Friday, July 31, 2015

CBF KUMUUNGA MKONO ZICO URAIS FIFA.

SHIRIKISHO la Soka la Brazil-CBF limetangza kumuunga mkono nguli wa soka wa nchi hiyo Zico (PICHANI) katika kinyang’anyiro cha urais wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA utakaofanyika Februari 26 mwakani. Rais wa CBF Marco Polo Del Nero amesema katika taarifa yake kuwa wanamuunga mkono Zico mwenye umri wa miaka 62 na kama atapata saini nne zinazohitajika hakuna shaka CBF watazipitisha. Ili Zico aweze kuwa mgombea rasmi wa kiti hicho anatakiwa aungwe mkono na mashirikisho ya soka kutoka nchi nne tofauti. Rais wa sasa Sepp Blatter alitangaza kuachia ngazi wadhifa wake huo Juni 2 mwaka huu ikiwa zimepita siku nne toka achaguliwe kuongoza kwa muhula wa tano kufuatia tuhuma za ufisadi zilizolikumba shirikisho hilo. Mbali na Zico wengine waliotangaza nia ya kuchukua nafasi hiyo ya Blatter, ni pamoja na rais wa Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA Michel Platini.

No comments:

Post a Comment