelea kuitumikia timu hiyo mpaka atakapofikisha miaka 40. Ronaldo mwenye umri wa miaka 30 na mshindi wa tuzo tatu za Ballon d’Or amekuwa akihusishwa na tetesi za kwenda Paris Saint-Germain au klabu yake ya zamani ya Manchester United kabla hajatundika daruga zake. Nyota huyo wa kimataifa wa Ureno ana mkataba na Madrid unaomalizika Juni mwaka 2018, lakini Mendes amesisitiza mteja wake bado anaweza kuendelea kubakia Santiago Bernabeu kwa muongo mwingine mmoja. 
Jorge Mendes akipokea tuzo ya wakala bora wa mwaka katika sherehe za Globe Soccer zilizofanyika huko Dubai jana.
Mendes amesema Ronaldo ndio mchezaji bora wa wakati wote na ana uhakika kuwa anaweza kucheza kwa miaka mingine zaidi ya saba akiwa Madrid. Wakala huyo aliendelea kudai kuwa ana furaha kuitumikia klabu hiyo na atastaafu akiwa na umri wa miaka 40.

POCHETTINO AWAZODOA WANAOMUWINDA KANE.

MENEJA wa Tottenham Hotspurs, Mauricio Pochettino amesisitiza Harry Kane hatauzwa kwa bei yeyote ile. Kane alifunga bao lake la 10 na 11 msimu huu katika ushindi wa mabao 3-0 waliopata dhidi ya Norwich City Jumamosi iliyopita na kuwa mchezaji wa kwanza wa Spurs kufunga mabao 27 au zaidi kwa mwaka. Kiwango cha Kane katika kipindi cha miezi 12 iliyopita pia kimemfanya kuitwa katika kikosi cha timu ya taifa ya Uingereza, huku vilabu kadhaa vikubwa vikimmezea mate zikiwemo Manchester United na Chelsea. Hata hivyo, Pochettino amesisitiza kuwa hakuna klabu itakayoweza kumnunua nyota huyo kwasasa kwani ni muhimu katika kikosi chao. Meneja huyo amesema hakuna kiwango cha bei alichowekewa hivyo haitawezekana kununuliwa kwasasa.

TUNACHEZA KWA AJILI YA VAN GAAL - CARRICK.

KIUNGO wa manchester United, Michael Carrick amesema madai ya kuwa wachezaji wa timu hiyo hawajitumi ili kulinda kibarua cha meneja wao Louis van Gaal, ni kuwakosea heshima. Kipigo walichopata United Jumamosi iliyopita kinakuwa cha nne mfululizo na kuendelea rekodi yao kutoshinda katika mechi saba. Van Gaal ambaye amesema anaweza kujiuzulu alikuwa katika uwanja wa mazoezi wa United jana. Carrick amesema ni suala la ukosefu wa heshima watu kudai kuwa hawajitumi kwa ajili ya meneja wao ni jambo linalowaumiza kwani wao sio watu wa aina hiyo. Nyota huyo aliendelea kudai kuwa anafahamu kama ilivyo kwao matokeo yanawaumiza lakini sio kweli kuwa hawajitumi kwani wanafanya kila wawezali wakishirikiana vyema na meneja kubadili hali ilivyo.

ARSENAL YAMUWANI ELNENY WA FC BASEL.

KLABU ya Arsenal imeanza mazungumzo na FC Basel ya Uswisi kwa ajili ya kutaka kumsajili kiungo wao Mohamed Elneny. Nyota huyo wa kimataifa wa Misri mwenye umri wa miaka 23 alijiunga na klabu hiyo mwaka 2013 na kufanikiwa kushinda mataji ya Ligi Kuu ya nchi hiyo kwa misimu mitatu. Elneny anakadiriwa kuwa na thamani ya paundi milioni tano, ingawa atahitaji kibali cha kufanyia kazi nchini Uingereza. Kama Arsenal wakifanikiwa kumsajili wanaweza kumtumia katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kwani Basel hawakufanikiwa kufuzu hatua ya makundi msimu huu. Meneja wa Arsenal Arsene Wenger anajaribu kuongeza nguvu safu yake ya kiungo baada ya Francis Coquelin na Santi Cazorla kupata majeruhi ya muda mrefu huku Aaron Ramsey na Mikel Arteta nao wakikosa michezo kadhaa kutokana na majeruhi.

MCHEZAJI WA EL SALVADO AUAWA KWA KUPIGWA RISASI.

MCHEZAJI wa zamani wa kimataifa wa El Salvador, Alfredo Pacheco ameuawa kwa kupigwa risasi. Mtu mwenye silaha anadaiwa kumfuata Pacheco mwenye umri wa miaka 33 na kumfyatulia risasi kadhaa katika kituo cha mafuta kilichopo mji wa Santa Ana kilometa 76 kutoka magharibi mwa mji mkuu wa San Salvador. Maofisa wa polisi wamesema watu wengine wawili walijeruhiwa katika tukio hilo ambalo bado wanafanya uchunguzi wa chanzo chake. Beki huyo ambaye ndio mchezaji wa aliyeichezea mechi nyingi zaidi nchi yake, alifungiwa maisha kujishughulisha na masuala ya soka mwaka 2013 baada ya kukutwa na hatia ya kupanga matokeo. Pacheco na wachezaji wengine 13 wa timu ya taifa walikutwa na hatia ya kupkea rushwa na kupanga matokeo katika mechi kadhaa kati ya mwaka 2010 hadi 2013.

Sunday, December 27, 2015

WENGER AMUWEKA CHICHARITO KATIKA RADA ZAKE.


KLABU ya Arsenal inaripotiwa kuwa inapanga kufanya usajili wa kushtusha wa Javier Hernandez ambaye amekuwa katika kiwango bora toka aondoke Manchester United na kutua Bayer Leverkusen ya Ujerumani. Nyota huyo wa kimataifa wa Mexico aliondoka Old Trafford kwa kitita cha paundi milioni saba baada ya kuambiwa na meneja Louis van Gaal kuwa hayuko katika mipango yake msimu huu. Toka atue Bayer, Chicharito ameshafunga mabao 19 katika mechi 21 hivyo kumshawishi Wenger kumuwania ili aweze kusaidiana na Olivier Giroud. Inaaminika kuwa nyota huyo anapenda kurejea Ligi Kuu na kama uhamisho ukifanikiwa ataungana na Danny Welbeck ambaye walikuwa wote United.

ROBINHO ATAMANI KUREJEA BRAZIL.

MSHAMBULIAJI mkongwe wa kimataifa wa Brazil, Robinho amesema anaweza kurejea kucheza soka nchini kwao pindi mkataba wake na mabingwa wa soka wa Asia Guangzhou Evergrande utakapomalizika. Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 31 amefunga mabao matatu katika mechi tisa za ligi alizoichezea Guangzhou toka aliposaini mkataba wa miaka miezi sita na timu hiyo inayonolewa na Luis Felipe Scolari. Hata hivyo, Robinho amesema anataka kurejea Brazil ambako alicheza katika timu ya Santos katika msimu wa 2014-2015 kwa mkopo akitoke AC Milan ya Italia. Mkongwe huyo aliendelea kudai kuwa hilo ni jambo analofikiria lakini bado hajaamua chochote mpaka sasa kwani anafurahia mapumziko yake ya sikukuu.

KLOPP AKIRI HAIKUWA KAZI RAHISI KUIFUNGA LEICESTER CITY.

MENEJA wa Liverpool, Jurgen Klopp amekipongeza kikosi chake kwa kushinda mchezo wao dhidi ya vinara wa Ligi Kuu Leicester City jana katika Uwanja wa Anfield. Kabla ya mchezo huo wa jana ambao walishinda bao 1-0, Liverpool walikuwa wameambulia alama moja katika mechi tatu zilizopita za ligi. Lakini Liverpool walionekana kubalika kabisa katika mchezo huo wa jana ambao bao pekee liliwekwa kimiani na Christian Benteke aliyeingia akitokea benchi katika kipindi cha pili. Akihojiwa Klopp amesema kuwafunga vinara wa ligi ni kazi ngumu kwani timu nyingi ziejaribu lakini zimeshindwa ndio maana anafurahia ushindi kwakuwa walistahili. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa walikuwa na subira jambo ambalo limewasaidia kwa kiasi kikubwa katika mchezo huo.

COSTA AMTIA KIWEWE HIDDINK.

MENEJA wa Chelsea, Guus Hiddink amekiri kukosekana kwa Diaego Costa ni pigo kubwa kwa kikosi chao wakati watakapopambana na Manchester United katika Uwanja wa Old Trafford kesho. Hiddink alichukua mikoba ya kuinoa timu hiyo kwa mara ya kwanza toka alipoteuliwa meneja wa muda, akianza sare ya mabao 2-2 waliyopata dhidi ya Watford jana. Matokeo hayo yameifanya Chelsea kuendelea kubaki katika nafasi ya 15 katika msimamo wa ligi na Costa amepata kadi za njano tano kwa msimu huu hivyo atakosa mechi moja mabayo ni dhidi ya United. Akihojiwa Hiddink amesema kumkosa Costa ni pigo kwani amekuwa akiimarika na mchezo wao unaofuata ni muhimu sana kama angekuwepo. Hiddink aliendelea kudai kuwa pamoja na United kusuasua lakini sio timu ya kubeza kwani watakuwa wakicheza kwao.

RAIS WA ATLETICO AMFUNGULIA COSTA MILANGO YA KURUDI.

RAIS wa Atletico Madrid, Enrique Cerezo amedai mshambuliaji wa Chelsea anaweza kurejea katika klabu hiyo siku zijazo. Nyota huyo wa kimataifa wa Hispania ameanza kurejea katika makali yake kufuatia kufunga mabao mawili katika sare ya mabao 2-2 waliyopata dhidi ya Watford katika mchezo wa Ligi Kuu. Costa mwenye umri wa miaka 27 amekuwa akihusishwa na tetesi za kurejea Atletico ambako ndio alikoanzia kabla ya kuhamia Uingereza Julai mwaka jana. Akiulizwa kuhusiana na suala hilo Cerezo hakuonyesha kukubali wa kukanusha kuwa nyota huyo anaweza kurejea Hispania. Cerezo amesema kwasasa Costa ni mchezaji wa Chelsea lakini huwezi kujua kinachoweza kutokea mbele katika soka.

MAJERUHI YAMNYIMA RAHA KOMPANY.

NAHODHA wa Manchester City, Vincent Kompany amejipambanua kama mtu asiyeonekana katika mchezo wa jana pamoja na kupata majeruhi dakika nane toka aingie. Beki huyo wa kimataifa wa Ubelgiji mwenye umri wa miaka 29 aliingia katika kipindi cha pili akitokea benchi katika ushindi wa mabao 4-1 waliopata City lakini alisalia uwanjani kwa dakika nane kabla ya kutolewa tena kutokana na majeruhi. Akihojiwa Kompany amesema jana ilikuwa siku mbaya kwake kwani alikuwa akijisikia fiti lakini anapata changamoto ya majeruhi madogo madogo. Beki huyo aliendelea kudai kuwa jambo hilo linamkera sana lakini atajitahidi kupambana ili aweze kurejea akiwa fiti zaidi.

WENGER AAPA KULIPA KISASI.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema anaamini kikosi chake kitarudi vyema pamoja na kipigo kizito walichopata kutoka kwa Southampton jana wakati watakapoivaa Bournemouth kesho. Arsenal walibugizwa mabao 4-0 na Southampton katika Uwanja wa St Mary, na kushindwa kukaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu. Pamoja na kipigo hicho Wenger anawaunga mkono wa wachezaji wake kuonyesha ukomavu katika mchezo wao unaofuata ili waweze kupata matokeo mazuri. Akihojiwa Wenger amesema wachezaji wake wana ari ya kipekee na watalionyesha katika mchezo wao ujao. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa wanataka kuondoka katika hali ya huzuni na anawaamini wachezaji wake wanaweza kufanya vyema kesho.

Friday, December 25, 2015

HABARI PICHA: WACHEZAJI MBALIMBALI ULAYA WAKIONYESHA JINSI MAPUMZIKO YAO YA SIKUKUU YANAVYOKWENDA.










MECHI ZA LIGI KUU UINGEREZA ZITAKZOCHEZWA BOXING DAY.

15:45 STOKE CITY ? - ? MANCHESTER UNITED

18:00 AFC BOURNEMOUTH ? - ? CRYSTAL PALACE

18:00 ASTON VILLA ? - ? WEST HAM UNITED

18:00 CHELSEA ? - ? WATFORD

18:00 LIVERPOOL ? - ? LEICESTER CITY

18:00 MANCHESTER CITY ? - ? SUNDERLAND

18:00 SWANSEA CITY ? - ? WEST BROMWICH ALBION

18:00 TOTTENHAM HOTSPUR ? - ? NORWICH CITY

20:30 NEWCASTLE UNITED ? - ? EVERTON

22:45 SOUTHAMPTON ? - ? ARSENAL

UONGOZI WA BEKI3 UNAWATAKIWA WASOMAJI WAKE WOTE HERI YA MAPUMZIKO YA SIKUKUU.


Wednesday, December 23, 2015

MENDES AKANUSHA TETESI ZA MOURINHO KWENDA MAN UNITED.

WAKALA wa Jose Mourinho, Jorge Mendes amedai hakuna ofa yeyote rasmi iliyotolewa na Manchester United kwa ajili ya kumchukua kocha huyo. Mendez amesema hajui litakalotokea siku zijazo lakini kwasasa hakuna makubaliano yeyote wala ofa yeyote rasmi iliyokuja. Mourinho alitimuliwa na Chelsea wiki iliyopita, miezi saba baada ya kuingoza timu hiyo kunyakuwa taji la Ligi Kuu. Kocha huyo Mreno ambaye amewahi kunyakuwa matatu ya Ligi Kuu akiwa na Chelsea alishatoa taarifa akisisitiza kuwa hana mpango wa kupumzika.

SKRTEL NJE WIKI SITA.

BEKI wa Liverpool, Martin Skrtel amethibitisha kuwa anatarajia kukaa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki sita kutokana na mejeruhi. Nyota huyo wa kimataifa wa Slovakia mwenye umri wa miaka 31, alitolewa akiwa anachechemea katika dakika ya 44 ya mchezo wa Ligi Kuu ambao walitandikwa mabao 3-0 na Watford Jumapili iliyopita. Skrtel aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram kuwa alichanika msuli wa nyuma ya paja katika mchezo huo. Beki huyo aliendelea kudai kuwa anafahamu itakuwa ni safari ndefu kuelekea kupona lakini atafanya kila awezalo kuhakikisha anarejea haraka iwezekanavyo. Skrtel amekuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha Liverpool msimu huu akiwa amecheza mechi 26 za mashindano yote.

WENGER AMKINGIA KIFUA VAN GAAL.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger ameelezea tetesi zinazoendelea zikimhusisha Jose Mourinho kuchukua nafasi ya Louis van Gaal Manchester United, kuwa ni ukosefu wa heshima. Mourinho alitimuliwa Chelsea Alhamisi iliyopita baada ya mabingwa hao kushindwa kufanya vyema toka kuanza kwa msimu. Hata hivyo, kocha huyo Mreno toka wakati huo amekuwa akihusishwa na tetesi za kuhamia Old Trafford kufuatia shinikizo kubwa alilonalo Van Gaal ambaye ameshindwa kupata ushindi katika mechi zake sita zilizopita za mashindano yote. Akiulizwa kuhusu kuondoka kwa Mourinho, Wenger amesema anadhani vingi vimezungumzwa lakini ukweli ni kwamba huwa hapendi mtu apoteze kibarua chake. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa ana heshima kubwa kwa Van Gaal na kinachoendelea dhidi yake kwasasa sio heshima.

GUARDIOLA ANA UWEZO WA KUFUNDISHA POPOTE DUNIANI - RONALDINHO.

NYOTA wa zamani wa Barcelona, Ronaldinho amedai kuwa Pep Guardiola ana uwezo wa kufundisha soka popote duniani. Klabu ya Bayern Munich ilitangaza mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa Guardiola hataongeza mkataba wake na mabingwa hao wa Bundesliga huku Manchester City, Manchester United na Chelsea zikitajwa kuwania saini yake msimu ujao. Baada ya kunyakuwa mataji matatu ya La Liga, mawili ya Kombe la Mfalme na mawili ya Ligi ya mabingwa Ulaya akiwa na Barcelona, Guardiola amekuwa akibeba taji la Bundesliga toka atue Bayern ingawa bao hajapata taji la Ulaya akiwa Ujerumani. Popote atakapokwenda, Ronaldinho ambaye aliondoka Barcelona muda mfupi baada ya Guardiola kuteuliwa mwaka 2008, anategemea kocha huyo kuendelea kupata mafanikio. Ronaldinho amesema Guardiola ni kocha mkubwa ambaye ana uweze wa kufundisha timu yeyote duniani.

KOMPANY KUREJEA BOXING DAY.

MENEJA wa Manchester City Manuel Pellegrini amesema nahodha wake Vincent Kompany anaweza kurejea uwanjani katika mchezo dhidi ya Sunderland utakaofanyika Boxing Day. Kompany amekosa mechi tano za Ligi Kuu za City kutokana na majeruhi ya nyonga ambapo timu hiyo ilipoteza michezo mitatu kati ya hiyo na kushinda miwili na kuwafanya kuwa nyuma ya vinara Leicester City kwa alama sita. City imeshapoteza mechi tano jumla msimu huu lakini hawajafungwa wakati Kompany akiwa uwanjani. Pellegrini ana matumaini beki huyo wa kimataifa wa Ubelgiji mwenye umri wa miaka 29 atarejea katika kikosi cha kwanza katika mchezo huo wa Ligi Kuu. Kocha huyo amesema Kompany amekuwa akifanya mazoezi na kikosi cha kwanza kwa siku mbili zilizopita hivyo ana matumaini Jumamosi hii anaweza kuwa fiti kwa kucheza.

BRADLEY MCHEZAJI BORA WA MWAKA MAREKANI.

NAHODHA wa timu ya taifa ya Marekani, Michael Bradley ametajwa kuwa mwanasoka wa mwaka wa nchi hiyo jana. Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 28 ameshinda tuzo hiyo kwa mara ya kwanza katika maisha yake ya soka, kufuatia mafanikio ambayo amepata katika klabu yake na mechi za kimataifa. Akiwa nahodha wa Toronto FC amefainikiwa kuisaidia klabu hiyo kucheza hatua ya mtoano ya Ligi Kuu ya Marekani-MLS kwa mara ya kwanza katika historia yao. Mkongwe huyo ambaye amecheza katika fainali mbili za Kombe la Dunia alitimiza mechi yake ya 100 akiwa na kikosi cha Marekani na kuwa mchezaji wanne mdogo kufikia hatua hiyo.

VERON ADAI MESSI ANAPENDA KUCHEZA INTER.

MCHEZAJI wa zamani wa kimataifa wa Argentina, Juan Sebastian Veron amesema Lionel Messi alishawahi kumdokeza kuwa anataka kuichezea Inter Milan. Nyota huyo wa Barcelona maisha yake yote ya soka amekuwa akiitumikia klabu hiyo lakini amekuwa akihusishwa na tetesi za kuwindwa na vilabu kadhaa katika miaka ya karibuni. Na Veron ambaye amewahi kucheza katika klabu za Sampdoria, Parma, Lazio na Inter katika kipindi chake cha miaka 20 aliyocheza soka, amesema Messi alishawahi kumwambia kuhusu nia yake ya kwenda kucheza Inter. Veron aliendelea kudai kuwa ni miaka mingi imepita lakini kuna wakati nyota huyo alishawahi kumuambia angependa kucheza Inter.

CECH ATAMBA ARSENAL KUNYAKUWA LIGI KUU.

KIPA wa Arsenal, Petr Cech amedai kikosi chao kina uwezo wa kunyakuwa la Ligi Kuu msimu huu. Arsenal kwasasa wako katika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi wakiwa alama mbili nyuma ya vinara Leicester City na wamepoteza mechi moja kati ya 11 walizocheza. Cech mwenye umri wa miaka 33, amesema wana kikosi imara na pindi wote watakaporejea, meneja wao Arsene Wenger anaweza kumtumia mchezaji yeyote anavyotaka. Kipa huyo huyo aliendelea kudai kuwa hiyo itakuwa faida kubwa kwao na kuwafanya kuendelea kucheza katika kiwango cha juu. Arsenal ambao ni mabingwa watetezi wa Kombe la FA walimaliza katika nafasi ya tatu msimu uliopita, alama 12 nyuma ya mabingwa Chelsea na hawajashinda taji hilo toka msimu 2003-2004.

BLATTER KUTUPIWA VIRAGO VYAKE NA FIFA.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA linadaiwa kumpa taarifa rais wake aliyefungia Sepp Blatter kuwa anatakiwa kuondoka katika makazi ya rais ifikapo Februari 26 wakati mbadala wake atakapokuwa amechaguliwa. Makazi hayo ya zamani yaliyopo jijini Zurich ni moja ya vitu ambavyo Blatter mwenye umri wa miaka 79 atavipoteza baada ya kufungiwa miaka nane kujishughulisha na masuala ya soka na kamati ya maadili ya shirikisho hilo Jumatatu. Mbali na makazi hayo, Blatter pia atanyang’anywa simu ya mkononi, gari pamoja na email za kiofisi ambazo zote ni mali ya FIFA. Kwasasa Blatter ataruhusiwa kutumia vitu hivyo pamoja na kuendelea kupata mshahara wake mpaka pale mkataba wake utakapomalizika Februari 26.

Monday, December 21, 2015

MESSI ALIVYOTAKA KUMUANZISHIA SHABIKI WA RIVER PLATE ALIYEMTEMEA MATE.

KAMA ULIMISS BARCELONA ILIVYOWAADHIBU NDUGU ZAKE MESSI.

BLATTER, PLATINI WAFUNGIWA MIAKA NANE.

RAIS wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA Sepp Blatter na rais wa Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA Michel Platini kwa pamoja wamefungiwa miaka nane kujishughulisha na masuala yeyote yahusuyo soka kufuatia uchunguzi wa kimaadili. Wawili hao wamekutwa na hatia kufuatia malipo yasiyo ya uaminifu ya paundi milioni 1.3 ambayo Blatter alimlipa Platini mwaka 2011. Wote wawili walikanusha kufanya jambo lolote baya na adhabu hiyo itaanza kufanya kazi mara moja.m Blatter mwenye umri wa miaka 79 amekuwa rais wa FIFA toka mwaka 1998 na tayari alishatangaza kujiuzulu mara baada ya uchaguzi utakaofanyika Februari mwakani. Platini mwenye umri wa miaka 60 alikuwa akitajwa kama kiongozi wa baadaye na alikuwa na matumaini ya kuchukua nafasi ya Blatter. Mbali na dhabu hiyo Blatter pia amelimwa faini ya paundi 33,000 huku Platini yeye akilimwa faini ya paundi 54,000.

REAL MADRID WALIVYOIDHALILISHA RAYO VALLECANO.

Sunday, December 20, 2015

BARCELONA YAICHAPA RIVER PLATE NA KUNYAKUWA KOMBE LA KLABU YA DUNIA.

KLABU ya Barcelona imeshinda taji lake la tano kwa mwaka huu baada ya kunyakuwa Kombe la Klabu Bingwa ya Dunia kwa mara ya tatu kufuatia ushindi mnono waliopata dhidi ya River Plate katika mchezo wa fainali. Katika mchezo huo uliofanyika jijini Yokohama mapema leo, River Plate ya Argentina ilionekana kushindwa kabisa kuendana na kasi ya washambuliaji watatu wa Barcelona Lionel Messi, Luis Suarez na Neymar na kujikuta wakichapwa mabao 3-0. Messi alifunga bao la kuongoza katika mchezo huo baada ya kurejea tena kufuatia kusumbuliwa matatizo ya figo ambayo yalimfanya kuukosa mchezo wa nusu fainali. Mabao mengine ya Barcelona yalifungwa na Suarez ambaye amemaliza mashindano hayo akiwa na mabao matano baada ya kufunga hat-trick katika ushindi wa mabao 3-0 waliopata katika mchezo wa nusu fainali dhidi ya Guangzhou Evergrande ya China.

ANCELOTTI ASHUKURU KUPEWA NAFASI BAYERN.

MENEJA Carlo Ancelotti amejibu kufuatia kuthibitishwa meneja mpya ajaye wa Bayern Munich msimu ujao akieleza kuwa uteuzi huo ni heshima kubwa kwake. Bayern walithibitisha kuwa meneja Muitaliano ambaye amekuwa bila kibarua toka Mei mwaka huu alipotimuliwa na Real Madrid, atachukua nafasi ya Pep Guardiola anayeondoka mwishoni mwa msimu. Akihojiwa Ancelotti amesema ni heshima kubwa kwake kuwa sehemu ya klabu hiyo kubwa msimu ujao kwani wakati alipotambua kuwa wanamtaka alizuia kusikiliza ofa zingine zote. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa kwasasa anaitakia Bayern pamoja na rafiki yake Guardiola msimu mzuri.

ANCELOTTI KUCHUKUA NAFASI YA GUARDIOLA BAYERN.

MENEJA wa Bayern Munich, Pep Guardiola anatarajiwa kuondoka mwishoni mwa msimu huu na nafasi yake inatarajiwa kuchukuliwa na Carlo Ancelotti. Guardiola mwenye umri wa miaka 44, anahusishwa na tetesi za kwenda katika klabu Ligi Kuu zikiwemo Manchester City, Manchester United, Chelsea na Arsenal. Meneja huyo w zamani wa Barcelona ameshinda mataji mawili ya Bundesliga na moja la Kombe DFB toka ajiunge na Bayern kiangazi mwaka 2013. Ancelotti mwenye umri wa miaka 56, ambaye amekuwa mapumzikoni toka atimuliwe na Real Madrid Mei mwaka huu, amesaini mkataba wa miaka mitatu na Bayern. Mabingwa hao wa Ujerumani kwasasa wanaongoza Bundesliga kwa tofauti ya alama nane na wanatarajiwa kucheza Juventus ya Italia katika hatua ya timu 16 bora ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Ofisa mkuu wa bayern Karl-Heinz Rummenigge amemshukuru Guardiola kwa kila alichoipa klabu hiyo toka alipotua mwaka 2013 na ana matumaini kuwa atawaongezea mataji zaidi katika muda huu aliobakiza kabla hajaondoka.