Friday, July 31, 2015

CHELSEA VS ARSENAL NGAO YA JAMII JUMAPILI.

PAZIA la Ligi Kuu nchini Uingereza, linatarajiwa kufunguliwa mwishoni mwa wiki kwa mchezo wa Ngao ya Jamii utakaozikutanisha timu za Chelsea na Arsenal zote kutoka jijini London. Mchezo huo ambao utachezwa Jumapili hii katika Uwanja wa Wembley huzikutanisha timu ambazo ni mabingwa katika Ligi Kuu pamoja na Kombe la FA. Chelsea wao ndio waliibuka mabingwa wa ligi msimu uliopita huku Arsenal wao wakifanikiwa kutetea taji lao la FA kwa mara ya pili na kuweka historia kuwa timu ya kwanza kunyakuwa taji hilo mara nyingi zaidi. Ligi rasmi inatarajiwa kuanza kutimua vumbi Agosti 8 mwaka huu kwa michezo nane ambapo Manchester United watakuwa wenyeji wa Tottenham Hotspurs katika Uwanja wa Old Trafford huku Bournemouth ambao wamepanda daraja msimu huu wao wakiikaribisha Ason Villa. Nyingine ni Norwich City watakaokuwa wenyeji wa Crystal Palace, Leicester City dhidi ya Sunderland, Everton dhidi ya Watford na mabingwa Chelsea dhidi ya Swansea City.

FENERBAHCE YAIKATIA RUFANI SHAKHTAR KWA KUMCHEZESHA FRED.

KLABU ya Fenerbahce imetuma malalamiko yake Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA baada ya Shakhtar Donetsk kumchezesha kiungo wa kimataifa wa Brazil Fred dhidi yao, pamoja na kukabiliwa na tuhuma za kutumia dawa za kusisimua misuli. UEFA imethibitisha kuwa inafanyia uchunguzi mchezo huo wa mkondo wa kwanza wa hatua ya tatu ya kufuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya uliochezwa Jumanne iliyopita na kumalizika kwa sare ya mabao 2-2. Taarifa kutoka nchini Brazil zinadai kuwa Fred mwenye umri wa miaka 22, alikutwa na chembechembe za dawa hizo zilizopigwa marufuku wakati alipofanyiwa vipimo katika michuano ya Copa America iliyomalizika hivi karibuni huko Chile. Kocha wa Shakhtar Mircea Lucescu amekiri UEFA walimshauri kutomchezesha Fred katika mchezo huo. Mchezaji huyo atakabiliwa na adhabu ya kufungiwa kama vipimo vya pili vitathibitisha kuwa alitumia dawa hizo.

CBF KUMUUNGA MKONO ZICO URAIS FIFA.

SHIRIKISHO la Soka la Brazil-CBF limetangza kumuunga mkono nguli wa soka wa nchi hiyo Zico (PICHANI) katika kinyang’anyiro cha urais wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA utakaofanyika Februari 26 mwakani. Rais wa CBF Marco Polo Del Nero amesema katika taarifa yake kuwa wanamuunga mkono Zico mwenye umri wa miaka 62 na kama atapata saini nne zinazohitajika hakuna shaka CBF watazipitisha. Ili Zico aweze kuwa mgombea rasmi wa kiti hicho anatakiwa aungwe mkono na mashirikisho ya soka kutoka nchi nne tofauti. Rais wa sasa Sepp Blatter alitangaza kuachia ngazi wadhifa wake huo Juni 2 mwaka huu ikiwa zimepita siku nne toka achaguliwe kuongoza kwa muhula wa tano kufuatia tuhuma za ufisadi zilizolikumba shirikisho hilo. Mbali na Zico wengine waliotangaza nia ya kuchukua nafasi hiyo ya Blatter, ni pamoja na rais wa Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA Michel Platini.

VAN DER VAART AITUHUMU MADRID KWA KUKOSA UVUMILIVU.

KIUNGO wa zamani wa Real Madrid, Rafael van der Vaart ameituhumu klabu yake hiyo ya zamani wa kukosa uvumilivu. Kiungo huyo wa kimataifa wa Uholanzi alivaa jezi ya Madrid kuanzia mwaka 2008 mpaka 2010 kabla ya kuondoka na kuhamia Tottenham Hotspurs na anadhani mategemeo makubwa waliyonayo hayaisaidii timu hiyo. Akihojiwa Van der Vaart amesema ukiwa Madrid kama hutashinda chochote lazima utaingia katika matatizo makubwa. Mkongwe huyo aliendelea kudai kuwa kwa maono yake anadhani Madrid hawana uvumilivu kwani ukipoteza mechi moja kwao ni kama duniani inakuwa imeishia hapo.

JIJI LA BEIJING LAPEWA SHAVU LA WINTER OLIMPIKI.

JIJI la Beijing limechaguliwa kuwa mwenyeji wa michuano ya Olimpiki na Paralimpiki ya majira ya baridi wakiushinda mji wa Almaty ulioko Kazakhstan. Wakiwa wenyeji wa michuano ya olimpiki mwaka 2008, Beijing ambao ndio mji kuu wa China sasa unakuwa mji wa kwanza kuandaa michuano yote miwili ya majira ya kiangazi na baridi. Miji ya Beijing na Almaty haikuwa ikipewa nafasi wakati kinyang’anyiro cha kugombea nafasi hiyo kilipoanza miaka miwili iliyopita. Lakini baada ya miji kadhaa ya Ulaya kujitoa kutokana na sababu za kisiasa au kiuchumi, Beijing ilifanikiwa kuibuka kidedea kwa kuzoa kura 44 dhidi ya kura 40 za Almaty.

GUARDIOLA MGUU NDANI MGUU NJE BAYERN.

MENEJA wa Bayern Munich, Pep Guardiola amesema hatasaini mkataba mpya na klabu hiyo mpaka atakapojiridhisha kuwa ni jambo la busara kwa pande zote mbili. Kumekuwa na tetesi zilizoibuka juu ya mustakabali wa kocha huyo ambaye mkataba wake unamalizika mwakani huku taarifa zingine zikidai tayari ameshakubali kuhamia Manchester City. Guardiola mwenye umri wa miaka 44, hajathibitisha mipango yake lakini amekiri kuwa hana uhakika kama ataendelea kuwepo Allianz Arena. Akizungumza na wanahabari, Guardiola amesema kwasasa yeye ni kocha wa Bayern na anafurahia hilo lakini bado hajaamua kuhusu mustakabali wake na pindi atakapopata uamuzi atawaarifu Kalle Rummenigge ambaye ni rais, Mathias Sammer mkurugenzi wa michezo na Uli Hoeness ambaye ni rais wa zamani wa klabu hiyo.

Monday, July 27, 2015

HABARI PICHA: GOLIKIPA WA ARSENAL WOLCIECH SZCZESNY AMKIMBIA PETR CECH NA KUTIMKIA ROMA.

Golikipa wa Arsenal, Wojciech Szczesny akiwa katika uwanja wa ndege jijini Roma tayari kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya afya kabla ya kujiunga kwa mikopo na AS Roma.



HABARI PICHA; ALEXIS SANCHEZ AANZA KUJIFUA PEKE YAKE UFUKWENI.






WALCOTT NJIANI KUSAINI MKATABA MPYA ARSENAL.

MSHAMBULIAJI wa Arsenal, Theo Walcott anakaribia kuongeza mkataba wake na klabu hiyo hadi mwaka wa 2019. Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger amefichua kuwa Walcott atasaini mkataba mpya na timu hiyo huku ule wake wa awali ukiwa umebaki mwaka mmoja. Walcott mwenye umri wa miaka 26 aliifungia Arsenal goli la kipekee dhidi ya Wolfsburg ya Ujerumani na kuiwezesha timu hiyo kunyakuwa Kombe la Emirates jana. Aidha, kipa wa Poland, Scszesny yuko mjini Roma, Italia akimalizia taratibu za mwisho za kujiunga na klabu ya AS Roma baada ya kupoteza nafasi yake kwa aliyekuwa kipa wa Chelsea, Petr Cech. Scszesny kwasasa anasubiri vipimo vya afya kabla ya kujiunga na timu hiyo kwa mkopo. Wenger, amekuwa chini ya shinikizo kali kuimarisha kikosi chake ili kuleta ushindani katika Ligi Kuu na Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.

VAN GAAL KUONDOKA UNITED KWA AJILI MKEWE.

MENEJA wa Manchester United, Louis van Gaal pengine akaondoka klabuni hapo mwishoni mwa mkataba wake wa miaka mitatu ili kutimiza ahadi aliyompa mkewe. Akiulizwa kuhusu kuongeza mkataba Old Trafford, Van Gaal raia wa Uholanzi alidai kuwa ameamua kuondoka pindi atakapomaliza mkataba wake. Kocha huyo mwenye umri wa miaka 63, amesema sababu inayoweza kumfanya aondoke ni ahadi aliyompa mkewe kwakuwa hawajapa muda wa kutosha kukaa pamoja. Van Gaal amesema alimuahidi mkewe Truus kuwa atakapofikisha umri wa miaka 55 atastaafu lakini mpaka sasa bado anafanya kazi na wiki ijayo anatimiza umri wa miaka 64. Van Gaal aliendelea kudai kuwa ndoto yake kubwa ilikuwa kufundisha katika Ligi Kuu pia hivyo haoni sababu ya kuendelea pindi atakapomaliza mkataba wake.

AL-ITTIHAD KUWAKUTANISHA WATUKUTU WA GHANA, MUNTARI NA BOATENG.

KLABU kongwe ya Al-Ittihad ya Saudi Arabia inaweza kuwakutanisha nyota wa zamani wa AC Milan ya Italia Sulley Muntari na Kevin-Prince Boateng katika timu hiyo. Wawili hao ambao walisimamishwa kuitumikia timu ya taifa ya Ghana kutokana na sababu tofauti za utovu wa nidhamu wakati wa michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2014, walikuwa kwa pamoja wakiitumikia Milan mismu mitatu iliyopita kabla ya Boateng hajahamia Schalke ya ujerumani. Muntari na Boateng ambao wanajulikana kwa urafiki wao, kwasasa wako sokoni katika kipindi hiki cha usajili wa kiangazi. Muntari mwenye umri wa miaka 30, ni mchezaji huru baada ya kusitisha mkataba wake na Milan na tayari inaripotiwa kuwa ameshakubali kusaini mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya euro milioni 2.5 kila mwaka na Ittihad. Klabu hiyo pia imeripotiwa kumuwinda Boateng baada ya kushindwa kumsajili kiungo Fredy Guarin kutoka Inter Milan.

LUIZ AMPIGIA DEBE DI MARIA KWENDA PSG.

KIUNGO wa Paris Saint-Germain-PSG, David Luiz ana matumaini ya kusajiliwa kwa Angel Di Maria, kwani anaamini ujio wake utawafanya kuwa wapinzani wa kweli katika kugombea taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya. Inadaiwa kuwa kiungo huo mwenye umri wa miaka 27 anakaribia kufanya uhamisho wake kutoka Manchester United kwenda PSG baada ya kushindwa kujiunga na kikosi cha United katika ziara yao nchini Marekani huku meneja wa PSG Laurent Blanc akikiri kuwepo kwa uwezekano huo. Di Maria amekuwa akihangaika kucheza kwa kiwango chake toka asajiliwe kwa kitita kilichovunja rekodi nchini Uingereza cha paundi milioni 59.7 na United mwaka jana. Lakini Luiz ana uhakika kuwa Di Maria bado ni mchezaji mwenye ubora ambaye anaweza kuisaidia PSG kutawala soka la Ulaya kama akisajiliwa. Luiz amesema wanataka kushinda taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya na Di Maria ni mchezaji anayeweza kuwasaidia kuvuka hatua nyingine.

MEXICO YAWEKA REKODI KWA KUNYAKUWA TAJI LA GOLD CUP KWA MARA YA SABA.

TIMU ya taifa ya Mexico imefanikiwa kuweka rekodi kwa kunyakuwa Kombe la Gold kwa mara ya saba baada ya kuichapa Jamaica walioingia kwa mara ya kwanza katika fainali ya michuano hiyo. Jamaica imekuwa nchi ya kwanza kutoka ukanda wa Caribbean kutwaa taji hilo lakini walishindwa kufurukuta mbele ya Mexico ambao hilo ni tatu lao la tatu katika fainali nne zilizopita za michuano hiyo. Katika mchezo huo Mexico walifanikiwa kushinda mabao 3-1 mbele ya mashabiki 70,000 waliojitokeza katika Uwanja wa Philadelphia Lincoln ambayo yalifungwa na Andres Guardado, Jesus Corona na Oribe peralta huku lile la kufutia machozi kwa upande wa Jamaica likifungwa na Darren Mattocks. Akihojiwa mara baada ya fainali ya michuano hiyo ambayop hushirikisha nchi za ukanda wa Amerika Kaskazini, Kati na Caribbean-Concacaf, Kocha wa Mexico Miguel Herrera amesema hiyo ni siku ya kipekee kwao. Mexico sasa wamefuzu kwa ajili ya hatua ya mtoano dhidi ya mabingwa wa mwaka 2013 Marekani mchezo ambao utachezwa Octoba 9 mwaka huu katika kutafuta nafasi ya kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho nchini Urusi mwaka 2017.

ASTON VILLA YAKARIBIA KUMNASA CRESPO.

KLABU ya Cordoba imebanisha kuwa beki Jose Angel Crespo anatarajiwa kufanyiwa vipimo vya afya Aston Villa baada ya klabu hizo mbili kufikia makubaliano kuhusu ada ya uhamisho wake. Beki huyo mwenye umri wa miaka 28 msimu uliopita alikuwa akicheza kwa mkopo katika klabu ya Andalusian. Cordoba ambayo ilishuka daraja msimu uliopita baada ya kumaliza wa mwisho katika msimamo wa La Liga, wamedai leo kuwa Crespo anakaribia kukamilisha uhamisho wake kwenda Villa Park. Taarifa hizo zilithibitishwa katika mtandao wa klabu hiyo na kudai kuwa tayari beki huyo amesafiri kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya vipimo vya afya.

VAN GAAL ADOKEZA ROMERO ANAWEZA KUWA MBADALA WA DE GEA.

MENEJA wa Manchester United, Louis van Gaal amedokeza kuwa wamemsajili golikipa Sergio Romero (pichani) ili kujiandaa na uwezekano wa kuondoka kwa David de Gea katika kipindi hiki cha majira ya kiangazi. Romero alikamilisha uhamisho wake kutua Old Trafford baada ya kukubali kusaini mkataba wa miaka mitatu huku akiwa na nafasi ya kuongezwa mwingine. De Gea amekuwa akihusishwa na tetesi za kuhamia Real Madrid baada ya kuondoka kwa Iker Casillas. Kufuatia Victor Valdes kujiandaa kuondoka baada ya kukataa kucheza katika kikosi cha vijana chini ya umri wa miaka 21 msimu uliopita, Van Gaal ana Romero atakuwa chaguo sahihi hata kama De Gea naye ataamua kuondoka United. Akihojiwa Van Gaal amesema hajui kama De Gea ataondoka au atabakia hivyo ni vyema kwao kujiandaa na lolote na anadhani Romero atakuwa chaguo sahihi.

Thursday, July 23, 2015

BAYERN YATHIBITISHA ARTURO VIDAL ALMOST A DONE DEAL.

KLABU ya Bayern Munich, imethibitisha kuwa kiungo Arturo Vidal atajiunga na timu hiyo akitokea Juventus kwani sasa kilichobakia ni kufanyiwa vipimo vya afya na kusaini mkataba wake. Mabingwa hao wa Ujerumani walikubali kutoa ada ya euro milioni 40 iliyotakiwa na Juventus kwa ajili ya nyota huyo wa kimataifa wa Chile, Alhamisi iliyopita. Baadae ofisa mkuu wa Bayern Karl-Heinz Rummenigge alifafanua kuwa uhamisho huo unatarajiwa kukamilika baada ya vilabu vyote na mchezaji kukubaliana masuala ya fedha. Lakini taarifa zilizotoka leo zimedai kuwa kwasasa kila kitu kiko sawa na Vidal mwenyewe ameshafikia makubaliano binafsi ya mambo ya kifedha na kilichobakia sasa na vipimo vya afya na kusaini mkataba wenyewe. Vidal anayecheza nafasi ya kiungo wa kati anachukuliwa na wengi kama mbadala wa Bastian Schweinsteiger ambaye aliondoka Allianz Arena na kwenda Manchester United mapema mwezi huu.

BARCELONA YAKANUSHA KUPOKEA OFA KWA AJILI YA PEDRO.

RAIS wa Barcelona Josep Maria Bartomeu amekanusha klabu hiyo kupokea ofa yeyote kwa ajili ya Pedro ambaye amekuwa akihusishwa na tetesi za kuhamia Ligi Kuu ya Uingereza kipindi hiki cha kiangazi. Chelsea, Manchester United na Arsenal zote zinaaminika kumuwinda nyota huyo wa kimataifa wa Hispania mwenye umri wa miaka 27. Kiungo wa Barcelona Sergio Busquets amekiri mchezaji mwenzake huyo katika klabu na timu ya taifa ana mashaka ya kubakia katika timu hiyo kutokana na kutokuwa na uhakika na nafasi yake katika kikosi cha kwanza. Hata hivyo, Bartomeu ambaye amechaguliwa tena mwishoni mwa wikiendi iliyopita kuingoza Barcelona kwa kipind cha miaka sita ijayo, amesema klabu haijapokea ofa kwa ajili ya mchezaji yeyote mpaka sasa. Bartomeu aliendelea kudai kuwa meneja wa klabu Luis Enrique alishweka wazi kuwa timu yeyote inayohitaji mchezaji kutoka Barcelona ni lazima wafikie dau lililowekwa katika mikataba yao.

ATLETICO YANASA SAINI YA NYOTA WA GHANA.

KLABU ya Atletico Madrid imekubali kumsajili kiungo wa kimataifa wa Ghana Bernard Mensah kutoka klabu ya Vitoria Guimaraes ya Ureno. Hata hivyo, Atletico watampeleka kiungo huyo kwa mahasimu wao wa La Liga na majirani zao Getafe. Klabu hiyo ilithibitisha tarifa hizo kupitia mtandao wake jana huku wakidai kumpeleka kwa mkopo wa msimu mmoja Getafe. Vitoria na Getafe pia zilithibitisha dili hilo la nyota huyo mwenye umri wa miaka 20 ambaye ambali na kucheza kama kiungo wa kushambulia lakini pia anaweza kucheza kama winga.

BENTEKE TO LIVERPOOL DONE DEAL.

LIVERPOOL imefanikiwa kumsajili rasmi mshambuliaji wa Aston Villa, Christian Benteke kwa kitita cha paundi milioni 32.5. Benteke anakuwa mchezaji wa pili ghali kusajiliwa na Liverpool. Liverpool ambao wiki iliyopita walimuuza mshambuliaji Raheem Sterling kwenda Manchester City kwa kitita cha paundi milioni 49, walifanikiwa kunasa saini ya Benteke na kumfanya kuwa mchezaji wa saba kusajiliwa na timu hiyo kipindi hiki cha kiangazi. Nyota huyo wa kimataifa wa Ubelgiji amefunga mabao 49 katika mechi 101 alizoichezea Villa baada ya kumsajiliwa kutoka Genk kwa kitita cha paundi milioni saba mwaka 2012. Akihojiwa mara baada ya kukamilisha usajili huo Benteke alieleza kufurahishwa kwake na hatua hiyo na kuahidi kufanya kila awezalo kuhakikisha mataji yanamiminika Anfield.

MOURINHO AMKINGIA KIFUA GOLIKIPA WAKE GARASA ALIYEMCHUKUA KUTOKA STOKE.

MENEJA wa Chelsea, Jose Mourinho amemkingia kifua golikipa mpya Asmir Begovic baada ya nyota huyo wa kimataifa wa Bosnia kuruhusu mabao manne katika mchezo dhidi ya New York Redbull kufuatia kuingia kwake wakati wa mapumziko katika mchezo huo wa kirafiki uliochezwa jana. Begovic alisajiliwa akitokea Stoke City mwezi huu kwa akitita cha paundi milioni nane ili aweze kuleta changamoto kwa golikipa namba moja Thibaut Courtois. Katika mchezo huo Begovic alibadilishana na na Courtois Chelsea wakiwa wanaongoza kwa bao 1-0 lakini mambo yalibadilika na kujikuta wakichapwa mabao 4-2. Akihojiwa Mourinho amesema Begovic alikuwa amechoka kama ilivyokuwa kwa Courtois na golikipa akichoka siku zote huwa kunakosekana kwa uelewano. Mourinho aliendelea kudai kuwa Courtois alifanya makosa katika kipindi cha kwanza na Begovic naye alifanya makosa katika kipindi cha pili kwa kukosa kasi katika matukio jambo ambalo ni matokeo ya uchovu unaotokana na mazoezi makali.

HOFU YAMUINGIA WENGER AKIWAZA KUSTAAFU.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema mawazo ya kustaafu humfanya kuingiwa na hofu. Meneja huyo raia wa Ufaransa mwenye umri wa miaka 65, anatarajiwa kutimiza miaka 20 akiwa na Arsenal lakini amesema hana mpango wowote wa kufuata nyayo za meneja wa zamani wa Manchester United Sir Alex Ferguson aliyestaafu. Akihojiwa kuhusiana na hilo, Wenger amesema huwa analiwaza kwa muda usiozidi sekunde tano kwasababu humfanya apate hofu kidogo. Wenger aliendelea kudai kuwa wakati walipocheza na United alikutana na Ferguson na kumuuliza kama haoni kama kuna kitu anakikosa lakini alimjibu kuwa alishafanya ikamtosha kabisa. Wenger ambaye ameiongoza Arsenal kutetea taji lake la FA msimu uliopita, aliongeza kuwa pamoja na hayo lakini ni mara chache sana kumkosa Ferguson uwanjani. Wenger alijiunga na Arsenal akitokea Monaco mwaka 1996.

BAYERN YAIAMBIA UNITED ILIE TU KWA MULLER.

OFISA mkuu wa Bayern Munich, Karl-Heinz Rummenigge amewaonya Manchester United kuwa hakunja fedha zitakazotosha kwa ajili ya wao kumsajili Thomas Muller. United iliyo chini Louis van Gaal tayari imeshamsajili Bastian Schweinsteiger kutoka kwa mabingwa hao wa Bundesliga mapema mwezi huu na tetesi ziliibuka kuwa wako tayari tena kutoa ofa ya euro milioni 100 kwa ajili ya Muller. Akihojiwa na wanahabari katika ziara yao nchini China, Rummenigge amesema kuna wachezaji hawauziki kwa gharama yeyote na mmojawapo nia Muller. Rummenigge aliendelea kudai kuwa hawajawahi kupokea simu yeyote kutoka United na hakuna ofa iliyotolewa na yeyote kwa ajili ya mchezaji huyo.

BENITEZ ASISITIZA RAMOS HANG'OKI NG'O.

MENEJA mpya wa Real Madrid, Rafael Benitez amesema beki Sergio Ramos ana asilimia 100 za kubakia katika klabu hiyo kufuatia tetesi kuwa nyota huyo wa kimataifa wa Hispania anaweza kwenda Manchester United. Meneja wa United, Louis van Gaal alidokeza mapema wiki hii kuwa anaweza kumuwania Ramos mwenye umri wa miaka 29 ambaye amebakisha miaka miwili katika mkataba wake Madrid lakini anaweza kukwamishwa na kiwango chake cha mshahara. Pia baadae zikazuka tetesi zingine kuwa Ramos anaweza kujiunga na United kama sehemu ya mpango wa kubadilishana na golikipa David De Gea mwenye umri wa miaka 24. Hatahivyo, Benitez akizungumza na wanahabari mapema leo huko Melbourne, Australia amesema De Gea sio mchezaji wao na Ramos ni nahodha wao na mchezaji muhimu kwao. Benitez amesema anataka Ramos abakie hapo na iko wazi kwake na kwa klabu kuwa atendelea kuwepo hapo msimu ujao. Madrid wanajiandaa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Manchester City unaotarajiwa kuchezwa kesho ikiwa ni sehemu ya mandalizi ya timu hizo kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi zao.

Tuesday, July 21, 2015

VPL KUANZA SEPTEMBA 12.

LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania (VPL) itaanza Sept 12 badala ya Agosti 22 ili kumpa Charles Mkwasa fursa ya kuendelea na program yake kuelekea mechi ya Taifa Stars vs Nigeria itakayochezwa Sept 5. Mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) itakayozikutanisha Azam FC dhidi ya Yanga SC sasa itachezwa Agosti 22 badala ya Agosti 15. Ratiba ya Ligi Kuu iliyokuwa imeandaliwa, sasa inafanyiwa marekebisho kwa ajili ya tarehe mpya ya kuanza, ambapo pamoja na mambo mengine mechi sasa zitachezwa wikiendi na katikati ya wiki na wikiendi ya Oct 25 hakutakuwa na mechi kupisha Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge. Klabu za Ligi Kuu zimeandikiwa barua kujulishwa tarehe mpya ya kuanza Ligi, na dirisha la usajili linabaki kama lilivyo. Wamiliki wa viwanja vyenye upungufu wmeandikiwa barua kutakiwa kurekebisha upungufu katika muda maalumu, vinginevyo havitaruhusiwa kutumika kwa ajili ya PL na FDL. Timu ya Madini ya Arusha imeruhusiwa kutumia Uwanja wa Nyerere uliopo Mbulu mkoani Manyara kwa mechi za SDL kwa masharti upungufu uliopo kwenye uwanja huo urekebishwe kwanza.

HABARI PICHA: ARTURO VIDAL AKIPASHA NA KOCHA WA CHILE JORGE SAMPAOLI WAKATI AKIFURAHIA MAPUMZIKO YAKE HUKO MIAMI.




HABARI PICHA: MAZISHI YA DEREVA NYOTA WA LANGALANGA JULES BIANCHI.

Mamia ya waombolezaji wakiwa mbele ya jeneza la dereva wa langalanga Jules Bianchi aliyefariki miezi tisa baada ya majeraha ya kichwa aliyopata katika ajali kwenye mbio za Japan Grand Prix, Octoba mwaka jana.



GERRARD NA SUAREZ WAKUTANA MAREKANI.

Steven Gerrard akiwa katika picha ya pamoja na nyota wa mpira wa kikapu NBA Kobe Bryant.

Gerrard akiwa katika picha na rafiki yake Luis Suarez.



STERLING APIGA BAO MECHI YAKE YA KWANZA AKIWA NA CITY.

MSHAMBULIAJI mpya wa Manchester City, Raheem Sterling amefanikiwa kufunga bao dakika tatu katika mchezo wake wa kwanza wa kirafiki dhidi ya AS Roma uliochezwa katika Uwanja wa MCG jijini Melbourne leo. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 20, amejiunga na City kwa kitita cha paundi milioni 49 kutoka Liverpool Julai 14 mwaka huu. Sterling alikuwa akicheza akitokea upande wa kushoto sambamba na washambuliaji wengine wawili akiwemo David Silva na chipukizi Kelechi Iheanacho, kabla ya kutolewa katika muda wa mapumziko. Iheanacho pia alifunga bao katika mchezo huo ambao City walishinda kwa changamoto ya mikwaju ya penati 5-4 baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 katika muda wa kawaida. Mchezo huo ni wa kwanza kwa City katika michuano ya Kimataifa ya Kirafiki ambapo sasa watachuana Real Madrid Ijumaa hii.

VAN GAAL KUMTUMIA ROONEY KAMA MSHAMBULIAJI MSIMU UJAO.

MENEJA wa Manchester United, Louis van Gaal amesema amepanga kumtumia Wayne Rooney kama mshambuliaji wa kati msimu ujao. Rooney mwenye umri wa miaka 29, amekuwa akitumika katika nafasi ya kiungo katika kipindi kirefumsimu uliopita. Akizungumza na wanahabari, Van Gaal amesema amekuwa akisikiliza maoni yao kwani wamekuwa wanaufahamu zaidi yake hivyo atamtumia Rooney katika nafasi ya ushambuliaji zaidi msimu ujao. Mara ya mwisho Rooney kucheza kama mshambuliaji msimu wa 2011-2012, alifanikiwa kufunga mabao 34 na ana matumaini msimu ujao ataweza tena kufanya hivyo. Akihojiwa Rooney amesema ana matumaini ya kufunga mabao 20 au zaidi na kama akishindwa kufanya hivyo ni jambo ambalo litamhuzunisha.

PELE ARUHUSIWA KUTOKA HOSPITALI.

NGULI wa soka wa Brazil, Pele ameruhusiwa kutoka hospitali baada ya kufanyiwa upasuaji wa mgongo uliofanikiwa. Nguli huyo mwenye umri wa miaka 74 alikuwa akisumbuliwa na maumivu makali ya mgongo na lifanyiwa upasuaji huo katika hospitalia ya Albert Einstein iliyopo jijini Sao Paulo. Pele ambaye amewahi kushinda taji la Kombe la Dunia mara tatu akiwa na Brazil, amewahi kutibiwa maambukizi katika njia ya mkojo miezi nane iiyopita baada ya kuondolewa mawe katika figo. Pele amefanikiwa kucheza mechi 14 katika Kombe la Dunia akifunga mabao 12 na alitunukia tuzo mpira wa dhahabu kama mchezaji bora wa mashindano mwaka 1970.

Saturday, July 18, 2015

EID MUBARAK.

Uongozi wa Beki3 unawatakia waislamu wote popote ulimwenguni heri ya sikukuu ya Eid.

SCHNEIDERLING APIGA BAO PEKEE KATIKA USHINDI MWEMBAMBA WA UNITED HUKO MAREKANI.

KIUNGO mpya wa Manchester United, Morgan Schneiderling amefunga bao lake la kwanza akiwa mchezaji wa timu hiyo katika ushindi wa bao 1-0 walioupata dhidi ya Club America katika mchezo wa kirafiki uliofanyika huko Marekani jana. Nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa, ambaye alikamilisha usajili wake uliogharimu kitita cha dola milioni 39 kutoka Southampton mapema mwezi huu alifunga bao hilo kwa kichwa katika dakika ya tano ya mchezo. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo, meneja wa United Louis van Gaal amesema wachezaji wote walicheza kama alivyowaelekeza katika kipindi chote cha mchezo hivyo anafurahi kwamba wameibuka washindi. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa jambo lingine lililomfurahisha ni safu yake ya ulinzi kutoruhusu bao kwani hiyo ilikuwa sehemu ya malengo yao.


MCHEZAJI WA ZAMANI WA ARSENAL ALIMWA KADI BAADA YA KUWAJIBU WALIOMFANYIA VITENDO VYA KIBAGUZI.

MCHEZAJI wa zamani wa Arsenal, Emmanuel Frimpong alijikuta akitolewa nje akiwa na timu yake ya FC Ufa ya Urusi baada ya kuonyesha ishara ya tusi akijibu mashabiki waliokuwa wakimpigia kelele za nyani. Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 23, alikuwa kicheza ugenini dhidi ya Spartak Moscow katika mchezo wa ufunguzi wa Ligi Kuu ya nchi hiyo. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo ambao ulimalizika kwa sare ya mabao 2-2, nyota huyo wa kimataifa wa Ghana amesema wakati mchezo uliposimama mashabiki walianza kumpigia kelele za nyani. Frimpong aliendelea kudai kuwa alishindwa kuzua jazba zake na kuonyesha hisia zake na hilo ndilo kosa lilofanya. Frimpong alionyeshwa kadi nyekundu baada ya nusu ya mchezo huo wakati ambapo timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1.

DELPH ASAINI MIAKA MITANO CITY.

NAHODHA wa Aston Villa Fabian Delph amesaini mkataba wa miaka mitano katika klabu ya Manchester City ikiwa imepita wiki moja baada ya kudai atabakia Villa Park. Kiungo huyo wa kimataifa wa Uingereza, uhamisho wake kwenda City umekuja baada ya kueleza msimamo wake kuhusu mustakabali wake. Akihojiwa meneja wa City, Manuel Pellegrini amesema Delph ambaye ana umri wa miaka 25 bado ana miaka mingi ya kucheza soka kwa kiwango cha juu hivyo ana hamu kubwa ya kufanya naye kazi. Delph alikamilisha vipimo vya afya jana na anatarajiwa kusafiri leo kuelekea nchini Australia kujiunga na wachezaji wenzake kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu. Nyota huyo amepewa jezi namba nane ambayo ilikuwa ikitumiwa na Frank Lampard msimu uliopita ambaye kwasasa yuko katika klabu ya New York City FC ya Marekani.

GERRARD ATUPIA KATIKA GEMU LAKE LA KWANZA MLS.

NAHODHA wa zamani wa kimataifa wa Uingereza na klabu ya Liverpool, Steven Gerrard amefanikiwa kufunga bao lake la kwanza katika Ligi Kuu nchini Marekani huku akisaidia mengine mawili kati ya matatu yaliyofungwa na Robbie Keane wakati Los Angeles Galaxy ikiibatua San Jose Earthquakes. Mkongwe huyo mwenye umri wa miaka 35, alifunga bao lake hilo katika dakika ya 37 ya mchezo katika ushindi wa mabao 5-2 walioupata. Huo ndio ulikuwa mchezo wa kwanza wa kimashindano aliocheza Gerrard katika timu hiyo toka ajiunge nao mapema mwezi huu akitokea Liverpool. Sasa anakuwa mchezaji wa tatu kufunga bao, kusaidia moja na kusababisha penati katika ligi hiyo msimu huu, huku wengine wakiwa nyota wa zamani wa Serie A Sebastian Gionvico na Kaka.

JUVENTUS WARUDIA KWA FERUFI KUBWA KUWA POGBA HAUZWI.

KLABU ya Juventus imeongeza msisitiza kiungo wake Paul Pogba hatauzwa, pamoja na kutolewa kwa ofa na klabu ya Barcelona. Joan Laporta amedai kuwa ataweza kumsajili nyota huyo mwenye umri wa miaka 22, ambaye pia amehusishwa na tetesi za kutakiw Manchester City na Chelsea, kama akichaguliwa kuwa rais wa Barcelona tena. Mkuruzenzi wa Juventus Giuseppe Marotta amesema yeyote anayamtaka mchezaji huyo anapswa kuzungumza nao na sio kwenda kwa wakala wake Mino Raiola. Marotta aliendelea kudai kuwa kwasasa Barcelona hawazi kufanya usajili wowote na Juventus hawana mpango wa kumuuza Pogba. Nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa ambaye amewahi kuwa mchezaji wa Manchester United, ana mkataba na Juventus ambao unamalizika Juni mwaka 2019.

MAN UNITED YAIBANA MADRID, YAWAAMBIA BILA RAMOS HAWAMPATI DE GEA.

KLABU ya Manchester United wanajiandaa kupoteza zaidi ya paundi milioni 25 na kumuacha golikipa wao David De Gea kuondoka kama mchezaji huru majira ya kiangazi mwakani kuliko kuwauzia Real Madrid. Golikipa huyo mwenye umri wa miaka 24, atauzwa pale tu Madrid watakapokubali kumuachia beki wao Sergio Ramos mwenye umri wa miaka 29 kwenda United. De Gea ambaye amekuwa katika mipango ya Madrid kipindi hiki cha kiangazi, amebakisha mkataba wa mwaka mmoja na anataka kurejea nyumbani. Lakini United wameamua kukomaa na golikipa huyo hata kama ataodoka bure mwakani ili waweze kutoa msukumo kwa Madrid kumuachia Ramos.