Thursday, June 29, 2017

EVERTON YANASA BEKI WA BURNLEY.

KLABU ya Everton inakaribia kumsajili beki wa kimataifa wa Uingereza Michael Keane kutoka Burnley kwa kitita cha paundi milioni 25. Keane mwenye umri wa miaka 24 ameakuwa akiwindwa na meneja wa Everton Ronald Koeman na alishaweka wazi jinsi anavyomhusudu mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United msimu uliopita. Mazungumzo bado yanaendelea na Everton wana matumaini watakamilisha dili kabla wachezaji hawajarejea kwa ajili ya mazoezi ya maandalizi ya msimu mpya Jumatatu ijayo. United nao walikuwa wakitajwa kutaka kumsajili tena Keane baada ya kuuzwa Burnley kwa kitita cha paundi milioni mbili na meneja wa wakati huo Louis van Gaal.

DEFOE AREJEA TENA BOURNEMOUTH.

MSHAMBULIAJI wa Sunderland, Jermain Defoe amesajiliwa tena na klabu yake ya zamani ya Bournemouth akiwa mchezaji huru. Nyota huyo wa kimataifa wa Uingereza mwenye umri wa miaka 34, ambaye amesaini mkataba wa miaka mitatu amesema amefurahi kurejea tena katika Uwanja wa Vitality. Defoe alifunga mabao mabao 15 katika Ligi Kuu msimu uliopita aliendelea kudai ulikuwa uamuzi rahisi kujiunga na klabu kubwa yenye kocha bora. Defoe anakuwa mchezaji wa pili kusajiliwa na Bournemouth baada ya ujio wa kipa Asmir Begovic aliyetokea Chelsea. Bournemouth ilimaliza katika nafasi ya tisa katika msimamo katika msimu wao wa pili katika Ligi Kuu.

VIONGOZI WA TFF, SIMBA WAPANDISHWA KIZIMBANI.

RAIS wa Shirikisho la Soka nchini-TFF Jamal Malinzi na Katibu Mkuu Celestine Mwesigwa wamesomewa mashitaka 28 katika Mahakama ya Kisutu mapema leo. Viongozi hao walikamatwa mapema jana kwa mahojiano na TAKUKURU kabla ya kufikishwa mahakamani mapema leo. Malinzi na Mwesigwa wote wamerudishwa rumande mpaka Jumatatu ijayo ya Julai 03 ambapo dhamana yao ndio itajadiliwa kutokana na makosa yanayowakabili. Wakati huohuo, Rais wa klabu ya Simba Evans Aveva na Makamu wa Rais, Geofrey Nyange “Kaburu” nao wamerudishwa rumande mpaka Julai 13 baada ya kusomewa mashitaka matano ikiwemo utakatishaji fedha. Aveva na Kaburu nao waliitwa na TAKUKURU kwa mahojiano kama ilivyokuwa kwa Malinzi na Mwesigwa.

BAYERN WASHINDWA BEI YA SANCHEZ.

RAIS wa Bayern Munich, Uli Hoeness ameonyesha kuondoa uwezekano wa kumsajili nyota wa Arsenal Alexis Sanchez kwa kudai kuwa kikosi chao kinapaswa kujengwa na wachezaji vijana zaidi kuliko wale wazoefu. Mabingwa hao wa Bundesliga wamekuwa wakihusishwa kwa kiasi kikubwa na tetesi za kumuwania nyota huyo wa kimataifa wa Chile katika miezi ya karibuni, ingawa hivi sasa Manchester City ndio wanaoonekana kuwa kwenye nafasi nzuri zaidi ya kumsajili. Akizungumza na wanahabari kuhusiana na mipango ya Bayern, Hoeness amesema kikubwa wanachofanya ni kujenga kikosi chao kupitia wachezaji vijana. Hoeness aliongeza kuwa kamwe hawawezi kujenga kikosi bora cha baadae kwa kununua mchezaji mmoja mwenye umri wa miaka 29 au 30 kwa kiasi cha euro milioni 100, hizo sio sera zao.

RONALDO ATHIBITISHA KUPATA WATOTO WENGINE WAWILI.

MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo amethibitisha kuwa amekuwa baba tena wa watoto wawili wa kiume waliozaliwa wakati wa michuano ya Kombe la Shirikisho inayoendelea huko nchini Urusi. Ureno ilienguliwa katika michuano hiyo jana kwa changamoto ya mikwaju ya penati 3-0 na Chile kufuatia timu hizo kutoka sare ya bila kufungana katika muda wa kawaida na ule wa nyongeza. Ronaldo alionyesha kusikitishwa kwa kutolewa huko na kuthibitisha taarifa za kuzaliwa kwa watoto wake hao ambazo zinaweza kumfanya kukosa mchezo wa mtoano kutafuta mshindi wa tatu Jumapili hii. Ronaldo alituma ujumbe katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook akida alikuwa amejitoa kwa kila kitu kuisaidia nchi yake katika michuano hiyo pamoja na kuwa watoto wake walikuwa wamezaliwa. Nyota huyo aliendelea kudai kuwa amesikitishwa kwa kushindwa kufikia malengo waliyokuwa wamejiwekea lakini ana matumaini wataendelea kuwapa furahi mashabiki wa soka wa Ureno.

BARCELONA KUCHEZA NA CHAPECOENSE.

KLABU ya Barcelona inatarajiwa kuwa wenyeji wa Chapecoense katika mchezo wa kirafiki utakaofanyika Agosti 7 mwaka huu ili kutoa mchango wao kwa wale waliofariki dunia wakati ndege iliyokuwa imeibeba timu hiyo ya Brazil ilipoanguka Novemba mwaka jana. Wachezaji watatu pekee ndio waliosalimika katika ajali hiyo Novemba 29, wakati watu 71 kati ya 77 waliokuwepo ndani yake walifariki. Barcelona wamesema wanatarajia mchezo huo utaisaidia Chapecoense kujijenga kama taasisi na kurejea katika ushindani kama ilivyokuwa kabla ya ajali. Mshindi kwenye mchezo huo utakaofanyika katika Uwanja wa camp Nou anatarajiwa kupewa taji la Joan Gamper. Ajali hiyo ilitokea wakati Chapecoense wakisafiri kwenda kupambana na Atletico Nacional ya Colombia katika faiali ya Copa Sudamericana. Mabeki Neto na Alan Ruschel na kipa Jacson Follmann ambaye alikatwa mguu ndio miongoni mwa watu sita waliosalimika, wakati wachezaji 19 na benchi lote la ufundi walipoteza maisha.

ARTURO VIDAL AELEZA ALICHOWAAMBIA BRAVO KABLA YA KUOKOA PENATI TATU.

KIUNGO wa kikosi cha timu ya taifa ya Chile, Arturo Vidal amebainisha alichosema kipa Claudio Bravo kwa wachezaji wenzake kabla ya kuokoa penati tatu za Ureno katika nusu fainali ya Kombe la Shirikisho jana. Mchezo huo ulikwenda katika dakika za nyongeza kufuatia sare ya bila kufungana katika Uwanja wa Kazan Arena kabla ya kufikia hatua ya changamoto ya mikwaju ya penati ambayo iliivusha Chile katika hatua ya fainali. Ureno mabingwa wa Ulaya walijikuta wakipewa wakati mgumu kufuatia Bravo kupangua penati tatu za Ricardo Quaresma, Joao Moutinho na Nani. Akizungumza na wanahabari, Vidal amesema Bravo aliwaambia kabla ya penati kuwa ataokoa mbili au tatu na alifanya hivyo. Mara baada ya mchezo huo, Bravo alilalamika kuwa alikuwa ameumia lakini aliamua kuendelea ili kuisaidia timu yake kusonga mbele. Mabingwa hao wa Amerika Kusini sasa watakutana na aidha Ujerumani au Mexico katika hatua ya fainali itakayofanyika huko Krakow.

JINSI CHILE WALIVYOIANGAMIZA URENO.

Monday, June 26, 2017

MOURINHO AFIWA NA BABA YAKE.

BABA yake meneja wa Manchester United, Jose Mourinho aitwaye Felix Mourinho amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 79. Taarifa za kifo cha mzee huyo zimethibitishwa na klabu yake ya zamani ya Belenenses. Felix aliichezea klabu hiyo kwa kipindi kirefu akiwa kama kipa na baadae kupata nafasi ya kuichezea Ureno mara moja kabla ya kustaafu na kuanza kutafuta vipaji kazi ambayo ndio ilipelekea mwanae Jose kuja kujulikana na kuwa kocha bora duniani. Kufuatia kifo hicho Mourinho alituma picha akiwa na baba yake katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram bila kuweka ujumbe wowote. Mazishi ya Felix yanatarajiwa kufanyika huko Setubal kesho.

MONACO YAMKOMALIA MBAPPE.

KLABU ya AS Monaco imeendelea kujipanga kuhakikisha wanafanikiwa kumbakisha Kylian Mbappe kwa mwaka mmoja zaidi. Mabingwa hao wa Ufaransa siku zote wamekuwa wakieleza nia yao ya kubaki na chipukiz huyo mwenye umri wa miaka 18 pamoja na kuwaindwa na klabu mbalimbali Ulaya. Mbappe anawania na klabu nyingi kubwa Ulaya baada ya kufanya vyema katika msimu wake wa kwanza katika kikosi cha kwanza cha Monaco ambapo amefunga mabao 26. Real Madrid wako tayari kumfanya chipukizi huyo kuwa nyota wao mpya wa Galactico, wakati meneja wa Arsenal, Arsene Wenger naye anataka kumpeleka Emirates kwa ahadi ya kumpa nafasi ya kucheza mara kwa mara. Monaco wamekuwa wagumu kidogo kumuachia Mbappe kutokana na kuondoka kwa nyota wao kadhaa mpaka sasa ambao ni Bernardo Silva aliyekwenda Manchester City, Tiemoue Bakayoko anayetarajiwa kwenda Chelsea, wakati Binjamin Mendy, Thomas Lemar, Fabinho na Djibril Sidibe nao pia wanaweza kuondoka.

LYON YAKIRI ARSENAL KUMTAKA LACAZETTE.

RAIS wa klabu ya Olympique Lyon, Jean-Michel Aulas amesema Arsenal wako tayari kutoa fedha kwa ajili ya Alexandre Lacazette lakini yuko tayari kupambana kujaribu kumbakisha mshambuliaji huyo. Arsenal wamekuwa wakimtaka mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa kama mbadala wa Kylian Mbappe, kama meneja wa Arsene Wenger akishindwa kufanikiwa kumshawishi nyota huyo kutua Emirates. Wenger anaamini amefanikiwa kumshawishi Lacazette ambaye ameifungiwa Lyon mabao 37 msimu uliopita, kujiunga na Arsenal baada ya Atletico Madrid kukwama. Lacazette alikuwa ajiunge na klabu hiyo ya Hispania kipindi hiki cha majira ya kiangazi, lakini kufungiwa kusajili kulisitisha matumaini ya Atletico. Hata hivyo, Atletico wanadaiwa kuwa bado watamuwania nyota huyo Januari mwakani wakati adhabu ya kutosajili itakapomalizika.

DONNARUMMA KUZUNGUMZA NA MILAN.

WAKALA wa kipa chipukizi Gianluigi Donnarumma, Mino Raiola amedai kuwa mteja wake huyo anatarajia kukutana na AC Milan ili kuweka mambo sawa baada ya michuano ya Ulaya kwa vijana chini ya miaka 21. Awali kipa huyo alieleza kuwa hatasaini mkataba mpya pindi mkataba wake wa sasa utakapomalizika mwakani, lakini mapema jana alituma ujumbe katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram akidai kuwa atatoa nafasi nyingine ya majadiliano ya mkataba mpya. Hata hivyo, kipa huyo mwenye umri wa miaka 18, ambaye ameripotiwa kuwindwa na klabu za Juventus, Real Madrid na Manchester United baadae alidai kuwa akaunti yake ya Instagram ilidukuliwa kabla ya kuifuta. Akifafanua mkanganyiko huo, Raiola amesema anakuwa akiwasiliana na Donnarumma kama marafiki na baada ya michuano ya Ulaya wanatarajia kukutana na Milan.

BALOTTELLI AONGEZA MKATABA NICE.


MSHAMBULIAJI wa Nice, Mario Balotelli amesaini mkataba mpya wa mwaka mmoja na klabu hiyo ya Ligue 1. Nyota huyo wa kimataifa wa Italia, mwenye umri wa miaka 26, amefunga mabao 15 katika ligi msimu uliopita na kuiwezesha Nice kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye msimamo na kufuzu hatua ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao. Balotelli alisajiliwa na klabu hiyo akiwa mchezaji huru kutoka Liverpool Agosti mwaka jana, miaka miwili baada ya kusajiliwa Anfield kwa kitita cha paundi milioni 16. Mshambuliaji huyo wa zamani wa Manchester City pia amefunga mabao 13 katika mechi 33 alizoichezea timu ya taifa ya Italia lakini hajaitwa katika kikosi hicho toka kumalizika kwa michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2014.

MABINGWA WA AFRIKA CAMEROON HOI URUSI.

MABINGWA wa Afrika, Cameroon jana wameondoshwa katika michuano ya Kombe la Shirikisho inayoendelea nchini Urusi kwa kukubali kipigo cha mabao 3-1 kutoka kwa mabingwa wa dunia Ujerumani kwenye mchezo wa mwisho wa kundi B. Katika mchezo huo Cameroon walijikuta wakimaliza pungufu kufiatia nyota wao Ernest Mabouka kupewa kadi nyekundu kwa kumchezea vibaya Emre Can. Hata hivyo pamoja na kuomba usaidizi wa mfumo wa matumizi ya picha za video, mwamuzi wa mchezo huo Wilmar Roldan kutoka Colombia alitoa kadi kwa mchezaji asiye sahihi mpaka aliposisitizwa kurudia mara ya pili ndio akatoa kadi kwa mchezaji stahili. Katika hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo Ujerumani wanatarajiwa kupambana na Mexico huku mabingwa wa Ulaya Ureno wao wakicheza na mabingwa wa Amerika Kusini Chile mechi zitakazofanyika huko Sochi.

STARS WAANZA VYEMA COSAFA.

TIMU ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars imeanza vyema michuano ya Kombe la COSAFA baada ya kuididimiza kwa mabao 2-0 Malawi kwenye mchezo wa kundi A uliochezwa jana katika Uwanja wa Moruleng mjini Rusternburg, Afrika Kusini. Mabao mawili yaliyofungwa na kiungo Shiza Ramadhani Kichuya katika dakika ya 13 na 18 yalitosha kuihakikishia Stars ushindi huo muhimu kwenye mchezo huo. Stars sasa inaongoza kundi A kwa kujikusanyia alama tatu sambamba na Angola ambao nao walishinda bao 1-0 dhidi ya Mauritius jana. Timu moja pekee ndio itafuzu katika hatua ya robo fainali ya michuano hiyo ambapo watakwenda kukutana na Botswana, Zambia, Afrika Kusini, Namibia, Lesotho na Swaziland zilizofuzu hatua hiyo moja kwa moja. Kesho Stars inatarajiwa kupambana na Angola wakati Malawi wao watachuana na Mauritius kwenye mchezo mwingine wa kundi B.

Friday, June 23, 2017

MAPETO YA NGAO YA HISANI UINGEREZA KWENDA KWA WAATHIRIKA WA MOTO.

MAPATO kutoka katika mchezo wa Ngao ya Hisani nchini Uingereza mwaka huu yanatarajiwa kutolewa kwa ajili ya waathirika wa moto katika jingo la Grenfell Tower. Arsenal wanatarajiwa kucheza na Chelsea Agosti 6 mwaka huu katika Uwanja wa Wembley na kiasi cha paundi milioni 1.25 kinatarajiwa kukusanywa katika mchezo huo. Mwenyekiti wa Chama cha Soka cha Uingereza-FA, Greg Clarke amesema wana matumaini kiasi hicho kidogo watakachopata kupitia mchezo wa Ngao ya Hisani kinaweza kusaidia waathirika hao. Clarke amesema mchezo wa soka ni wa wote wana matumaini kwa njia zake yenyewe itaweza kurudisha hisani hiyo kidogo kwa wale wanaohitaji zaidi. Watu waliosalimika, familia za wahanga na watu waliotoa msaada wa dharura wanatarajiwa kualikwa katika mchezo huo kama wageni rasmi.

MESSI KULIPA FAINI BADALA YA KIFUNGO.

WAENDESHA mashitaka nchini Hispania wamekubali kubadilisha kifungo cha miezi 21 jela alichohukumiwa Lionel Messi kwa kosa la kukwepa kodi kwa kuamua kumtoza faini. Nyota huyo wa kimataifa wa Barcelona alipewa kifungo hicho Julai mwaka jana aada ya kukutwa na hatia ya makosa matatu ya kukwepa kodi sambamba na baba yake Jorge. Mahakama iliamua kuwa Messi kati ya mwaka 2007 na 2009 alikwepa kodi ya kiasi cha euro milioni 4.1 kutokana na mapato yake ya haki ya matumizi ya picha zake. Rufani kupinga adhabu hiyo ilitupiliwa mbali na Mahakama Kuu nchini Hispania Mei mwaka huu. Hata hivyo, taarifa zinadai kuwa waendesha mashitaka wamekubali kubadili kifungo hicho kwa faini ya euro 255,000.

NEYMAR ATENGANA NA MPENZI WAKE.

MSHAMBULIAJI nyota wa Barcelona, Neymar ametangaza kutengana na mpenzi wake Bruna Marquezine. Nahodha huyo wa kimataifa wa Brazil alirudiana na mpenzi wake huyo mwigizaji mwaka jana baada ya wawili kutengana mara ya kwanza mwaka 2014, ambapo Marquezine alikuwepo kushuhudia Neymar akiongoza nchi yake kutwaa medali ya dhahabu katika michuano ya Olimpiki iliyofanyika katika ardhi yao. Hata hivyo, akizungumza na wanahabari jijini Sao Paulo katika shughuli ya hisani, Neymar alikiri kuwa kwa mara nyingine wameamua kutengana. Neymar amesema huwa hapendi kuzungumzia masuala binafsi lakini ni kweli ameachana na Bruna na ilikuwa makubaliano ya pande zote mbili.

SALAH APEWA NAMBA YA COUTINHO LIVERPOOL.

KLABU ya Liverpool imefanikiwa kukamilisha usajili wa winga wa zamani wa Chelsea Mohamed Salah kutoka AS Roma. Nyota huyo wa kimataifa wa Misri mwenye umri wa miaka 25, amesaini mkataba wa miaka mitano na alikuwa chaguo namba moja la meneja Jurgen Klopp. Kiasi hicho cha usajili kimeshindwa kufikia rekodi ya paundi milioni 35 Liverpool ilizolipa kwa ajili ya Andy Carroll mwaka 2011 lakini kimefikia kiasi alichosajiliwa Sadio Mane mwaka 2016. Mwaka 2014 Salah ilibaki kidogo atue Anfield akitokea FC Basle lakini dili hilo lilishindikana na kwenda Chelsea.

Thursday, June 22, 2017

BALOTELLI KUBAKIA NICE.

RAIS wa Nice, Jean-Pierre Rivere amedai kuwa Mario Balotelli yuko tayari kubakia katika klabu hiyo hata kwa kupunguziwa mshahara wake. Balotelli ambaye alitua Nice Agosti mwaka jana akiwa mchezaji huru kufuatia kuachwa na Liverpool, mkataba wake unatarajiwa kumalizika wiki ijayo. Baada ya kufunga mabao 15 msimu uliopita na kuiwezesha Nice kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligue 1, nyota huyo wa kimataifa wa Italia anataka kuendelea kubakia hapo pamoja na kuwaniwa na Marseille na timu kutoka Uturuki. Akizungumza na wanahabari mapema leo, rais huyo amesema Balotelli ataka kuendelea kubakia Nice na yuko tayari kushiorikiano nao kifedha ili aendelee kufanya nao kazi.

JUVENTUS YAKIRI KUPOKEA OFA YA SANDRO.

KLABU ya Juventus imedai kupokea ofa kubwa kwa ajili ya Alex Sandro na hawatamzuia beki huyo wa kushoto kuondoka katika timu hiyo kama akitaka. Mabingwa wa Ligi Kuu Chelsea wamekuwa wakihusishwa na tetesi za kumuwania beki huyo wa kimataifa wa Brazil mwenye umri wa miaka 26. Meneja wa Chelsea, Antonio Conte alikuwa akiinoa Juventus wakati walipomsajili Sandro kwa kitita cha paundi milioni 23 kutoka FC Porto mwaka 2015. Ofisa mkuu wa Juventus, Giuseppe Marotta amesema kama mchezaji ataamua kuondoka hawawezi kumzuia. Sandro alikuwepo katika kikosi cha Juventus kilichofungwa katika hatua ya fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid msimu uliopita.

TIMU YA SOKA YA CHINA KUCHEZA LIGI UJERUMANI.

Ligi Daraja la Nne nchini Ujerumani, inatarajiwa kufanya jambo la kipekee msimu ujao kwa kuongeza timu kutoka China kuwa miongoni mwa timu 20 zitakazoshiriki ligi hiyo. Chama cha Soka cha Ujerumani-DFB kilifikia makubaliano nawashirika wao Chama cha Soka cha China-CFA Novemba mwaka jana kuhusu mpango huo. Makamu wa rais wa DFB, Ronny Zimmermann alikaririwa na jarida la Kicker akidai kuwa klabu zote zinazoshiriki ligi hiyo zimekubaliana na mpango huo. Timu hiyo kutoka China itakuwa sio klabu badala yake itakuwa ni kundi la wachezaji walio chini ya umri wa miaka 20. Timu hiyo haitarajiwi kuwa na uwanja wake wa nyumbani na haijawekwa wazi wataweka kambi yao wapi ingawa kila klabu inatarajiwa kucheza mechi mbili za nyumbani dhidi yao. Timu hiyo itakuwa ikicheza nje ya mashindano kwa maana kuwa hawataweza kupandishwa daraja wala kushushwa.

JUVENTUS MBIONI KUNASA MSHAMBULIAJI WA SAMPDORIA.

KLABU ya Juventus inatarajia kukamilisha usajili wa Patrik Schick wa euro milioni 25 kutoka Sampdoria baada ya nyota huyo kuwasili jijini Turin kwa ajili ya vipimo vya afya leo. Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 21 amefunga mabao 11 katika mechi 32 za Serie A alizoichezea Sampdoria toka alijiunga nao kwa kitita cha euro milioni nne akitokea Sparta Prague. Ingawa nyota huyo wa kimataifa wa Jamhuri ya Czech alikuwa na mkataba na Sampdoria unaomalizika mwaka 2020, lakini kwa kipindi kirefu amekuwa akihusishwa na tetesi za kuwaniwa na klabu kadhaa zikiwemo Juventus, Inter na Tottenhma Hotspurs. Mapema hivi karibuni alikiri kuwa upo uwezekano wa kuhamia Juventus na sasa suala hilo linaonekana kukaribia kukamilika.

NDUGU WA MBAPPE AELEZA NDUGUYE ANAWEZA KWENDA ARSENAL.

NDUGU wa karibu wa Lylian Mbappe amekiri nyota huyo wa Monaco anaweza kujiunga na Arsenal kipindi hiki cha majira ya kiangazi na kusisitiza kutokuwepo katika michuano ya Ligi ya Mabingwa kwa klabu hiyo sio tatizo. Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger alikaribia kumsajili Mbappe kiangazi mwaka jana lakini mshambuliaji huyo aliamua kubakia kwa mwaka mwingine zaidi. Nyota huyo ambaye amefunga mabao 26 msimu uliopita amezivutia klabu kubwa barani Ulaya zikiwemo Real Madrid na Barcelona. Awali ilikuwa ikihofiwa kuwa kushindwa kwa Arsenal kufuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya kunaweza kuwanyima nafasi ya kumsajili nyota huyo.

OSCAR AFUNGIWA MECHI NANE KWA VURUGU CHINA.

MSHAMBULIAJI wa zamani wa Chelsea, Oscar amefungiwa kutocheza mechi nane na Chama cha Soka cha China-CAF kufuatia kuzusha vurugu katika mchezo ambao timu yake ya Shanghai SIPG ilitoka sare ya bao 1-1 Jumapili iliyopita. Nyota huyo wa kimataifa wa Brazil, alipiga mpira kwa makusudi kuwalenga wachezaji wawili wa Guangzhou R&F na kusababisha tafrani kubwa kati ya wachezaji wa timu zote mbili. Oscar sasa anatarajiwa kutumikia adhabu hiyo mpaka Agosti 13 huku pia akitozwa faini ya dola 5,000 kutoka tukio hilo. Awali CFA walikuwa hawafamu ni jinsi gani haswa kumuadhibu kiungo huyo na walilazimika kuliandikia Shirikisho la Soka Duniani-FIFA kuwaomba ushauri kutokana na tukio hilo. Oscar ameichezea SIPG mechi 21 na kufanikiwa kufunga mabao manne na kusaidia mengine 10.

JUVENTUS KUMUACHIA DANI ALVES.

KLABU ya Juventus imethibitisha itamuacha beki wake wa kulia Dani Alves pamoja na kuwa amebakisha mkataba wa mwaka mmoja. Meneja huyo wa Manchester City, Pep Guardiola anadaiwa kumuwania nyota huyo mwenye umri wa miaka 34, ambaye walikuwa wote Barcelona. Ofisa mkuu wa Juventus, Beppe Marotta amesema Alves anataka kutafuta changamoto mpya hivyo ana matumaini watafikia muafaka kwenye suala lake ili aweze kutimiza ndoto zake. Marotta aliendelea kudai kuwa wanamtakia kila la heri beki huyo ambaye wamekuwa naye kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Tuesday, June 20, 2017

USAJILI WA SALAH WANUKIA LIVERPOOL.

WINGA wa kimataifa wa Misri, Mohamed Salah anategemewa kukamilisha usajili wake kwenda Liverpool akitokea AS Roma Alhamisi baada ya kutua nchini Uingereza leo kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya afya. Taarifa zilizotoka jana zimedai kuwa Liverpool bado wanamalizia majadiliano na Roma kuhusu uhamisho huo unaotarajiwa kuwagharimu kiasi cha paundi milioni 39. Usajili huo ukikamilika utakuwa umezidi ule wa Andy Carroll wa paundi milioni 35 uliofanyika Januari mwaka 2011. Kama kila kitu kikienda kama kilivyopangwa mpaka ifikapo Juni 22 Salah mwenye umri wa miaka 25 atakuwa amesaini mkataba wa miaka mitano ambao utamfanya kukunja kitita cha paundi 90,000 kwa wiki.

BAADA YA RONALDO, MOURINHO NAYE ATUHUMIWA KUKWEPA KODI.

MENEJA wa Manchester United, Jose Mourinho anatuhumiwa kwa makosa ya kukwepa kodi kufuatia uchunguzi wa waendesha mashitaka wa Hispania wakati akiifundisha Real Madrid. Mourinho raia wa Ureno anatuhumiwa kukwepa kodi inayokadiriwa kufikia paundi milioni 2.9 kati ya mwaka 2011 na 2012 ambapo bado hajatoa kauli yeyote kuhusiana na tuhuma hizo. Waendesha mashitaka wamedai kuwa hakuweka wazi mapato yake kwa ajili ya haki ya matumizi ya picha zake. Hivi karibuni majina kadhaa makubwa katika soka yamekuwa yakituhumiwa kukwepa kodi nchini Hispania. Miongoni mwa majina hayo ni nyota wa Madrid Cristiano Ronaldo ambaye anatarajiwa kufikishwa kizimbani kutoa utetezi wake Julai 31 mwaka huu.

CONTE KUSAINI MKATABA MPYA BAADA YA CHELSEA KUKUBALI KUTOA FUNGU LA USAJILI.

MENEJA wa Chelsea, Antonio Conte anatarajiwa kusaini mkataba mpya wa paundi milioni 9.5 ili kuendelea kubaki katika klabu hiyo mpaka mwaka 2021 baada ya kuhakikishiwa kuwa atapewa fungu la kusajili kufuatia kutoelewana wiki iliyopita. Mkurugenzi wa Chelsea Marina Granovskaia ameonekana kumaliza tofautia na Conte Jumapili iliyopita kufuatia kudokeza suala la usajili na mkataba mpya wa meneja huyo. Conte anatarajiwa kuwa meneja wa saba anayelipwa zaidi duniani na watu kwa nchini Uingereza kama akitia saini mkataba huo mpya. Hivi karibuni kulikuwa kumezuka tetesi za mustakabali wa Conte kufuatia Muitaliano huyo kuweka wazi kutofurahishwa na jinsi suala la usajili lilivyo katika klabu hiyo. Conte anatarajiwa kurejea kutoka likizo Julai 7 mwaka huu kwa ajili ya kuanza maandalizi ya msimu mpya kabla ya Chelsea haijakutana na Arsenal katika mchezo wa Ngao ya Hisani.

MCHAKATO WA UCHUKUAJI FOMU TFF.

WAKATI leo Jumanne Juni 20, 2017 itakuwa mwisho wa kuchukua na kurejesha fomu kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), wagombea 62 tayari wamejitokeza. Wanafamilia hao ni wale waliojitokeza kuanzia Ijumaa iliyopita Juni 16, mwaka huu wakiongozwa na Jamal Malinzi aliyekuwa wa kwanza kuchukua fimu kati ya wagombea tisa walioomba nafasi hiyo. Fomu hizo zinachukuliwa na kurejeshwa katika ofisi za TTF, Karume jijini Dar es Salaam na Uchaguzi wa TFF utakafanyika Agosti 12, mwaka huu mkoani Dodoma. Mbali ya Malinzi, wengine waliochukua fomu hizo ni Imani Madega, Wallace Karia, Fredrick Masolwa, Athumani Nyamlani, Fredrick Mwakalebela na Ally Mayay wakati waliojitokeza kuwania Makamu wa Rais wako Mulamu Nghambi, Michael Wambura, Geofrey Nyange, Mtemi Ramadhani na Robert Selasela.


Wajumbe wa Kamati ya Utendaji kwa kufuata Kanda 13 ni kama ifuatavyo:

Kanda Na. 1 Mikoa ya Kagera na Geita;
Soloum Chama
Kaliro Samson
Samwel Daniel
Leopold Mukebezi
Abdallah Mussa

Kanda Na. 2 Mikoa ya Mara na Mwanza;
Vedastus Lufano
Ephraim Majinge

Kanda Na. 3 Mikoa ya Shinyanga na Simiyu;
Benista Rugora
Mbasha Matutu
Stanslaus Nyongo

Kanda Na. 4 Mikoa ya Arusha na Manyara;
Omari Walii
Sarah Chao
Peter Temu

Kanda Na. 5 Mikoa ya Kigoma na Tabora;
John Kadutu
Issa Bukuku
Abubakar Zebo


Kanda Na. 6 Mikoa ya Katavi na Rukwa;
Kenneth Pesambili
Baraka Mazengo

Kanda Na. 7 Mikoa ya Mbeya na Iringa;
Elias Mwanjala
Cyprian Kuyava
Erick Ambakisye

Kanda Na. 8 Mikoa ya Njombe na Ruvuma;
James Mhagama
Golden Sanga
Vicent Majili

Kanda Na. 9 Lindi na Mtwara;
Athuman Kambi
Dunstan Mkundi


Kanda Na. 10 Mikoa ya Dodoma na Singida;
Hussein Mwamba
Mohamed Aden
Musa Sima
Stewart Masima
Ally Suru

Kanda Na. 11 Mikoa ya Pwani na Morogoro;
Charles Mwakambaya
Gabriel Makwawe
Francis Ndulane


Kanda ya 12. Mikoa ya Kilimanjaro na Tanga
Khalid Mohamed
Goodluck Moshi

Kanda Na. 13 Mkoa wa Dar es Salaam
Emmanuel Ashery
Ayoub Nyenzi
Saleh Alawi
Shaffih Dauda
Thabit Kandoro
Abdul Sauko
Peter Mhinzi
Ally Kamtande
Said Tully
Mussa Kisoky
Lameck Nyambaya
Ramadhani Nassib
Aziz Khalfan



GHARAMA ZA KUCHULIA FOMU.
1. Rais TSHS 500,000/=
2. Makamu wa Rais TSHS 300,000/=
3. Wajumbe wa kamaki ya utendaji TSHS 200,000/-

SIFA ZA WAGOMBEA.

1. Awe raia wa Tanzania.
2. Awe na kiwango cha elimu kisichopungua kidato cha nne (Cheti cha Elimu ya Sekondari).
3. Awe na uzoefu wa uendeshaji Mpira wa Miguu uliothibitishwa wa angalau miaka mitano.
4. Asiwe na hatia yoyote ya kosa la jinai na asiwe amewahi kuhukumiwa kifungo kisicho na mbadala wa faini.
5. Awe na umri angalau miaka 25.
6. Awe amewahi kuwa ama Mchezaji Mpira wa Miguu, Kocha, Mwamuzi. Au kushiriki katika uendeshaji wa Mpira wa Miguu angalau katika ngazi ya Mkoa au ngazi ya daraja la kwanza.
7. Awe muadilifu na muaminifu mwenye uwezo wa utendaji katika utekelezaji na utimizaji wa majukumu na malengo ya TFF.
8. anayegombea nafasi ya Rais au makamu wa Rais awe na kiwango cha elimu kisichopungua shahada moja, mwenye utu na uwezo wa kuiwakilisha TFF ndani na nje ya nchi.

Mwisho wa kuchukua na kurudisha fomu ni tarehe 16-20/06/2017 saa kumi (10:00) jioni.

OZIL AONYESHA DALILI ZA KUBAKI ARSENAL.

KIUNGO wa Arsenal, Mesut Ozil amedokeza kubaki Emirates kwa kuzungumzia ziara yao ya maandalizi ya msimu mpya huko Australia. Mustakabali wa nyota huyo wa kimataifa wa Ujerumani bado haujakaa sawa kufuatia mkataba wake kutarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu ujao. Bado hajakubali kusaini mkataba mpya lakini Ozil alweka pembani suala la yeye kuondoka na kuzungumzia jinsi alivyokuwa na hamu kubwa ya kusafiri na timu hiyo katika ziara la maandalizi ya msimu ujao. Akizungumza na wanahabari, Ozil amesema amesikia Sydney ni mji mzuri na kuna watu wengi wazuri wanaishi kule. Ozil aliendelea kudai kuwa hafahamu sana kuhusu Australia lakini ziara hiyo itakuwa nafasi nzuri ya kuona mji, watu na anafurahia kwenda huko na Arsenal.

RAIS WA MADRID KUTETA NA RONALDO.

RAIS wa Real Madrid, Florentino Perez amesema hajazungumza na Cristiano Ronaldo kuhusu mustakabali wake lakini anatarajia kufanya hivyo baada ya kumalizika kwa michuano ya Kombe la Shirikisho. Ronaldo mwenye umri wa miaka 32 anadaiwa kutaka kuondoka Hispania baada ya kutuhumiwa na makosa ya ukwepaji kodi. Mshambuliaji huyo ambaye yuko nchini Urusi na kikosi cha timu ya taifa ya Ureno, alisaini mkataba mpya wa miaka mitano Novemba mwaka jana lakini amekuwa akihusishwa na tetesi za kurejea Manchester United. Perez ambaye alichaguliwa tena kuiongoza klabu hiyo jana, amesema jambo pekee analoweza kusema ni kuwa Ronaldo ni mchezaji wa Madrid. Perez aliendelea kudai kuwa kwasasa hataki kuisumbua timu ya Ureno kwakuwa wako katika michuano muhimu hivyo atasubiri mpaka itakapomalizika.

DANI ALVES ANUKIA MAN CITY.

BEKI wa kimataifa wa Brazil, Dani Alves anadaiwa kukubali mkataba wa miaka miwili na Manchester City na uhamisho wake unatarajiwa kuthibitishwa pindi mazungumzo ya kuvunja mkataba wake Juventus yatakapokamilika. Alves alikutana na maofisa wa Juventus jana mchana ili kueleza mpango wake wa kuondoka. Taarifa zinadai kuwa City wanaweza kulipa kiasi kidogo cha fedha kinachokadiriwa kufikia paundi milioni tano kwa ajili ya kunasa saini beki huyo. Taarifa kutoka nchini Italia zinadai kuwa Alves atakuwa akilipwa kiasi cha paundi milioni 4.3 kwa mwaka kiasi ambacho bdio ofa aliyopewa Nolito majira ya kiangazi mwaka jana.

FIFA WATETEA MFUMO VAR.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA limetetea matumizi ya mfumo wa picha za video kumsaidia mwamuzi-VAR katika michuano ya Kombe la Shirikisho wakidai kuwa teknologia hiyo ni kwajili ya soka lijalo. Mfumo huo umeshatumika mara tano mpaka sasa katika michuano hiyo inayoendelea nchini Urusi, na kusababisha mkanganyiko miongoni mwa mashabiki. Rais wa FIFA, Gianni Infantino amesema tumeona jinsi gani mfumo huo unavyosaidia waamuzi kufanya maamuzi sahihi. Infantino aliongeza kuwa anafurahia jinsi VAR inavyofanya kazi mpaka sasa katika michuano hiyo. Mfumo wa VAR ulianza kutambulishwa rasmi kwa mara ya kwanza katika michuano ya Klabu Bingwa ya Dunia ya FIFA iliyofanyika Japan Desemba mwaka jana.

Monday, June 19, 2017

WILSHERE "AVUTA JIKO".

KIUNGO wa Arsenal, Jack Wilshere amefunga ndoa na mpenzi wake wa siku nyingi Andriani Michael katika sherehe kubwa ya siku tatu iliyofanyika nchini Italia. Wilshere alituma picha akiwa na mpenzi wake huyo kwenye harusi katika mitandao ya kijamii huku kukiwa na ujumbe wa kuwashukuru wale wote walioshirikiana naye kwenye siku yake hiyo muhimu. Wawili hao walifunga ndoa huko Tuscany, huku mwanamuziki nyota wa Uingereza Graig David akitumbuisha katika sherehe hizo. Sherehe hiyo ilihudhuriwa na familia pamoja na marafiki zake wa karibu akiwemo Benik Afobe, Wjciech Szczesny, Danny Welbeck na Dan Crowley ambao wote amecheza nao Arsenal.

IBRAHIMOVIC ANA OFA KIBAO - RAIOLA.

WAKALA Mino Raiola amesema mteja wake Zlatan Ibrahimovic angekuwa tayari amesharejea AC Milan kama Adriano Galliano angekuwa katika klabu hiyo, lakini amesisitiza nyota huyo ana ofa kibao mezani za kuchagua. Ibrahimovic amekuwa mchezaji huru baada ya kuachwa na Manchester United wakati akiendelea kujiuguza jeraha la goti alilopata Aprili mwaka huu. Ingawa nyota huyo mwneye umri wa miaka 35 atakuwa nje ya uwanja kwa miezi kadhaa, tayari ameshahusishwa na tetesi za kuwaniwa na klabu mbalimbali ikiwemo suala la kurejea Italia. Kwa mujibu wa wakala wake Inter, Juventus na Milan zote zingeweza kuwa chaguo lake. Raiola amesema Ibrahimovic anaendelea vyema hivi sasa na ameshapokea ofa nyingi kutoka Marekani na sehemu nyinginezo.

LIVERPOOL YAMUWANIA AUBAMEYANG.

TAARIFA kutoka nchini Ufaransa zinadai kuwa Liverpool inajipanga kumuwania mshambuliaji wa Borussia Dortmund Pierre-Emerick Aubameyang. Taarifa hizo zimeongeza kuwa Jurgen Klopp anafikiria kuungana tena na mashambuliaji huyo Anfield baada ya kuwahi kumfundisha wakati wakiw ote Dortmund. Liverpool inajipanga kuimarisha kikosi chake kwa kiasi kikubwa kutokana na ushiriki wao katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao na tayari Aubameyang alishaeleza nia yake ya kuondoka Dortmund kama ofa sahihi ikipatikana. Aubameyang alifunga mabao 42 kwa klabu na nchi yake msimu uliopita na ni mmoja kati ya washambuliaji wanaohofiwa barani Ulaya.

PEREZ KUENDELEA KUWA RAIS WA MADRID.

RAIS wa Real Madrid, Florentino Perez anatarajia kuendelea na wadhifa wake huo mpaka mwaka 2021 baada ya kutojitokeza mgombea yeyote wa kugombea nafasi hiyo. Perez ambaye mara ya kwanz akushika wadhifa huo ilikuwa ni mwaka 2000, amefanikiwa kupita bila kupingwa katika taarifa iliyotolewa na mabingwa hao wa Hispania na Ulaya mapema leo. Perez mwenye umri wa miaka 70 ameendelea kuchagiza mafanikio katika klabu hiyo baada ya kutwaa taji la tatu la michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya katika kipindi cha misimu minne iliyopita. Madrid pia walifanikiwa kutwaa taji la La Liga kwa mara ya kwanza toka mwaka 2012.

KIPA WA AC MILAN ATISHIWA KUUAWA.

WAKALA maarufu Mino Raiola amedai kuwa kipa wa AC Milan Gianluigi Donnarumma ametumia vitisho vya kuuwawa wakati wa majadiliano ya nyongeza ya mkataba. Mapema wiki iliyopita mvutano ulikuwa mkubwa baada ya Milan kutangaza kuwa kipa huyo mwenye umri wa miaka 18 ameamua kutoongeza mkataba mwingine mpya zaidi ya ule wa awali unaomalizika mwaka 2018. Taarifa zinadai kuwa kipa huyo anayedaiwa kuwa na kipaji cha kipekee alikataa ofa ya mshahara wa euro milioni tano kwa mwaka jambo ambalo lilizua hisia mbaya miongoni mwa mashabiki wa timu hiyo. Akizungumza na wanahabari, Raiola amesema Donnarumma ametishiwa na familia yake imetishiwa hivyo hadhani kama mchezaji huyo ataendelea kubaki Milan. Raiola aliendelea kudai kuwa uongozi wa Milan ulikosea jinsi ya kujadili nyongeza ya mkataba na kipa huyo ndio maana hali imekuwa hivyo.

RONALDO AMTAKA WAKALA WAKE KUFANYA MIPANGO YA KUREJEA OT.

MSHAMBULIAJI wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo anaripotiwa kumtaka wakala wake Jorge Mendes kuhakikisha anafanya mipango ya yeye kurejea Manchester United. Nyota huyo wa kimataifa wa Ureno bado ameendelea kuhusishwa na tetesi za kurejea Old Trafford baada ya kufanya maamuzi ya kutaka kuondoka Madrid. Ronaldo amekuwa akituhumiwa kukwepa kodi nchini Hispania inayokadiriwa kufikia paundi milioni 13, hivyo kuamua kuondoka La Liga. Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na gazeti la The Sun, nyota huyo anataka kurejea United na amemtaka wakal wake kuhakikishia anafanikisha suala hilo. Ronaldo alijiunga na United mwaka 2003 akiwa na umri wa miaka 18 na kufanikiwa kufunga mabao 118 katika mechi 292 alizoichezea timu hiyo kwa kipindi cha miaka sita. Mwaka 2009 alihamia Madrid na kuja kuwa mfungaji bora wakati wote wa timu hiyo kwa kufunga mabao 406 katika mechi 394 alizocheza mpaka sasa. Taarifa zingine zilizotoka mapema leo zimedai kuwa United wako tayari kutoa kitita cha paundi milioni 175 kwa ajili ya usajili huo kipindi hiki cha kiangazi pamoja na kumruhusu David de Gea kwenda Madrid.

KOCHA WA CHILE ALAUMU MFUMO WA VAR.

KOCHA wa timu ya taifa ya Chile, Juan Antonio Pizzi anadhani mfumo wa matumizi wa picha video kumsaidia mwamuzi-VAR uliwaathiri wachezaji wake na kufanya kupata tabu kuwafunga Cameroon katika mchezo wao wa Kombe la Shirikisho uliochezwa jana usiku. Mabingwa wa Amerika Kusini walishuhudia bao zuri la Eduardo Vargas katika kipindi cha kwanza likikataliwa baada ya mfumo huo wa VAR kutumika na kuonekana kuwa alikuwa ameotea. Hata hivyo, baadae Vargas alinufaika baada ya VAR kukataa maamuzi ya mshika kibendera na kuamua kuwa Alexis Sanchez alikuwa hajaotea wakati akitengeneza mazingira ya bao la pili. Bao hilo la Vargas liliifanya Chile kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 ambapo la kwanza lilifungwa na Alex Vidal aliyemalizia pasi safi ya Sanchez. Pizzi amesema anadhani mfumo huo unahitaji muda kwani hata wachezaji wake walionekana kuathirika kwa kiasi fulani.

Thursday, June 15, 2017

HUDDERSFIELD YAANZA USAJILI KWA KISHINDO.

KLABU ya Huddersfield iliyopanda Ligi Kuu ya Uingereza msimu huu imekubali kutoa ada ilitakayovynja rekodi ya klabu hiyo ya paundi milioni 10 kwa ajili ya kiungo wa kimataifa wa Australia Aaron Mooy kutoka Manchester City. Mooy mwenye umri wa miaka 26 aliitumikia Huddersfield kwa mkopo msimu uliopita na alicheza pia mchezo wa mwisho wa mtoano dhidi ya Reading ambao walishinda na kujihakikishia nafasi ya kukwea Ligi Kuu. Taarifa zinadai kuwa Huddersfield watatoa kitita cha paundi milioni nane awali na paundi milioni mbili zilizobaki watalipa baadae. Mooy alijiunga na City akitokea klabu ya Melbourne City miezi 12 iliyopita kwa mkataba wa mitatu.

JUVENTUS YAPELEKA NGUVU KWA COSTA BAADA YA KUMNASA N'ZONZI.

MENEJA wa Juventus, Massimiliano Allegri amethibitisha kuwa klabu hiyo inataka kumsajili winga wa Bayern Munich Douglas Costa. Nyota huyo wa kimataifa wa Brazil hana furaha Bayern baada ya kushindwa kupata nafasi kwenye kikosi cha kwanza katika siku za karibuni na kukiri kuwa anafikiria kuondoka. Akizungumza na wanahabari, Allegri amesema Douglas Costa yuko katika mipango yao ya usajili kwani ni mchezaji mzuri lakini hakuna lolote liliafikiwa mpaka sasa. Wakati huohuo kluna taarifa kuwa kiungo wa Sevilla Steven N’Zonzi amekubali kujiunga na klabu hiyo kipindi hiki cha majira ya kiangazi. N’Zonzi ambaye alikuwa akihusishwa na tetesi za kuwaniwa na Barcelona, amekuwa akicheza kwa kiwango kikubwa msimu uliopita chini Jorge Sampaoli kwa kufunga mabao matatu katika mshindano yote na kusaidia mengine matatu.

PSG WAKIRI KUMUWINDA MBAPPE.

MENEJA wa Paris Saint-Germain-PSG, Unai Emery amemtaka mshambuliaji wa AS Monaco Kylian Mbappe kusajiliwa na klabu yake. Nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa mwenye umri wa miaka 18, amekuwa akiwani klabu mbalimbali barani Ulaya huku dau lake likidaiwa kufikia euro milioni 120. Klabu za Real Madrid na Arsenal zimekuwa zikipigana vikumbo kuwania kumsajili chipukizi huyo lakini Emery amekiri kuwa anataka mchezaji ahamie PSG. Akizungumza na wahabari, Emery amesema ukimzungumzia Mbappe nchini Hispania lazima utazitaja klabu za Real Madrid na Barcelona lakini kwakuwa yeye anafundisha PSG angependa nyota huyo aiwakilishe timu yake. Emery aliendelea kudai kuwa pamoja na kluiheshimu Monaco lakini anadhani Mbappe anastahili kwenda PSG kwani familia yake iko kule na pia alianza katika akademi ya huko.

SOUTHAMPTON WAMTIMUA KOCHA WAO.

KLABU ya Southampton imemtimua rasmi meneja wake Claude Puel baada ya kuinoa timu hiyo kwa msimu mmoja. Meneja huyo mwenye umri wa miaka 55 raia wa Ufaransa, ambaye aliteuliwa kushika nafasi hiyo Juni mwaka jana, aliiongoza Southampton kushika nafasi ya nane katika msimamo wa Ligi Kuu msimu uliopita pamoja na kupotez amechi 16. Southampton pia ilifanikiwa kutinga fainali ya Kombe la Ligi ikiwa ni fainali yao ya kwanza kubwa toka mwaka 2003. Katika taarifa ya klabu hiyo imedai kuwa mchakato wa kutafuta kocha mpya tayari umeanza na wana uhakika watapata chaguo sahihi. Puel aliinoa Nice kwa mwaka mmoja kabla ya kuja kuchukua nafasi ya Ronald Koeman aliyeingoza Southampton kushika nafasi ya sita katika msimamo wa ligi msimu wa 2015-2016.

BIRMINGHAM WAMTUPIA NDOANO JOHN TERRY.

MENEJA wa Birmingham, Harry Redknapp amedai kuwa klabu hiyo imetuma ofa ya mkataba kwa nahodha wa zamani wa kimataifa wa Uingereza na Chelsea, John Terry. Terry mwenye umri wa miaka 36 aliondoka Chelsea mwishoni mwa msimu uliopita baada ya kuichezea mechi 717 na kufanikiwa kushinda mataji 13 katika kipindi cha miaka 22.  Hata hivyo, Terry alifanikiwa kucheza mechi 14 pekee akiwa na Chelsea msimu uliopita. Akizungumza na wanahabari, Redknapp amesema wamemtengea Terry ofa nzuri na wamefanya kila wanaloweza hivyo ni juu ya mchezaji mwenyewe kuamua kuipokea au kuacha.

Wednesday, June 14, 2017

SUPER AGENT JORGE MENDES AITWA MAHAKAMANI.

WAKALA maarufu, Jorge Mendes ambaye miongoni mwa wachezaji anaowasimamia yupo Cristiano Ronaldo, ameitwa mahakamani nchini Hispania kufuatia tuhuma za ukwepaji kodi zinazomkabili mshambuliaji wa kimataifa wa Colombia Radamel Falcao. Falcao anayecheza soka lake katika klabu ya Monaco hivi sasa, anatuhumiwa kushindwa kuweka wazi mapato yake ya euro milioni 5.6 zilizotokana na haki ya matumizi ya picha zake kati ya mwaka 2012 na 2013 wakati akiwa Atletico Madrid. Falcao anatuhumiwa kutumia kampuni za nje ikiwemo Visiwa vya Virgin, Ireland, Colombia na Panama ili kukwepa kodi. Mendes ameitwa kutoa ushahidi mahakamani Juni 27 mwaka huu jijini Madrid. Wito huo umekuja ikiwa imepita siku moja baada ya Ronaldo naye kutuhumiwa na Waendesha Mashitaka nchini Hispania kukwepa kodi ya euro milioni 14.7 kupitia kampuni za nje.

LINDELOF ATUA OLD TRAFFORD KUKAMILISHA USAJILI WAKE.

BEKI wa kimataifa wa Sweden, Victor Lindelof ametua katika uwanja wa mazoezi wa Manchester United kuelekea kukamilisha uhamisho wake wa paundi milioni 30. United imethibitisha kuwa tayari kumsajili beki huyo, ambaye atakuwa mchezaji wa kwanza kusajiliwa na Jose Mourinho kipindi hiki cha majira ya kiangazi. Lindelof amewasili katika uwanja wa mazoezi wa United wa AON kufanyiwa vipimo vya afya ili kukamilisha usjaili wake kutoka Benfica ya Ureno. Taarifa zinadai kuwa Lindelof amekubali mkataba wa miaka minne Old Trafford huku kukiwa na kipengele cha kuongezewa.

ROMA YAMCHUKUA DI FRANCESCO.

KLABU ya AS Roma imetangaza kumteua Eusebio di Francesco kuwa meneja wao mpya kwa mkataba wa miaka miwili. Meneja huyo mwenye umri wa miaka 47 raia wa Italia, anachukua nafasi ya Luciano Spalletti ambaye alijiuzulu mwishoni mwa msimu huu na kwenda kuwa meneja wa Inter Milan. Di Francesco ambaye aliisaidia Roma kutwaa taji la Serie A msimu wa 2000-2001 wakati huo akicheza nafasi ya kiungo, amesema amefurahi kurejea katika klabu hiyo baada ya kupita miaka mingi. Di Francesco aliisaidia Sassoulo kupanda katika Serie A mwaka 2013 na msimu uliopita aliiwezesha kushika nafasi ya 12 katika msimamo wa ligi. Roma ambao wamemsajili beki wa Mexico Hector Moreno kutoka PSV Eindhoven hivi karibuni, walimaliza katika nafasi ya pili msimu uliopita na wanatarajiwa kushiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.

LEICESTER YANASA BEKI KUTOKA HULL CITY.

KLABU ya Leicester City inatarajiwa kutangaza usajili wa beki wa Hull City Harry Maguire ambao umewagharimu kiasi cha paundi milioni 17. Taarifa kutoka nchini Uingereza zinadai kuwa Leicester wanatarajia kutoa paundi milioni 12 mwanzo huku nyingine ikitarajiwa kulipwa kwa makubaliano na tayari nyota huyo ameshakamilisha vipimo vya afya. Maguire mwenye umri wa miaka 24, alifunga mabao matatu katika mechi 36 alizoichezea Hull City iliyoteremka daraja msimu uliopita. Beki huyo wa kati ambaye alijiunga na Hull City kwa kitita cha paundi milioni 2.5 akitokea Shiffield United mwaka 2014 alikuwa amebakisha mwaka mmoja katika mkataba wake.

REAL MADRID YAMUUNGA MKONO RONALDO TUHUMA ZA KUKWEPA KODI.

KLABU ya Real Madrid imedai kumuunga mkono kwa asilimia 100 Cristiano Ronaldo baada ya mshambuliaji huyo kutuhumiwa kukwepa kodi na Mamlaka za Hispania. Mapema jana waendesha mashitaka wa Madrid walifungua kesi katika mahakama ya Pozuel de Alarcon wakimtuhumu Ronaldo kwa kukwepa kodi. Katika taarifa yao, Madrid wamedai kuwa toka Ronaldo atue katika klabu hiyo alionyesha ushirikiano wa wazi wa kufanya majukumu yake yote yahusuyo kodi hivyo klabu ina uhakika kuwa nyota wao huyo atakutwa hana hatia yeyote kwenye suala hilo. Tuhuma za Ronaldo zinakuja kufuatia nyota wa Barcelona Lionel Messi naye kuhukumiwa hivi karibuni kwa makosa kama hayo. Messi alikutwa na hatia mwaka jana na kuhukumiwa miezi 21 jela, lakini hataitumikia adhabu hiyo jela kwakuwa adhabu zote za chini ya miaka miwili mfungwa hupewa kifungo cha nje.