Tuesday, September 30, 2014

NTAONDOKA CHELSEA NIKIFUKUZWA - MOURINHO.

MENEJA wa klabu ya Chelsea, Jose Mourinho amesisitiza kuwa ataondoka katika timu hiyo endapo kama atatimuliwa. Mara ya kwanza Mourinho kuondoka Stamford Bridge ilikuwa Septemba mwaka 2007 baada ya kushindwa kuelewana na mmiliki wa klabu hiyo Roman Abramovic. Kocha huyo raia wa Ureno aliondoka na kwenda kupata mafanmikio nchini Italia na Hispania akiwa na Inter Milan na Real M,adrid lakini aliwashangaza wengi kwa kurejea tena Chelsea katika kipindi cha kiangazi mwaka jana kufuatia kuondoka kwa Rafa Benitez. Katika kipindi hicho ilikuwa imeripotiwa kuwa Mourinho atarejea nchini Uingereza kuchukua nafasi ya Sir Alex Ferguson kama meneja wa Manchester United lakini kocha huyo badala yake akamchukua David Moyes kushika nafasi yake. Mourinho amesema ana mpango wa kukaa muda mrefu Chelsea lakini kama itatokea kutimuliwa anaweza kufikiria kutafuta timu nyingine ya Ligi Kuu.

26 WAITWA TAIFA STARS KUIVAA BENIN.

WACHEZAJI 26 wameitwa kwenye kikosi cha timu ya Taifa Tanzania,Taifa Stars kwa ajili mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Benin itakayochezwa Oktoba 12 mwaka huu jijini Dar es Salaam. Kocha wa Stars Mart Nooij ambaye yuko jijini Cairo, Misri kwenye kongamano la makocha la Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika-CAF, amesema kikosi cha Taifa Stars kitaingia kambini Oktoba 6 mwaka huu jijini Dar es Salaam. Wachezaji walioitwa na vilabu wanavyotoka ni makipa Deogratias Munishi,(Yanga), Aishi Manula na Mwadini Ali wote Azam. Mabeki ni Said Moradi, Azam, Shomari Kapombe (Azam), Oscar Joshua (Yanga), Nadir Haroub (Yanga), Kelvin Yondani (Yanga), Aggrey Morris (Azam), Miraji Adam (Simba), Charles Edward (Yanga) na Emmanuel Simwanda (African Lyon). Viungo ni Erasto Nyoni (Azam), Mwinyi Kazimoto (Al Markhiya, Qatar), Amri Kiemba (Simba), Himid Mao (Azam), Salum Abubakar (Azam), Said Ndemla (Simba) na Haruna Chanongo (Simba). Washambuliaji ni Khamis Mcha (Azam), Simon Msuva (Yanga), Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, DR Congo), Mbwana Samata (TP Mazembe, DR Congo), Mrisho Ngasa (Yanga), Mwegane Yeya (Mbeya City), na Juma Liuzio (Zesco, Zambia).


Monday, September 29, 2014

CHAMPIONS LEAGUE ROUNDUP.

MICHUANO ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya hatua ya makundi inatarajiwa kuendelea tena kesho na keshokutwa ambapo viwanja mbalimbali vinatarajiwa kuwaka moto. Katika michezo ya kesho macho yatakuwa yameelekezwa kwa matajiri na mabingwa wa soka nchini Uingereza Manchester City ambao watakuwa wenyeji wa AS Roma ya Italia katika mchezo wa kundi E utakaofanyika katika Uwanja wa Etihad. City wataingia katika mchezo wakihitaji ushindi baada ya kupoteza mchezo wao kwanza waliochezwa na mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich ambao walifungwa bao 1-0 huko Allianz Arena. Katika mchezo mwingine wa kundi hilo CSKA Moscow ya Urusi watakuwa nyumbani kujiuliza mbele ya Bayern baada ya kuchabangwa mabao 5-1 na Roma katika mchezo wao uliopita. Kwa upande wa Kundi F matajiri wa Ufaransa, Paris Saint-Germain,PSG watakuwa wenyeji wa Barcelona wakitafuta alama tatu muhimu baada ya kutoka sare ya bao 1-1 na Ajax Amsterdam ya Uholanzi. Barcelona wao walipata ushindi mwembamba wa bao 1-0 katika mchezo dhidi ya APOEL Nicosia ya Cyprus ambao kesho watakuwa wenyeji wa Ajax katika mchezo mwingine wa kundi hilo. Katika mechi zao za kwanza Barcelona ambao ndio wanaongoza kundi hilo walipata ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya timu ya APOEL Nicosia ya Cyprus huku PSG wao wakitoa sare ya bao 1-1 dhidi ya Ajax Amsterdam ya Uholanzi. Mchezo mwingine utakaovuta hisia za mashabiki hapo kesho ni wa kundi G ambao utawakutanisha vinara wa Ligi Kuu Chelsea wakaokuwa wageni wa Sporting Lisbon ya Ureno huku Schalke ya Ujerumani wakiwa wenyeji wa NK Maribor ya Slovenia timu zote katika kundi hili zilitoka sare ya bao 1-1 katika mechi zao za kwanza. Kesho pia kutakuwa na michezo itakayochezwa katika kundi H ambapo BATE Borislov ya Belarus watawakariisha Athletic Bilbao ya Hispania na Shakhtar Donetsk ya Ukraine wakiwa wenyeji wa FC Porto ya Ureno.

Barcelona vs Granada 6-0 2014-NEYMAR Hat-Trick

KAMA ULI-MISS FAULO YA KIJINGA ALIYOCHEZA ROONEY.

ROONEY AOMBA RADHI KWA KADI NYEKUNDU ALIYOPEWA.

MSHAMBULIAJI nyota wa klabu ya Manchester United, Wayne Rooney amewaomba radhi wachezaji wenzake kwa kadi nyekundu aliyopewa katika mchezo dhidi ya West Ham United uliochezwa Jumamosi iliyopita. Nahodha huyo wa United alitolewa baada kumkwatua kwa makusudi mchezaji wa West Ham Stewart Downing na amedai kuwa hatakata rufani kupinga uamuzi wa mwamuzi Lee Mason aliyechezesha mchezo huo. Akihojiwa Rooney amesema alifanya mahesabu yake vibaya kwani alidhani mchezaji huyo anaweza kuleta madhara katika lango lao lakini haikuwa hivyo ndio maana anaomba radhi. Katika mchezo huo United ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 pamoja na kucheza wakiwa pungufu kwa muda wa dakika 30. Rooney sasa hataitumikia United ka michezo mitatu mpaka Novemba 2 mwaka huu wakati watakapokwaana na mahasimu wao Manchester City. 


Friday, September 26, 2014

SIMBA, YANGA SASA KUKIPIGA OCTOBA 18.

MCHEZO wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaowakutanisha watani wa jadi Yanga na Simba umesogezwa mbele mpaka Octoba 18 mwaka huu kutokana na ratiba ya ligi kufanyiwa marekebisho. Ratiba hiyo ambayo hapo awali ilielekeza mchezo huo kuchezwa Octoba 12 sasa imesogezwa mbele ili kupisha ratiba ya mechi za kimataifa ambayo iko katika kalenda ya Shirikisho la Soka Duniani-FIFA. Badala ya mchezo huo sasa timu ya taifa ya Tanzania-Taifa Stars itaivaa Benin katika mchezo wa kirafiki utakaochezwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mbali na mchezo huo mechi zingine zote ambazo zilikuwa zichezwe tarehe hiyo na siku inayofuata sasa zitachezwa wikiendi inayofuata ya Octoba 18 na 19.

BALOTELLI BADO HAJAFIKIA HADHI YA DUNIA - RODGERS.

MENEJA wa klabu ya Liverpool, Brendan Rodgers amekiri kuwa Mario Balotelli bado hajafikia hadhi ya kiwango cha dunia lakini amemuunga mkono kuwa anaweza kuvaa viatu vya Luis Suarez na kufanya vitu vikubwa Anfield. Suarez aliuzwa Barcelona kwa kitita cha euro milioni 88 katika usajili wa kiangazi huku nafasi yake ikizibwa na Balotelli aliyesajiliwa akitokea AC Milan kwa kitita cha euro milioni 20. Rodgers anaamini kuwa nyota huyo wa kimataifa wa Italia anapswa kufuata nyayo za Suarez akiwa hapo na kuonyesha thamani yake akiwa kama mshambuliaji. Rodegrs amesema pamoja na kwamba Balotelli hajafikia hadhi ya kiwango cha dunia lakini hana shaka na kipaji chake kwani ana uwezo wa kufikia huko kama akitilia maanani kazi yake hiyo.

SIHITAJI MAPUMZIKO - RONALDO.

MSHAMBULIAJI nyota wa klabu ya Real Madrid, Cristiano Ronaldo amesisitiza kuwa hahitaji muda wa mapumziko katika hatua hizo za mwanzo wa msimu. Nyota huyo wa kimataifa wa Ureno alipatwa na tatizo la majeruhi mwishoni mwa msimu wa 2013-2014 na wakati wa michuano ya Kombe la Dunia nchini Brazil. Hata hivyo, Ronaldo amesisitiza kuwa kwasasa yuko fiti na anataka kuendeleza makali yake aliyokuwa nayo kwa mabingwa hao wa Ulaya baada ya kufuinga mabao ya kutosha katika wiki chache zilizopita. Ronaldo alikaririwa akidai kuwa kwasasa wako mwanzoni mwa msimu na anataka kucheza ili kujijengea hali ya kujiamini na wakati utakapofika wakati muafaka ukifika atapumzika ili aweze kuwapa wenzake nafasi lakini huu sio wakati muafaka. Mpaka sasa Ronaldo ameshafunga mabao tisa katika mechi nne za ligi alizocheza msimu huu.

MAJERUHI WAMLIZA WENGER.

MENEJA wa klabu ya Arsenal, Arsene Wenger anaamini kuwa timu hiyo haina bahati kutokana na idadi ya mabeki wake waliokuwa majeruhi na kusisitiza kusajili wachezaji wa kuziba nafasi hizo katika usajili wa majira ya kiangazi ilikuwa kazi ngumu. Kuondoka kwa Thomas Vermaelen kwenda Barcelona kwa kitita cha euro milioni 19, kujumuisha na kushindwa kusajiliwa kwa beki wa kimataifa wa Ugiriki Kostas Manolas kumeifanya Arsenal kuanza msimu wakiwa na wachezaji sita pekee katika nafasi za ulinzi kati ya nne zilizopo. Kwasasa Arsenal wana majeruhi Mathieu Debuchy ambaye atakuwa nje kwa miezi mitatu wakati Ncho Monreal naye yuko nje kutokana na matatizo ya mgongo kumeifanya timu hiyo kuonyesha udhaifu mkubwa katika safu hiyo. Wenger amekiri kua matatizo ya majeruhi yamewasababishia matatizo mwanzoni mwa msimu huu lakini amedai alifanya kila analoweza kujaribu kusajili mabeki zaidi katika wakati wa kiangazi. Arsenal ilitumia zaidi ya euro milioni 888 kwa ajili ya kuwasajili Alexis Sanchez, Danny Welbeck, Calum Chambers, Debuchy na David Ospina katika majira haya ya kiangazi.

DEBRY ZA LIGI KUU MWISHONI MWA WIKI.

MWISHONI mwa wiki katika michezo ya Ligi Kuu nchini Uingereza tutashuhudia mechi mbili zitakazowahutanisha mahasimu katika miji wanayotoka. Kwa upande wa kaskazini mwa jiji la London Arsenal watawakaribisha majirani zao Tottenham Hotspurs wakati Liverpool wao watakuwa wenyeji wa majirani zao wa Merseyside timu ya Everton. Mechi hizo ambazo zitapigwa kesho zinaleta mvuto wa ziada kwani zote nne zinahitaji ushindi baada ya kuanza kwa kusuasua toka msimu ulipoanza. Liverpool ambao walipoteza taji kwa tofauti ya alama chache mbele ya Manchester City msimu uliopita na Everton kumaliza katika nafasi ya tano wakiweka rekodi kwa kukusanya alama nyingi zaidi, kwasasa wote wako chini katika nafasi ya 11 na 14 kuelekea katika mchezo wao huo. Kwa upande wa Arsenal wao kwasasa wanashika nafasi ya nne wakiwa wamejikusanyia alama tisa katika mechi tano walizocheza huku mahasimu wao Spurs wakiwa nafasi ya tisa kwa kujikusanyia alama saba.

KIONGOZI WA QATAR ATAMBA NCHI HIYO KUANDAA KOMBE LA DUNIA BORA ZAIDI KUWAHI KUTOKEA.

KIONGOZI wa Qatar, Sheikh Tamim bin Hamad al-Thani jana amesema taifa hilo la Ghuba litaandaa moja ya michuano bora kabisa katika historia ya Kombe la Dunia wakati watakapokuwa wenyeji wa michuano hiyo mwaka 2022. Qatar na Shirikisho la Soka Duniani-FIFA kwasasa wako chini ya shinikizo kali la kuondoa michuano hiyo ya mwaka 2022 kutoka katika nchi hiyo huku kukizungukwa na tuhuma za rushwa katika kupata nafasi hiyo. Ligi kubwa barani Ulaya pia zinapinga wazo la kuhamisha michuano hiyo kutoka kiangazi mpaka majira ya baridi ili kuepuka joto kali katika miezi ya kiangazi nchini Qatar. Akihojiwa na CNN kiongozi huyo amesema watu wanapaswa kuelewa kuwa Qatar ni mzabuni bora na anaweza kuandaa michuano bora kabisa kuwahi kutokea katika historia. Al-Thani aliendelea kudai kuwa tatizo la watu wengi hawataki kukubali kuwa nchi ndogo ya Kiarabu inaweza kuandaa michuano mikubwa kama hiyo. Kiongozi huyo aliendelea kutamba kuwa Qatar ina uwezo wa kuandaa michuano hiyo wakati wa kiangazi kama walivyoahidi tena bila tatizo lolote na kama wakiamua kubadili na kupeleka majira ya baridi pia wako tayari.

APPIAH AELEZA MADUDU YA PRINCE BOATENG.

HATIMAYE aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya Ghana Kwesi Appiah amezungumza sababu zilizomfanya kumtimua katika kikosi chake Kevin-Prince Boateng katika kambi ya timu hiyo nchini Brazil. Uamuzi wa kumtimua kiungo huyo wa klabu ya Schalke na kiungo wa AC Milan Suley Muntari uliteka vyombo vya habari vya kimataifa na Appiah amesema alifanya hivyo kwasababu ya kutokuwa mfano wa kuigwa kwa wenzake. Appiah amesema Boateng mara kadhaa amekuwa akitumia lugha ya matusi mazoezini na muda mwingi amekuwa akinyamaza kimya na kujifanya hakusikia. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa aliamua kufikia uamuzi wa kumtimua baada ya kuelekeza matusi hayo moja kwa moja kwake na mengine kwa viongozi wenzake wa benchi la ufundi. Appiah amesema alikuwa hana nia ya kumuondoa lakini wakati alipotoa matusi hayo mbele ya wachezaji wenzake akaona hana jinsi kwani alikuwa analeta mfano mbaya mbele ya wachezaji wadogo.

RUFANI YA KABYLIE YATUPWA.

Albert Ebosse
KAMATI ya nidhamu ya Shirikisho la Soka la Algeria imetupilia mbali rufani ya klabu ya JS Kabylie kupunguza adhabu waliyopewa kufuatia kutopkea kwa kifi kwa mchezaji wa kimataifa wa Cameroon Albert Ebosse katika uwanja wao wa nyumbani mwezi uliopita. Kabylie walikutwa na hatia ya uzembe baada ya tukio hilo lililotokea katika Uwanja wa Novemba 1st uliopo huko Tizo Ouzou ambapo walifungiwa kutumia uwanja huo mpaka watakapopewa taarifa vinginevyo. Klabu hiyo yenye maskani yake kaskazini mwa Algeria pia itacheza mechi zake za nyumbani za ligi zilizosalia katika uwanja huru na bila kuwa na mashabiki. Uongozi wa klabu hiyo sasa umedai kuwa utapeleka suala hilo katika mahakama ya michezo ya nchi hiyo. Ebosse alitandikwa na kitu kizito kichwani kilichoruswa na shabiki mwenye hasira wakati wachezaji wa Kabylie akitoka uwanjani baada ya kufungwa na USM Alger mabao 2-1 Agosti 23 mwaka huu. Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 24 alifariki saa chache baadae akiwa hospitalini kufuatia damua kuganda katika ubongo kutokana na tukio hilo.

LAMPARD AKANUSHA KUFANYA MAZUNGUMZO NA CITY.

KIUNGO mkongwe wa klabu ya Manchester City, Frank Lampard amesema hajafanya mazungumzo yoyote na klabu hiyo kuhusu kuongeza muda wake wa mkopo. Kiungo huyo wa zamani wa kimataifa wa Uingereza mwenye umri wa miaka 36 amefunga mabao matatu katika katika mechi tatu alizoichezea City toka ajiunge nao kipindi hiki cha kiangazi akitokea timu ya New Yorkl City inayoshiriki Ligi Kuu nchini Marekani-MLS. Mkataba wa mkopo wa Lampard unatarajiwa kumalizika Januari lakini meneja wa City Manuel Pellegrini alikaririwa mapema wiki hii kuwa anaweza kuendelea kuwepo. Akiulizwa kuhusu suala hilo, Lampard amesema kwasasa hawezi kusema kusema chochote kuhusu kuendelea kwani anachojua mkataba wake unamalizika Januari. Lampard ambaye alistaafi soka la kimataifa Agosti baada ya kuitumikia nchi yake kwa michezo 106, alicheza mechi yake ya kwanza akiwa na City katika sare ya mabao 2-2 dhidi ya Arsenal Septemba 13 mwaka huu.

SUAREZ AITWA URUGUAY.

LUIS Suarez amekuwa mmoja kati ya wachezaji 29 walioitwa katika kikosi cha awali cha timu ya taifa ya Ureno kwa ajili ya mechi za kirafiki mwezi ujao dhidi ya Saudi Arabia na Oman. Kocha wa timu hiyo Oscar Tabarez bado atahitajika kuamua kama atamchukua Suarez kwa ajili ya michezo hiyo ambapo mmoja dhidi ya Saudi Arabia utachezwa Octoba 10 huku ule dhidi ya Oman ukichezwa siku tatu baadae. Suarez yuko anatumikia adhabu ya mechi nane za kimataifa kwa kosa la kumng’ata Giorgio Chiellini katika Kombe la Dunia, hivyo inamaanisha kuwa atakosa michuano ya Copa Amerika mwakani na baadhi ya mechi za kufuzu Kombe la Dunia 2018. Adhabu hiyo hiyo inamzuia kucheuia kucheza mechi za mashindano katika klabu yake ya Barcelona mpaka mwezi ujao. Tabarez hakumuita Suarez katika mechi mbili za kirafiki zilizochezwa mwezi huu dhidi ya Japan na Korea Kusini ambazo zote Uruguay ilishinda.

SIMBA NA YANGA SASA KUVAANA OCTOBA 18.

MCHEZO wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaowakutanisha watani wa jadi Yanga na Simba umesogezwa mbele mpaka Octoba 18 mwaka huu kutokana na ratiba ya ligi kufanyiwa marekebisho. Ratiba hiyo ambayo hapo awali ilielekeza mchezo huo kuchezwa Octoba 12 sasa imesogezwa mbele ili kupisha ratiba ya mechi za kimataifa ambayo iko katika kalenda ya Shirikisho la Soka Duniani-FIFA. Badala ya mchezo huo sasa timu ya taifa ya Tanzania-Taifa Stars itaivaa Benin katika mchezo wa kirafiki utakaochezwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mbali na mchezo huo mechi zingine zote ambazo zilikuwa zichezwe tarehe hiyo na siku inayofuata sasa zitachezwa wikiendi inayofuata ya Octoba 18 na 19.

Thursday, September 25, 2014

TIMU YA KIKAPU YA WANAWAKE YA QATAR YAJITOA KATIKA MASHINDANO KWA KUNYIMWA KUVAA HIJAB.

TIMU ya taifa ya mpira wa kikapu ya wanawake ya Qatar imejitoa katika michuano ya Asia inayofanyika nchini Korea Kusini baada ya kukataliwa ombi lao la kutaka kuruhusiwa kutumia hijab wakati michuano hiyo. Wachezaji wa timu hiyo walitakiwa kuondoa vitambaa kichwani ambavyo hutumiwa na wanawake wa dini ya Kiislamu kabla ya mchezo dhidi ya Mongolia lakini walikataa na kupoteza mchezo huo. Sheria za mchezo huo duniani imeorodhesha kofia za kichwani na vibanio vya nywele kama vitu visivyotakiwa uwanjani. Huku kukiwa na hakuna dalili kwanza sheria hiyo inaweza kubadilishwa kabla ya mchezo wao unaofuata dhidi ya Nepal, timu hiyo imemua kujitoa. Michezo mingine katika mashindano hayo ya Asia yanaruhusu wanamichezo kuvaa hijab ambapo kilele chake kinatarajiwa kuwa Octoba 4 mwaka huu.

CAIN HOY YAJITOA KUINUNUA SPURS.

KAMPUNI ya uwekezaji ya Marekani ya Cain Hoy imedai kuwa haifikirii tena kutoa ofa kwa ajili ya kuinunua klabu ya Tottenham Hotspurs. Septemba mwaka huu kampuni hiyo ilithibitisha kuwa iko katika hatua za awali za kupitia ofa kwa ajili ya kuinunua klabu hiyo ya Ligi Kuu. Lakini kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa katika soko la hisa la London, kampuni imedai kusitisha nia yake hiyo. Cain Hoy wana muda mpaka Octoba 10 mwaka huu kuhthibitisha nia yao au kujiondoa rasmi katika kinyang’anyiro hicho. Kwasasa Spurs inajaribu kukusanya fedha kwa ajili ya mpango wa ujenzi wa uwanja mpya utakaokuwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 56,250.

GYAN AKANA KUMTOA KAFARA RAFIKI YAKE.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Ghana, Asamoah Gyan ametoa taarifa kukanusha kuhusika na kifo cha mwanamuziki wa rap nchini Ghana Castro. Castro ambaye ni rafiki wa mshambuliaji huyo wa zamani wa klabu ya Sunderland alipotea katika mazingira ya kutatanisha sambamba na rafiki yake wa kike Janet Bandu Julai mwaka huu. Mwanamuziki huyo ambaye jina lake halisi ni Theophilus Tagoe na mpenzi wake walitoweka baharini wakati wakiwa likizo na familia ya Gyan jijini Ada. Kumekuwa na taarifa za kuhusishwa na mambo ya kimazingara kwa kupotea kwa Castro jambo ambalo limepingwa na Gyan kwa kukataa kuhusika na lolote. Miili ya wawili hao haikuwahi kupatikana na madai yaliendelea kusambazwa mwezi huu wakati ambapo kakake Gyan, Baffour Gyan alidaiwa kuwa mmoja wa genge la vijana waliowashambulia wandishi wa habari waliohoji maswali kuhusu madai hayo. Wakili wake Kissi Agbyabeng alitoa taarifa akisema kuwa familia ya Gyan imeshangazwa sana na madai hayo na iliamua kutosema chochote ili polisi waendelee na uchunguzi wao.

CAF CHAMPIONS LEAGUE 2014: SETIF, VITA KUVUNJA MWIKO?

KLABU za Entente Setif ya Algeria na Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo-DRC mwishoni mwa wiki hii zinaweza kuandika historia mpya katika mechi zao za nusu fainali za mkondo wa pili wa michuano ya Mataifa ya Afrika. Setif na Vita zilitengenezea ushindi wa mabao 2-1 katika mechi zao za nyumbani dhidi ya TP Mazembe ya DRC na CS Sfaxien ya Tunisia. Lakini katika historia ya miaka 49 ya mashindano hayo katika timu saba ambazo zilijitengenezea ushindi kama huo katika mechi ya kwanza ya nusu fainali hazikufanikiwa kutinga fainali. Klabu ambacho zimewahi kutangulia na ushindi kama huo lakini baadae kushindwa kumaliza kazi walioanza ni pamoja na ASEC Mimosas ya Ivory Coast, Lome 1 ya Togo, Diaraf na Jeanne d’Arc zote za Senegal, Canon Younde ya Cameroon, El-Hilal ya Sudan na Al-Ahly ya Misri.

ODIMWINGIE APIGWA KISU.

MSHAMBULIAJI wa klabu ya Stoke City, Peter Odimwingie amethibitisha kuwa upasuaji wake wa goti aliofanyiwa umekuwa wa mafanikio. Mshambualiji huyo wa kimataifa wa Nigeria alipata majeruhi hayo Agosti 30 wakati Stoke ilipoitandika Manchester City bao 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu uliofanyika katika Uwanja wa Etihad. Odemwingie alithibitisha taarifa hizo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa twitter huku pia akikipongeza kikosi chao kwa kutinga mzunguko wa nne wa michuano ya Kombe la Ligi. Nyota huyo ambaye hatarajii kurejea uwanjani kwa mwaka huu anaamini Stoke inaweza kuendelea kufanya vyema bila uwepo wake.

NEYMAR ANANIKUMBUSHA ALIVYOKUWA ROMARIO - DUNGA.

KOCHA wa timu ya taifa ya Brazil, Dunga amesema Neymar anamkumbusha jinsi alivyokuwa mshambuliaji nguli Romario na kudai kuwa atakuwa mfano wa kuigwa katika soka duniani. Nyota huyo wa klabu ya Barcelona ameanza vyema msimu huu kwa kufunga mabao matatu katika mechi nne za ligi baada ya kuifungia pia Brazil mabao manne katika Kombe la Dunia kabla ya kuumia mgongo katika robo fainali na kumfanya kutocheza tena michuano hiyo. Dunga amemfananisha Neymar na nyota mwingine wa zamani wa Barcelona na Brazil Romario ambaye amewahi kufanya naye kazi na kudai kuwa kama ilivyo kwa nguli huyo, Neymar naye anafanya kama aliyowahi kufanya wakati akicheza. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa Neymar ni kiongozi wa ufundi na pia ni mfano wa kuigwa nchini Brazil na dunia kwa ujumla jambo ambalo ndiovyo ilivyokuwa kwa Romario enzi zake. Dunga pia alidokeza uwezekano wa kumuita kiungo Kaka katika kikosi chake kama akiendelea kucheza kwa kiwango cha juu kama hivi sasa katika klabu yake ya Sao Paulo.

LIVERPOOL YAINGIA MATATANI UEFA.

KLABU ya Liverpool ni moja ya vilabu kadhaa vinavyotarajiwa kufanyiwa uchunguzi kama wamekiuka Sheria ya Matumizi ya Fedha-FFP. Kwa mujibu wa sheria za Shirikisho la Soka barani Ulaya-UEFA vilabu vyote barani humo vinapaswa kuweka kikomo cha hasara kutofikia paundi milioni 35.4 kwa misimu miwili. Kuna adhabu hutolewa kwa wasiotimiza masharti hayo ambapo Manchester City tayari wameshakumbana nayo kwa kutozwa faini na kuwekewa kiwango cha matumizi katika usajili na kupunguziwa idadi ya wachezaji katika kikosi chake Mei mwaka huu. Lakini pamoja na kupata hasara ya paundi milioni 49.8 katika msimu wa mwaka 2012-2013 na paundi milioni 41 msimu wa mwaka 2011-2012, Liverpool wana uhakika wanaweza kuvuka kikwazo hicho bila adhabu. Liverpool sambamba na vilabu vya Monaco, Inter Milan na AS Roma ambazo zote hazikushiriki michuano ya Ulaya msimu uliopita tarayi zimepeleka taarifa za akaunti zao Bodi ya Udhibiti wa Fedha ya Klabu-CFCB lakini kuna uwezekano wa kuagizwa kupelekea maelezo zaidi kuhusu fedha hizo. Msimu uliopita vilabu 76 viliingia katika uchunguzi wa FFP lakini vilabu tisa pekee ndio vilipewa adhabu kwa kukiuka sheria hiyo.

KOMBE LA LIGI: LIVERPOOL KUIVAA SWANSEA, MAN CITY NA NEWCASTLE, CHELSEA WAPEWA VIBONDE KUTOKA DARAJA LA NNE.

MENEJA wa klabu ya Liverpool, Brendan Rodgers anatarajia kukwaana na klabu yake ya zamani ya Swansea City katika mzunguko wa nne wa michuano ya Kombe la Ligi kufuatia ratiba iliyopangwa jana. Liverpool ambao walitinga hatua hiyo baada ya kuitoa Middlesbrough kwa changamoto ya mikwaju ya penati 14-13, watakuwa wenyeji wa Swansea ambao kwasasa wanashika nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu. Mabingwa watetezi wa michuano hiyo Manchester City wao watakuwa wenyeji wa Newcastle United na vinara wa Ligi Kuu Chelsea watasafiri kuifuata timu ya daraja la nne ya Shrewsbury Town ambayo ni timu ya daraja la chini zaidi kubakia katika michuano hiyo. Mechi nyingine Stoke City wao watakuwa wenyeji wa Southampton huku Tottenham Hotspurs nao wakiikaribisha timu ya daraja la pili Brighton & Hove Albion. Wengine ni West Bromwich Albion ambao watakuwa wageni wa timu ya daraja la pili Bournemouth, MK Dons watachuana na wenzao wa daraja la tatu Sheffield United huku Fulham nao wakiwakaribisha wenzao wa daraja la pili Derby County.

FIFA YATUPILIA MBALI RUFANI YA SANTOS.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA limetupilia mbali rufani ya kocha mpya wa timu ya taifa ya Ureno Fernando Santos aliyokuwa kipinga kufungiwa mechi nane kutokana na makosa ya utovu wa nidhamu katika michuano ya Kombe la Dunia. FIFA imedai katika taaifa yake kuwa kamati yake ya rufani imekataa uitetezi wa kocha huyo wa zamani wa Ugiriki. Santos sasa aneweza kukata tena rufani katika Mahakama Kimataifa ya Michezo-CAS. Kocha huyo aliajiriwa na Shirikisho la Soka la Ureno Juzi pamoja na kuwa amefungiwa kukaa katika benchi la ufundi kwa mechi nane. Santos ataanza kutumikia adhabu yake hiyo wakati wa mechi za kufuzu michuano ya Ulaya ingawa ameruhusiwa kuchagua mechi na kuhudhuria vipindi vya mazoezi. Santos mwenye umri wa miaka 59, aliwatukana waamuzi wakati Ugiriki ilipotolewa na Costa Rica katika hatua ya timu 16 bora katika michuano hiyo iliyofanyika nchini Brazil.

DAKTARI ATHIBITISHA MUSANA ALIKUFA KWA BRONCOPNEUMONIA.

RIPOTI ya daktari aliyefanyia uchunguzi mwili wa mchezaji wa klabu ya Simba Fahad Musana imedai kuwa mchezaji huyo alifariki duniani kutokana na kusumbuliwa na tatizo la kupumua kwa kitaalamu bronchopneumonia. Taarifa hiyo iliwasilishwa na meneja wa klabu hiyo Perez Muwezi juzi wakati wa mazishi ya mchezaji huyo katika kijiji cha Walugogo, wilaya ya Iganga nchini Uganda. Taarifa hiyo ilitolewa kutoka hospitali ya rufaa ya taifa ya Mulago na kusainiwa na daktari aliyefanya uchunguzi huo Acola Caroh. Musana alifariki dunia Jumapili iliyopita wakati akiangalia mchezo wa Ligi Kuu nchini Uingereza kati ya Chelsea na Manchester City huko Bombo ambapo ndipo maskani ya klabu yake ya Simba.

TAIFA STARS, BENIN KUCHEZA DAR OKTOBA 12.

TIMU ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inashuka uwanjani Oktoba 12 mwaka huu kuikabili Benin katika mechi ya kirafiki ya kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA). Mechi hiyo itachezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni. Programu ya Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager kwa ajili ya mechi hiyo itatangazwa baadaye na Kocha Mkuu Mart Nooij. Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linaendelea na taratibu nyingine kwa ajili ya mechi hiyo ikiwemo usafiri wa Benin kuja nchini, ambapo timu hiyo inatarajiwa kutua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Oktoba 10 mwaka huu ikiwa na msafara wa watu 28. Pambano la Stars na Benin litatanguliwa na mechi ya kudumisha upendo kati ya viongozi wa dini ya Kikristo na Kiislamu. Wakati huo huo, kutokana na mechi hiyo ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inafanyiwa marekebisho madogo, na marekebisho hayo yatatangazwa kesho (Septemba 26 mwaka huu).



RAIS MALINZI KUFUNGA KOZI YA WANAWAKE
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi anatarajia kufunga mafunzo ya uongozi kwa viongozi wa vyama vya mpira wa miguu wa wanawake vya mikoa ya Tanzania Bara. Hafla ya kufunga mafunzo hayo itafanyika kesho (Septemba 26 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za TFF, Uwanja wa Karume, Dar es Salaam. Mafunzo hayo ya siku tano yalishirikisha viongozi 34 wakiwemo baadhi ya waandishi wa habari na Meneja wa Twiga Stars, na yaliendeshwa na Mkufunzi wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Henry Tandau.

Wednesday, September 24, 2014

MILNER ATAKA UHAKIKA WA NAMBA KABLA YA KUSAINI MKATABA MPYA.

KIUNGO wa Manchester City, James Milner amekiri kuwa anataka uhakika kwa namba katika kikosi cha kwanza kabla ya kuamua kuongeza mkataba mwingine katika klabu hiyo zaidi ya msimu huu. Milner anamaliza mkataba wake mwishoni mwa msimu huu na wakati City wakihaha kuhakikisha wanamuongeza mkataba mwingine, nyota huyo wa kimataifa wa Uingereza hana na suala hilo kwasasa. Baada ya kuachwa katika benchi katika mechi tatu za Ligi Kuu za mwanzo za City, Milner mwenye umri wa miaka 28 alianza katika michezo iliyofuatia ya ligi dhidi ya Arsenal na Chelsea. Milner mwenyewe amesema anataka kuangalia mambo yanavyokwenda kwanza kabla ya kukubali mkataba mpya huku suala la kuanza katika kikosi cha kwanza likiwa jambo la kwanza katika akili yake. Milner aliendelea kudai kuwa anajua amebakisha mwaka mmoja katika mkataba wake na tayari ameshazungumza na klabu na anapenda kubakia hapo ila jambo la kwanza kama mchezaji anahitaji kucheza mara kwa mara.

ALGERIA SASA YAJITOSA KUWANIA AFCON 2017.

BAADA ya kukosa nafasi ya uandazi wa michuano ya Mataifa ya Afrika-AFCON mwaka 2019, 2021 na 2023, Shirikisho la Soka la Algeria sasa limetangaza kutuma maombi ya kutaka uenyeji wa michuano hiyo mwaka 2017. Taifa hilo lililopo kaskazini mwa bara la Afrika litachuana na nchi za Ethiopia, Ghana, Kenya, Tanzania, Mozambique, Zimbabwe na Misri katika kugombea nafasi hiyo. Libya ilishindwa kuandaa michuano hiyo kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea nchini humo toka kuondolewa kwa utawala wa Muamar Gaddafi. Mshindi katika kinyang’anyiro hicho anatarajiwa kutangazwa mapema mwakani na Shirikisho la Soka barani Afrika-CAF. Cameroon wao walishinda haki za kuandaa michuano hiyo mwaka 2019 wakati Ivory Coast na Guinea wao walipata nafasi ya kuandaa michuano ya mwaka 2021 na 2023.

KLOPP AUNGANA NA GUARDIOLA KUTETEA AFYA ZA WACHEZAJI KUTOKANA NA RATIBA NGUMU ZA MECHI.

MENEJA wa klabu ya Borussia Dortmund, Jurgen Klopp amemuunga mkono Pep Guardiola kwa kauli yake kuwa ratiba ya mechi nyingi inaumiza afya za wachezaji. Guardiola ambaye anainoa Bayern Munich alilalamika kuwa ratiba iliyobana katika soka la wakati huu linawaumiza sana wachezaji na Klopp sasa ameonya kuwa wachezaji watalazimika kustaafu soka mapema pindi wafikishapo miaka 30 kama hali hiyo haitabadilika. Klopp amekaririwa akidai kuwa katika kipindi cha miaka 10 inayokuja kutakuwa hakuna wachezaji wanaoweza kucheza mpaka kufikia umri wa miaka 35. Klopp amesema wachezaji wa zamani walioshika nafasi muhimu katika uongozi wameshasahau jinsi mambo yalivyokuwa magumu wakati wakicheza soka. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa michuano ya Ulaya mwakani itakuwa na timu 24 kwasababu baadhi ya watu wanaona ni wazo zuri lakini wanasahau kuwa wanawaumiza wachezaji kwa kuwachezesha mechi nyingi zaidi.

LA GALAXY YATHIBITISHA KUMTAKA PIRLO.

KIUNGO mahiri wa kimataifa wa Italia, Andrea Pirlo anatarajiwa kufanya uhamisho wa kushtukiza kwenda klabu ya Los Angeles Galaxy ya Marekani. Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 35 ambaye kwasasa anakipiga katika klabu ya Juventus amecheza soka nchini Italia katika muda wake wote lakini pamoja na kupewa mkataba wa miaka zaidi galaxy wanafikiria kumsajili nyota huyo. Klabu hiyo ya zamani ya David Beckham inamtaka kiungo huyo mkongwe kuziba nafasi ya London Donovan ambaye ametangaza kustaafu soka mwishoni mwa msimu wa Ligi Kuu ya Soka nchini Marekani-MLS baadae mwaka huu. Mwezi uliopita Pirlo alikaririwa akidai kuwa hana sababu ya kuhama kwani anaona maisha bado mazuri Juventus na kuongeza kuwa labda baada ya miaka miwili ya mkataba wake kunalizika anaweza kufikiria kwenda Marekani. Hata hivyo muda huo unawezekana usifike kwani kocha wa Galaxy Bruce Arena tayari amethibitisha nia yao ya kumsajili mkongwe huyo.

KOCHA WA ELCHE AMFANANISHA RONALDO NA MICHAEL JORDAN BAADA YA KUTUPIA NNE.

MENEJA wa klabu ya Elche, Fran Escriba amemfananisha Cristiano Ronaldo na nguli wa mpira wa kikapu nchini Marekani Michael Jordan baada ya mshambuliaji huyo wa Real Madrid kuonyesha kiwango cha hali ya juu katika mchezo wa La Liga uliochezwa jana. Katika mchezo huo Ronaldo alifunga mabao manne wakati Madrid walipotoka nyuma na kuibuka na ushindi wa mabao 5-1 katika Uwanja wa Santiago Bernabeu. Ronaldo mwenye umri wa miaka 29 sasa ameipita rekodi ya Santillana kwa kuwa mfungaji wa tatu aliyefunga mabao mengi zaidi katika klabu hiyo kwa kufikisha mabao 187 huku akifunga hat-trick yake ya 25 akiwa na Madrid toka alipotoka Manchester United mwaka 2009. Sasa Ronaldo anakaribia rekodi iliyowekwa na nguli Alfredo Di Stefano ambaye ndio kinara wa mabao anayeoongoza katika klabu hiyo kwa kipindi chote. Escriba alimmwagia sifa Ronaldo baada ya mchezo huo kwa kumfananisha na Jordan ambaye amewahi kushinda mataji sita ya Ligi ya Mpira wa Kipapu nchini Marekani-NBA huku akinyakuwa tuzo tano za mchezaji mwenye thamani zaidi-MVP. Escriba amesema Ronaldo ni mchezaji wa kipekee mwenye uwezo wa hali ya juu kufunga ndio maana anamfananisha na Jordan enzi zake wakati akicheza na kufunga alama 50 katika mechi moja.

GIBBS, MATERSACKER FITI KUIVAA SPURS JUMAMOSI.

MENEJA wa klabu ya Arsenal, Arsene Wenger amesema anategemea Per Martesacker na Kieran Gibbs kurejea katika kikosi cha timu yake katika mchezo wa Jumamosi ambao watakutana na mahasimu wao wa kaskanini mwa jijini la London Tottenham Hotspurs. Majeraha madogo madogo yalipelekea Martersacker na Gibbs kukosa mchezo wa Kombe la Ligi dhidi ya Southampton na kupelekea Wenger kuwatumia mabeki wasio wazoefu akiwemo Hector Bellerin na Isaac Hayden. Kukosekana kwa Nacho Monreal kunamaanisha Calum Chambers ndio mchezaji pekee katika safu ya ulinzi mwenye uzoefu aliyechezeshwa na Wenger lakini kinda huyo amecheza katika mechi saba pekee za Arsenal toka alipojiunga akitokea Southampton. Katika mchezo huo Arsenal walitandikwa nyumbani mabao 2-1 na Southampton lakini Wenger ana uhakika kuwa mabeki wake wazoefu Matersacker na Gibbs watakuwa fiti kwa ajili ya mchezo wa Jumamosi. Safu ya ulinzi ya Arsenal ilizidi kupungua baada ya taarifa za Jumatatu kuwa beki wa kimataifa wa Ufaransa Mathieu Debuchy atakosekana dimbani kwa miezi mitatu kufuatia kufanyiwa upasuaji wa kifundo cha mguu wake wa kushoto.

Tuesday, September 23, 2014

SUAREZ KUCHEZA MECHI YA KIRAFIKI YA KIKOSI B CHA BARCELONA.

MENEJA wa Barcelona, Luis Enrique amethibitisha kuwa Luis Suarez atacheza katika kikosi B cha timu hiyo katika mchezo wao wa kirafiki dhidi ya timu ya vijana na Indonesia kesho. Nyota huyo wa kimataifa wa Uruguay alisajiliwa Barcelona kwa kitita cha euro milioni 88 Julai lakini bado hajapata nafasi ya kucheza kutokana na kutumikia adhabu ya kufungiwa miezi minne kwa kumng’ata Giorgio Chiellini ambapo adhabu inatarajiwa kumalizika Octoba 25 mwaka huu. Hata hivyo, Enrique amebainisha kuwa atamchezesha mshambuliaji huyo ili kumpa mazoezi kabla ya kurejea katika kikosi cha kwanza pindi atakapomaliza adhabu yake. Kocha huyo amesema ni jambo jema kwa Suarez kucheza kwani anakuwa ajiweka fiti tayari kwa mechi baada ya kukaa nje kwa muda mrefu bila kucheza mechi ya mashindano. Wakati Suarez akitarajia kucheza katika kikosi B hapo kesho, wachezaji wenzake wa kikosi cha kwanza watasafiri kuifuata Malaga huku wakiwa na matumaini ya kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa La Liga.

LIVERPOOL YARUHUSIWA KUUTANUA UWANJA WA ANFIELD.

KLABU ya Liverpool imepewa ruhusa ya kutanua Uwanja wa Anfield kutokana uwezo wa kubeba mashabiki 45,500 mpaka 59,000 ikiwa ni sehemu ya mpango utakaogharimu kiasi cha paundi milioni 100. Kamati ya mipango ya halmashauri ya mji wa Liverpool imepitisha mpango wa kutanua jukwaani kubwa kwa viti 8,300 na jukwaa linatizama barabara kwa viti 4,800. Mapendekezo hayo yamejumuisha ukumbi wa mikutano na sehemu za kutunzia vifaa, maduka mapya na eneo la ziada la kuegesha magari. Ujenzi wa upanuzi unatarajiwa kuanza rasmi mwakani huku ukitarajiwa kukamilika msimu wa 2016-2017. Mpango huo utaifanya klabu hiyo kuweza kuandaa mechi za kimataifa sambamba na mechi za Ulaya. Uwanja wa Anfield ulifungiliwa rasmi mwaka 1884 ukiwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 20,000 na ulikuwa ukitumiwa na timu ya Everton mpaka walipoondoka na kwenda katika Uwanja wao wa Goodison Park na klabu ya Liverpool ilipoanzishwa mwaka 1892 ndio ikachukua uwanja huo.

SANTOS ATEULIWA KUWA KOCHA WA URENO.

SHIRIKISHO la Soka nchini Ureno, FPF limemteua Fernando Santos kuwa kocha mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo. Katika taarifa ya FPF iliyotumwa katika mtandao ilithibitisha habari hiyo ya kumuajiri Santos ambaye alikuwa akiinoa timu ya taifa ya Ugiriki hapo kabla. Santos ambaye aliingoza Ugiriki katika hatua ya timu 16 bora katika michuano ya Kombe la Dunia nchini Brazil ambapo walikuja kufungwa na Costa Rica kwa matuta anachukua nafasi ya Paulo bento aliyetimuliwa. Kibarua chake cha kwanza akiwa na Ureno, utakuwa mchezo unaiofuata wa kufuzu michuano ya Ulaya dhidi ya Denmark Octoba 14 mwaka huu.

ESSIEN PANCHA TENA.

KIUNGO mahiri wa kimataifa wa Ghana, Michael Essien anatarajiwa kuwa nje kwa wiki mbili kutokana na majeruhi. Kiungo wa klabu ya AC Milan alipata majeraha ya mguu wakati wa maandalizi ya mchezo wa Serie A wa mwishoni mwa wiki iliyopita dhidi ya Juventus ambao walifungwa bao 1-0. Essien hatarajiwi kuwa sehemu ya kikosi cha wachezaji 23 watakaosafiri kwenda kupambana na Empoli. Nyota huyo amekuwa akiandamwa na majeruhi katika miezi ya karibuni kwani alishindwa kuitumikia vyema timu yake ya taifa kutoka matatizo ya majeruhi hatua am,bayo ilichangia kuondolewa mapema.

WALCOTT KUREJEA UWANJANI OCTOBA.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Uingereza, Theo Walcott anatarajiwa kurejea uwanjani tena uwanjani kuitumikia timu yake ya Arsenal Octoba baada ya kukaa nje kwa miezi 10 kutokana na majeruhi goti. Walcott anatarajiwa kurejea baada ya mapumziko ya mechi za kimataifa ambapo Uingereza itacheza na San Marino Octoba 9 na Estonia siku tatu baadae. Walcott mwenye umri wa miaka 25 aliumia goti lake la kushoto wakati wa mchezo wa Kombe la FA mzunguko wa tatu dhidi ya Tottenham Hotspurs Januari mwaka huu. Majeruhi hayo yalipeleka kukosa michuano ya Kombe la Dunia iliyofanyika nchini Brazil. Kama akifanikiwa kurejea uwanjani mwezi ujao, anaweza kujumuishwa katika kikosi cha timu ya taifa ya Uingereza kitakachoachuana na Slovenia katika mchezo wa kufuzu michuano ya Ulaya Novemba 15.

MECHI ZA LIGI KUU UGANDA KUSIMAMA KWA DAKIKA KWA HESHIMA YA MCHEZAJI ALIYEAGA DUNIA AKITIZAMA MECHI CITY NA CHELSEA.

VILABU vinavyoshiriki Ligi Kuu nchini Uganda vinatarajia kusimama kwa dakika moja na kuvaa vitambaa vyeusi kabla ya kuanza kwa mechi zao wiki hii kwa heshima beki wa timu ya Simba Fahad Musana aliyefariki dunia mwishoni mwa wiki iliyopita. Musana mwenye umri wa miaka 24 alifariki dunia Jumapili wakati akitizama mchezo wa Ligi Kuu ya Uingereza kati ya Manchester City na Chelsea timu ambayo ni anaishabikia. Taarifa zinadai kuwa Musana ambaye alizikwa leo nyumbani kwake katika wilaya ya Iganga alifariki kwa shinikizo baada ya timu yake ya Chelsea kufungwa bao la kusawazisha dakika za mwisho wakati wengine wanadai alikuwa ameshafariki wakati Frank Lampard akiisawazishia City. Jambo lingine linalohusishwa na kifo cha mchezaji huyo ni katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Entebe uliochezwa Jumamosi iliyopita ambapo Musana aligongwa kichwani.

FIFA KUANZISHA MPANGO MPYA KUWALINDA ZAIDI WACHEZAJI.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA linatarajia kuwasilisha pendekezo katika kamati ya utendaji la kuangalia mbinu mpya za kukabiliana na majeraha ya kichwa. Kiongozi wa kamati ya tiba ya FIFA, Michel D’Hooghe aliandaa mpango huo mapema mwezi huu. Mpango huo unampa nafasi mwamuzi kusimamisha mchezo kwa dakika tatu ili daktari wa timu aweze kufanya tathmini yake uwanjani huku pia akipewa rungu la kuamua kama mchezaji anaweza kuendelea kucheza. Mapendekezo hayo yanafanana na taratibu mpya za Ligi Kuu zilizotolewa mwanzoni mwa msimu huu na ambazo pia ziliwasilishwa Shirikisho la Soka barani Ulaya-UEFA Septemba 18 mwaka huu. Kama mapendekezo hayo yakipitishwa na FIFA na UEFA, yataanza kufanya kazi kuanzia Octoba na kujumuishwa katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, Europa League pamoja na mechi za kimataifa.

SINA SHAKA NA GERRARD - RODGERS.

MENEJA wa klabu ya Liverpool Brendan Rodgers amesisitiza kuwa hana mashaka na Steven Gerrard baada ya kupoteza michezo mitatu kati ya mitano ya Ligi Kuu waliyocheza msimu huu. Gerrard ambaye ni nahodha wa Liverpool alikuwa akihaha huku na kule katika mchezo wa Jumamosi dhidi ya West ham United ili kuona uwezekano kama anaweza kubadilisha matokeo. Hata hivyo mambo hayakwenda kama walivyotarajia kwani mwisho wa mchezo walijikuta wamechapwa mabao 3-1 na timu hiyo. Rodgers amekaa kumshuhia lawama nahodha wake huyo kwa kudai kuwa kikosi kizima hakucheza vizuri katika mchezo huo waliopoteza. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa Gerrard bado ana mchango mkubwa sana kwa timu hiyo.

MAN UNITED INAHITAJI KUTUMIA PAUNDI MILIONI 100 ZAIDI ILI WAWEZE KUSHINDA TAJI LA LIGI KUU - NEVILLE.

BEKI wa zamani wa Manchester United, Phil Neville amedai kuwa klabu hiyo inahitaji kutumia tena kitita cha paundi milioni 100 kwa ajili ya kununua wachezaji kabla ya kuanza kushindania taji la Ligi Kuu nchini Uingereza. United ilitandikwa kwa mabao 5-3 na Leicester City Jumamosi iliyopita lakini Neville amesema hakushangazwa na matokeo hayo. Neville mwenye umri wa miaka 37 amesema anajua kuwa United wametumia kitita cha paundi 150 katika usajili uliopita lakini anafikiri vipindi vingine viwili vya usajili ambavyo watahitajika kutumia kiasi kama hicho cha pesa kabla ya kuanza kufikiria kushionda taji. Meneja mpya wa United Louis van Gaal alitumia kitita cha paundi milioni 150 kuwasajili viungo Angel Di Maria, Ander Herrera na Daley Blind pamoja na mabeki Marcos Rojo na Luke Shaw wakati Mshambuliaji Radamel Falcao yeye alichukuliwa kw amkopo wa paundi milioni sita. Neville amesema United kwasasa wanapaswa kuangalia uwezekano wa kupata beki mzuri wa kati sambamba na kiungo mkabaji au mchezaji anayeweza kucheza nafasi ya kiungo wa kati. Tyler Blackett mwenye umri wa miaka 20 ndio amekuwa akicheza nafasi ya beki wa kati katika mechi tano za Ligi Kuu za United msimu huu lakini alionekana kuzidiwa na kasi ya Leicester na kutolewa nje.

HUWEZI KUMFANANISHA GOTZE NA RIBERY - BECKERNBAUER.

RAIS wa heshima wa klabu ya Bayern Munich, Franz Beckenbauer amesisitiza kuwa Mario Gotze hawezi kufananishwa na Franck Ribery kwakuwa ni wachezaji wa aina ya tofauti. Nyota huyo wa zamani wa Borussia Dortmund alihamishwa nafasi yake na kocha Pep Guardiola kutoka kati kwenda wingi ya pembeni mara kadhaa wakati Ribery alipokuwa kijiuguza. Hata hivyo, Beckernbauer haoni kama Gotze ni mchezaji muafaka kuziba nafasi ya Ribery. Nguli huyo wa soka wa zamani amesema huwezi kumuiga mtu kama Ribery kutokana na aina yake ya uchezaji ya kutanua uwanjani ili kuwavuta mabeki wa upinzani. Beckernbauer aliendelea kudai kuwa Gotze yuko tofauti na anadhani anafaa kwa mbinu za Guardiola kwani anapenda kucheza kitimu zaidi kwa kutoa pasi za haraka ila inabidi aongeze bidii kukuza kiwango chake. Gotze mwenye umri wa miaka 22 amefunga mabao mawili katika mechi saba za mashindano yote alizocheza za Bayern msimu huu.

KOUYATE NJE WIKI SITA.

KIUNGO wa klabu ya West Ham United, Cheikhou Kouyate atakaa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki sita baada ya kupata majeruhi ya nyonga. Kouyate aliumia wakati wa mchezo wa Jumamosi dhidi ya Liverpool ambapo walishinda ka mabao 3-1. Kiungo huyo huenda akakosa michezo mitano ya ligi kuu ya England iliyo mbele yao ukiwemo ule wa dhidi ya Manchester United utakaopigwa Septemba 27 mwaka huu. Kouyate alihamia West Ham akitokea Anderlect kwa kitita cha paundi milioni saba Julai na toka ametua hapo ameonyesha kiwango cha hali ya juu.

Monday, September 22, 2014

KABYLIE YALIMWA MIAKA MIWILI NA CAF.

KLABU ya JS Kabylie imefungiwa kushiriki katika michuano ya Afrika kwa miaka miwili kufuatia shambulio lililosababisha kifo cha mchezaji wa kimataifa wa Cameroon Albert Ebosse. Uamuzi umechukuliwa na Shirikisho la Soka barani Afrika-CAF katika kiakao chake kilichofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia. Kabylie ilimaliza katika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu nchini humo hivyo kuwapa nafasi ya kushiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani. Hatua hiyo ya CAF imekuja kufuatia Shirikisho la Soka la Algeria kuitaka Kabylie kucheza mechi zake za nmyumbani bila ya mashabiki katika uwanja huru msimu huu. Ebosse alifariki dunia hospitalini mwezi uliopita kutokana na majeraha ya kichwa yaliyosababishwa na kupigwa na kitu kizito na mashabiki wa klabu hiyo ambao walikasirishwa na kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa wapinzani wao USM Algers.


KOMBE LA DUNIA 2022 HALITAFANYIKA QATAR - ZWANZIGER.

MJUMBE wa kamati ya utendaji ya Shirikisho la Soka Duniani-FIFA, Theo Zwanziger amesema michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2022 haitaweza kufanyika Qatar kutokana na joto kali katika nchi hiyo ya Mashariki ya Kati. Zwanziger ambaye ni raia wa Ujerumani aliliambia jarida la michezo la Bild jana kuwa anadhani mwisho wa siku michuano ya Kombe la Dunia 2022 haitafanyika katika nchi hiyo. Mjumbe huypo aliendelea kudai kuwa watabibu wamesema hawatakubalia kuwajibika kama michuano hiyo itafanyika katika hali ya hatari kama hiyo. Ingawa Qatar wamesisitiza ambao ni matajiri wakubwa wa mafuta wamesisitiza kuwa wanaweza kuandaa michuano hiyo majira ya kiangazi kwa kutumia teknologia ya vipoza hewa katika viwanja vyake, sehemu za mazoezi na mahali watakapofikia mashabiki bado kumekuwa na wasiwasi mkubwa kuhusiana na afya za wachezaji na mashabiki watakaokuja kushuhudia michuano hiyo. Zwanziger amesema anajua wanaweza kuweka vipoza hewa viwanjani lakini Kombe la Dunia halichezwi viwanjani pekee kwani mashabiki kutoka duniani kote watakwenda na kusafiri katika hali hiyo ya joto jambo ambalo ni hatari kwa afya na maisha yao. Michuano ya mwaka 2022 imekuwa ikileta mjadala mkubwa huku rais wa FIFA Sepp Blatter akikiri kuwa walifanya makosa kuipa Qatar kuandaa michuano hiyo na kutaka kuangalia uwezekano wa kuamisha michuano hiyo ichezwe katika majira ya baridi.

BILIONEA LA SINGAPORE LANUNUA HISA KATIKA TIMU YA KINA GIGGS.

BILIONEA Peter Lim ambaye aliwahi kujaribu kuinunua Liverpool na akikaribia kuichukua Valencia, amenunua hisa za asilimia 50 za timu ya daraja la kwanza kanda ya kaskazini ya Salford City. Nyota wa zamani wa Manchester United Gary na Phil Neville, Ryan Giggs, Paul Scholes na Nicky Butt ambao walikubali kuinunua klabu hiyo Machi mwaka huu nao watamiliki hisa asimilia 50. Katika taarifa yao nyota hao wamedai kuwa uzoefu alionao Lim katika biashara hizo utawasaidia kwa kiasi kikubwa sana. Bilionea huyo raia wa Singapore mwenye umri wa miaka 61 anakadiriwa na jarida la Forbes kuwa na utajiri unaofikia kiasi cha paundi bilioni 1.5 lakini aliondoa zabuni ya paundi milioni 320 ili ainunue Liverpool mwaka 2010. Nyota hayo wamedai kuwa wamefahamiana na Lim kwa zaidi ya miaka 10 na wanategemea mambo ya kusisimua kwa Salford ambao wanaongoza ligi yao ambayo kwa Uingereza ni Ligi Daraja la Nane.

TAJIRI WA PSG AMPA UHAKIKA BLANC PAMOJA NA MATOKEO MABOVU.

RAIS wa klabu ya Paris Saint-Germain-PSG Nasser Al-Khelaifi amemuhakikishia meneja wa klabu hiyo kuwa kibarua chake hakipo hatarini pamoja na kuanza vibaya msimu wa ligi. PSG iling’ang’aniwa sare ya bao 1-1 nyumbani na Olympique Lyon mwishoni mwa wiki hii na kwasasa wanashika nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu wakiwa wameshinda mechi mbili pekee kati ya sita walizocheza. Huku pia wakiwa wametoa sare katika mchezo wao wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Ylaya dhidi ya Ajax Amsterdan, tetesi juu ya kibarua cha Blanc zikavuma kwa kasi lakini Al-Khelaifi amezima tetesi hizo kwa kusisitiza kuwa kocha huyo ataendelea kuinoa PSG mpaka mwishoni mwa msimu. Akihojiwa Al-Khelaifi amesema pamoja na kiwango kisichoridhisha walichoanza nacho lakini ana uhakika watafanya vizuri katika siku za mbele na kuonyesha imani kwa Blanc. Blanc mwenye amesema anajua siku zote matokeo mabaya lazima yalete mkanganyiko lakini ana matumani hali hiyo itakwisha baada ya kurejesha makali yao na kuanza kushinda mechi zao.

VITA YAPIGA HATUA MOJA KUELEKEA FAINALI YA LIGI YA MABINGWA AFRIKA.

KLABU ya AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo-DRC jana ilifanikiwa kuutumia vyema uwanja wake wa nyumbani baada ya kushinda mabao 2-1 dhidi ya CS Sfaxien ya Tunisia katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika. Mabao ya Vita katika mchezo huo uliochezwa katika Uwanja wa Tata Raphael jijini Kinshasa yalitupiwa kimiani na Firmin Ndombe Mubele na Heritier Luvumbu Nzinga huku lile la kufutia machozi la Sfaxien likifungwa na Ali Maaloul. Vita watakwenda katika mchezo wao wa marudiano wiki ijayo wakijua sare ya aina yoyote inaweza kuwapeleka fainali ambapo watakutakana na aidha Etente Setif ya Algeria au TP Mazembe ya DRC. Sfaxien ambao ni mabingwa wa Kombe la Shirikisho na Super Cup walionekana kuzimiliki vyema dakika 20 za mwisho katika mchezo huo lakini walishindwa kutafuta nafasi ya kusawazisha. Sasa timu hizo zinatarajiwa kukutana katika mchezo wa marudiano Sepetmba 27 ili kuamua atayekwenda fainali inayotarajiwa kuchezwa kwa mikondo miwili kati ya Octoba 25-26 na Novemba 1-2.

MCHEZAJI WA LIGI KUU UGANDA AFARIKI GHAFLA KUFUATIA BAO LA KUSAWAZISHA LA LAMPARD JANA.

MCHEZAJI wa soka nchini Uganda Fahad Musana ameanguka na kufariki muda mchache baada ya Frank Lampard kufunga bao kusawazisha katika mchezo wa Ligi Kuu nchini Uingereza kati ya Manchester City na Chelsea. Kifo cha Musana mwenye umri wa miaka 24 kimekuja kwa mshtuko hususani baada ya beki huyo kucheza mechi yote katika ya klabu yake ya Simba iliyoshinda bao 1-0 dhidi ya Entebe FC katika mchezo wa Ligi Kuu nchini Uganda uliofanyika katika Uwanja wa Nakivubo. Kwa mujibu wa kocha wa Simba Fred Kajoba, Musana pia alifanya mazoezi na timu siku ya jana asubuhi katika viwanja vya Bombo na hakuonyesha tatizo lolote. Shirikisho la Soka la Uganda-FUFA lilituma taarifa za kifo hicho cha ghafla jana usiku ambapo mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya Barracks iliyopo huko Bombo kwa ajili taratibu za mazishi. Shuhuda aliyekuwepo eneo ambalo Musana alikuwa akitazama mechi hiyo amesema mchezaji huyo alikuwa akifurahia mchezo huo mpaka ilipofikia hatua ya Lampard aliposawazisha ndipo alipoanguka ghafla ya kukimbizwa hospitali ya Jeshi ya Bombo. Inaarifiwa kuwa mbali na kupenda kucheza kamari, Musana alikuwa shabiki wa kutupwa wa Chelsea na alikuwa yuko tayari kufanya lolote kwa ajili ya timu hiyo. Mashabiki wa soka la Uingereza nchini Uganda wamekuwa wakipata matukio katika miaka ya karibuni ambapo mwaka jana mshabiki wa klabu ya Arsenal aliripotiwa kupoteza nyumba baada ya kuweka kamari kwamba timu hiyo ingeifunga Manchester United katika mchezo wa Ligi Kuu lakini matokeo yake wakafungwa bao 1-0.

BALOTELLI AZUA JAMBO TWITTER KUFUTIA KIPIGI CHA MAN UNITED.


POLISI nchini Uingereza wameanzisha uchunguzi kuhusu tukio ambalo mshambualiji wa klabu ya Liverpool na timu ya taifa ya Italia Mario Balotelli alitukanwa kutokana na rangi ya ngozi yake kupitia kwa mtandao wa kijamii wa Twitter. Polisi katika mji wa Merseyside wameanzisha uchunguzi kufuatia matusi hayo yaliyotokea baada ya nyota huyo kutuma ujumbe akicheka kichapo cha Manchester United walichpata kutoka kwa timu ndogo ya Leicester City jana. Balotelli aliandika ujumbe huo ambao ulisambazwa kwa zaidi ya 150,000 kwa mashabiki wake. Hata hivyo miongoni mwa wale waliouona ujumbe huo walimshambulia kwa kucheka kichapo hicho cha United na wengine kufikia hatua ya kumtukana kwa misingi ya rangi yake. Pamoja na Uraia wa Italia alionao, Balotelli mwenye umri wa miaka 24 ana asili ya Afrika. Polisi tayari wamefunga kurasa kadha zilizotuma ujumbe huo huku wakianza uchunguzi waliozimiliki ni kina nani na wanaishi wapi iliwakamatwe na kujibu mashataka ya ubaguzi wa rangi. Kundi linalopigania kumaliza ubaguzi wa rangi katika michezo Kick It Out lilisema kuwa baada ya kuarifiwa kuwepo kwa matusi yenye kumdhalilisha Balotelli, kundi hilo lilianzisha uchunguzi kwa ushirikiano na polisi wa mitandao ya kijamii.