Saturday, April 29, 2017

TOURE AINANGA MAN UNITED.

KIUNGO mahiri wa Manchester City, Yaya Toure amesema kwa jinsi Manchester United walivyoshangilia sare ya bila kufungana na City inaonyesha jinsi gani klabu hiyo ilivyopiga hatua toka alipojiunga nao. City walitawala mchezo huo kwa kwa asilimia 69 na kupiga mashuti 19 kulinganisha na matatu ya ya United lakini walishindwa kabisa kumfunga kipa David de Gea. Matokeo hayo yanaifanya City kuendelea kukaa juu ya mahasimu wao na kumaanisha United bado wako nje ya eneo la kufuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao. Lakini mashabiki wa United walionekana kufurahia kwa kiasi kikubwa sare hiyo mara mchezo ulipomalizika na Toure amesema imekuwa tofauti na wakati anajiunga na City mwaka 2010 wakati Sir Alex Ferguson akiwa anatawala Ligi Kuu. Akizungumza na wanahabari, Toure amesema kumekuwa na mabadiliko makubwa toka ametua hapo kwa kipindi cha nyuma United ndio walikuwa wakitawala hivyo kuona mashabiki wao wakishangilia sare inaonyesha jinsi gani walivyopiga hatua.

PIRES AMTAKA MBAPPE KWENDA ARSENAL.


NGULI wa zamani wa soka wa Arsenal, Robert Pires amedai kuwa chipukizi wa Monaco Kylian Mbappe ataweza kunufaika kwa kiasi kikubwa kama akijiunga na klabu hiyo na kuongeza anadhani nyota huyo atakwenda huko. Hata hivyo, Pires amesema bado ni mapema sana kumfananisha nyota huyo na mshambuliaji nyota wa zamani wa timu hiyo Thierry Henry. Mbappe mwenye umri wa miaka 18 anatajwa kama mmoja kati ya wachezaji bora kabisa wanaochipukia duniani kufuatia kiwango bora alichoonyesha kwa klabu ya Monaco iliyotinga nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Pires ambaye aliwahi kucheza na henry katika kikosi cha Arsene Wenger miaka ya 2000 anaamini Arsenal ndio sehemu sahihi kwa Mbappe kukua na kuimarika kama mchezaji.

SPURS KUHAMIA WEMBLEY MSIMU UJAO.

KLABU ya Tottenham Hotspurs, imethibitisha kuwa itautumia Uwanja wa Wembley kuanzia msimu wa 2017-2018 kama uwanja wake wa nyumbani wakati ujenzi wa uwanja wao mpya ukiendelea. Uwanja mpya wa klabu hiyo unatarajiwa kuingiza mashabiki wapatao 61,000 na unajengwa pembeni ya uwanja wao wa sasa wa White Hart Lane. Spurs imecheza mechi zake za Ligi ya Mabingwa Ulaya na Europa League katika Uwanja wa Wembley msimu huu lakini amefanikiwa kushinda mechi moja kati ya nne. Mwenyekiti wa klabu hiyo, Daniel Levy amesema wakati ni mzuri katika historia ya klabu hiyo, kwani wanakwenda Wembley kwa msimu mmoja halafu wanahamia katika moja ya viwanja bora kabisa duniani. Levy aliendelea kudai kuwa uwanja huo ambao pia utakuwa ukitumika kwa ajili ya mechi za Ligi ya Soka ya Marekani-NFL, utakuwa muhimu kwa maendeleo na mafanikio yao ya baadae. Uwanja huo mpya unatarajiwa kujengwa kwa kitita cha paundi milioni 750 lakini unatarajiwa kutengeneza ajira karibu 3,500 katika eneo hilo wakati utakapomalizika.

Friday, April 28, 2017

POGBA KUIKOSA SWANSEA CITY.

MENEJA wa Manchester United, Jose Mourinho amesema Paul Pogba anatarajiwa kukosa mchezo wa Ligi Kuu Jumapili hii dhidi ya Swansea City utakaofanyika Old Trafford, lakini anatarajiwa kurejea tayari kwa ajili ya mchezo wa mkondo wa kwanza wa nusu fainalia ya Europa League Alhamisi ijayo. Pogba alitolewa nje kabla ya kumalizika kwa mchezo kati ya United dhidi ya Burnley Jumapili iliyopita kutokana na kupata majeruhi ya msuli wa nyuma ya paja na kumfanya kukosa mchezo wa jana waliotoka sare ya bila kufungana na mahasimu wao wa jiji Manchester City. Na Mourinho sasa amethibitisha kuwa kiungo huyo wa kimataifa wa Ufaransa hatakuwepo katika mchezo huo dhidi ya Swansea mwishoni mwa wiki hii. Hata hivyo, Mourinho aliwaambia wanahabari kuwa Pogba atakuwepo katika mchezo dhidi ya Celta Vigo.

LOVREN APEWA MKATABA MREFU LIVERPOOL.

BEKI wa kati wa Liverpool, Dejan Lovren amesaini mkataba mpya wa muda mrefu na klabu hiyo ambao unamalizika 2021. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 27 alitua Anfield akitokea Southampton kwa kitita cha paundi milioni 20 mwaka 2014 na mkataba wake wa sasa ulikuwa unatarajiwa kumalizika mwakani. Beki huyo wa kimataifa wa Croatia alianza kwa kusuasua katika msimu wake wa kwanza lakini alifanikiwa kurejea kwenye kiwango chake na kuja kucheza mechi 105 akiwa na klabu hiyo huku akifunga mabao manne. Akizungumza na wanahabari kuhusiana na suala hilo, Lovren amesema anadhani ni mtu mwenye furaha zaidi duniani kwasasa. Lovren aliendelea kudai kuwa ilikuwa ni ndoto zake kubakia Liverpool kwa kipindi kirefu zaidi kwani anaipenda klabu hiyo. Lovren amecheza mechi 28 msimu huu na kufunga mabao mawili.

BAYERN YAMUONGEZA MKATABA THIAGO ALCANTARA.

KLABU ya Bayern Munich imetangaza kumuongeza mkataba mpya kiungo wa kimataifa wa Hispania, Thiago Alcantara. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 26 amekubali kusaini mkataba wa nyongeza ya miaka miwili ambao utamuweka Allianz Arena mpaka Juni mwaka 2021. Thiago alijiunga na Bayern akitokea Barcelona mwaka 2013 na kujiimarisha mpaka kuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha kwanza pamoja na kusumbuliwa na majeruhi ya mara kwa mara. Hata hivyo, msimu huu unaonekana kuwa mzuri kwake kwani ameshacheza mechi 39 za mashindano yote akifunga mabao nane na kusaidia mengine tisa. Mwenyekiti wa Bayern Karl-Heinz Rummenigge amesema Thiago ni mmoja kati ya wachezaji wazuri na anafurahi kuendelea kuwepo naye.

WENGER ASEMA BADO SANA KWA SPURS KUFIKIA HADHI YA ARSENAL.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema itawachukua zaidi ya miaka kadhaa kwa Tottenham Hotspurs kuendelea kupata mafanikio kabla ya kuweza kutajwa rasmi kwamba ndio watawala wa soka kaskazini mwa jiji la London. Kauli ya Wenger imekuja kufuatia mafanikio ambayo Spurs wameyapata msimu huu wakiwa wanashikilia nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu wakitofautiana alama nne na Chelsea. Ushindi kwa Spurs katika mchezo wao dhidi ya Arsenal utakaofanyika White Hart Lane Jumapili hii, utaihakikishia klabu hiyo kumaliza msimu wa ligi wakiwa juu ya Arsenal toka Wenger alipokuwa meneja mwaka 1996. Wakati huohuo, Wenger amesema Arsenal iliwahi kutaka kumsajili Dele Alli kabla ya kwenda Spurs. Wenger amesema maskauti wa Arsenal walikua wakimfuatilia toka akiwa kinda na Spurs walifanya vyema kumsajili kwani ni mchezaji aliyekamilika.

CONTE ADOKEZA KUREJEA SERIE A.

MENEJA wa Chelsea, Antonio Conte amedokeza kuwa angependa kupata nafasi ya kurejea ya Serie A siku zijazo. Kocha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Italia na klabu ya Juventus, alitua Stamford Bridge mwaka jana na kuongoza vyema Chelsea ambayo iko kwenye nafasi nzuri ya kutwaa taji la Ligi Kuu na Kombe la FA katika msimu wake wa kwanza. Hata hivyo, Conte amekuwa akihusishwa na tetesi za kurejea tena Italia mara kadhaa huku klabu ya Inter Milan ikitajwa kutaka kumnasa kocha huyo. Akiulizwa kuhusiana na suala hilo, Conte amesema siku zote moyo wake umekuwa Italia na amekuwa akifahamu kuwa iko siku atarejea tena Serie A. Chelsea kwasasa ndio vinara wa ligi wakitofautiana alama nne na Tottenham Hotspurs wanaoshika nafasi ya pili huku wakiwa tayari wamefika hatua ya fainali ya Kombe la FA na watacheza dhidi ya Arsenal.

CELTA VIGO YATISHIA KUISHITAKI MAN UNITED.


KLABU ya Celta Vigo imetishia kuishitaki Manchester United katika Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA kufuatia klabu hiyo kushindwa kuwapatia tiketi zao zote za mchezo wa mkondo wa nusu fainali ya Europa League utakaofanyika Old Trafford. Kwa mujibu wa kanuni za UEFA zinaeleza kuwa klabu mwenyeji inatakiwa kutoa asilimia ya tano ya sehemu ya uwanja kwa ajili ya mashabiki wa ugenini. Uwanja wa Old Trafford ndio uwanja mkubwa zaidi miongoni mwa klabu za Ligi Kuu ukiwa na uwezo wa kubeba mashabiki zaidi 75,000. Celta Vigo wamethibitisha kupokea tiketi 1,900 pekee kati ya 3,780 ambazo wanastahili kupatiwa kwa ajili ya mchezo huo utakaofanyika Mei 11 mwaka huu na juhudi za kujaribu kupatiwa ufafanuzi kuhusiana na hilo zimeshindikana. Msemaji wa Celta Vigo amesema kikao kilifanyika toka juzi kati ya pande zote mbili lakini hakuna chochote kilichotekelezwa mpaka sasa. Msemaji huyo aliendela kudai kuwa kama suala hilo lisipopatiwa ufumbuzi katika siku za karibuni ni wazi watalazimika kuiomba UEFA kuingilia kati.

Thursday, April 27, 2017

COMAN AJITIA KITANZI CHA MOJA KWA MOJA BAYERN.

KLABU ya Bayern Munich imetangaza kumsajili Kingsley Coman kwa mkataba wa moja kwa moja kutoka Juventus. Nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa amesaini mkataba wa mpaka Juni 2020 baada ya Bayern kukubali kulipa euro milioni 21 zilizokuwa zikihitajika. Mwenyekiti wa Bayern, Karl-Heinz Rummenigge amesema Coman ni mchezaji muhimu kwa ajili ya maendeleo ya baadae ya timu yao ndio maana wameamua kumsajili moja kwa moja. Coman alijiunga na Bayern kwa mkopo wa miaka miwili mwaka 2015 huku mabingwa hao wa Bundesliga wakiwa na nafasi ya kumsajili moja kwa moja kama wakimuhitaji. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 20, hivi karibuni alikuwa akihusishwa na tetesi za kuondoka Allianz Arena huku klabu za Ligi Kuu Chelsea na Manchester City zikitajwa kumuwania.

BEKI WA ZAMANI WA CITY AMPONDA GUARDIOLA.

BEKI wa zamani wa Manchester City, Martin Demichelis amesema msimu wa kwanza wa meneja Pep Guardiola katika klabu hiyo unaonyesha jinsi gani mtangulizi wake Manuel Pellegrini alivyodharauliwa. Hali inavyokwenda kwasasa inaonyesha Guardiola anaweza kumaliza msimu wake wa kwanza bila taji kwa mara ya kwanza toka aanze kibarua hicho. Akizungumza na wanahabari, Demichelis amesema ukiangalia timu ya City hivi leo utaona ni jinsi gani hakuna kinachokuja kirahisi hata kwa kocha bora. Beki huyo aliendelea kudai kuwa kadri muda unavyokwenda kila mtu ataona na kuthamini kazi kubwa iliyofanywa na Pellegrini. Pellegrini alishinda taji la Ligi Kuu na Kombe la Ligi katika msimu wake wa kwanza akiwa na klabu hiyo baada ya kujiunga nao akitokea Malaga Juni mwaka 2013. Meneja huyo pia alimaliza nyuma ya Chelsea kwenye mwaka wake wa pili uliofuatia na kuiongoza City katika hatua ya nusu fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kabla ya mkataba wake kumalizika kiangazi mwaka jana.

SAKHO AIWEKA NJIA PANDA PALACE.

MENEJA wa Crystal Palace, Sam Allardyce ana matumaini Mamadou Sakho hajapata majeraha makubwa kwenye goti lake wakati walipofungwa nyumbani na Tottenham Hotspurs jana. Sakho alilazimika kutolewa nje baada ya kuumia kwa kukwatuliwa na mshambuliaji Spurs Harry Kane na beki huyo ambaye yuko kwa mkopo Palace amelazimika kufanyiwa vipimo zaidi kugundua ukubwa wa tatizo lake. Kutokana na mkataba wa mkopo wa Sakho kutoka Liverpool kukaribia kumalizika mwishoni mwa msimu huu, nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa anaweza kuwa amecheza mechi yake ya mwisho Palace lakini Allardyce ana matumaini majeruhi hayo hayakuwa makubwa sana. Akizungumza na wanahabari, Allardyce amesema hafahamu ukubwa wa tatizo la Sakho lakini ana matumaini hayatakuwa makubwa sana mpaka kumfanya kukaa nje ya uwanja kwa msimu wote uliosalia.

KOSCIELNY HATIHATI KUWEPO DHIDI YA SPURS.

KLABU ya Arsenal inaweza kumkosa beki wake mahiri Laurent Koscielny katika mchezo wao wa Jumapili dhidi ya mahasimu wao wa London ya Kaskazini Tottenham Hotspurs Jumapili hii. Hatua hiyo inakuja kufuatia beki huyo kuumia goti katika mchezo wao jana walioshinda bao 1-0 dhidi ya mabingwa watetezi Leicester City. Akizungumza na wanahabari baada ya mchezo huo, Wenger amesema Koscielny amepata matatizo ya goti lakini hajui ameumia kwa kiasi gani mpaka atakapofanyiwa vipimo. Huku beki mwingine Shkodran Mustafi pia akiwa katika hatihati kutokana na majeruhi ya msuli, kukosekana kwa Koscielny kunaweza kuiathiri Arsenal kwa kiasi kikubwa haswa wakati huu ambao wanafukuzia nafasi nne za juu ili wafuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao. Arsenal kwasasa wako nafasi ya sita katika msimamo wa ligi, na wanakwenda kupambana na Spurs ambao hawajafungwa mchezo wowote katika uwanja wao wa nyumbani.

SHABIKI WA SPURS APIGWA NA MASHABIKI WENZAKE.

SHABIKI mmoja wa Tottenham Hotspurs alijikuta matatani na kuumizwa vibaya baada ya kushambuliwa na mashabiki wenzake wa timu hiyo ambayo walidhani ni shabiki wa Chelsea. Shabiki huyo, Michael Voller alikuta katika mkasa huo kufuatia mchezo wa nusu fainali kati ya klabu hizo mbili kutoka jiji la London uliofanyika katika Uwanja wa Wembley Jumamosi iliyopita. Tukio hilo linadaiwa kutokea nje ya mgahawa wa Moore Spice ambapo shabiki huyo alionekana na mashabiki wa Spurs akienda upande tofauti ndipo sakata hilo lilipomkuta. Voller alipigwa na kuumizwa vibaya kwa kuvunjwa taya pamoja na kuvimba uso kwa kipigo hicho.

Arsenal vs Leicester 1-0 Goals & Highlights 2017 HD

Deportivo Vs Real Madrid 2-6 - All Goals & Highlights - Resumen y Goles ...

Bayern Munich vs Borussia Dortmund 2-3 All Goals & Highlights DFB Pokal ...

Barcelona vs Osasuna 7-1 - All Goals & Extended Highlights - La Liga 26/...

Wednesday, April 26, 2017

RATIBA YA MAKUNDI MICHUANO YA LIGI YA MABINGWA AFRIKA.



RATIBA YA MAKUNDI MICHUANO YA KOMBE LA SHIRIKISHO.



MOURINHO KUENDELEA KUWAPA "MAKAVU LIVE" WACHEZAJI WAKE.

MENEJA wa Manchester United, Jose Mourinho amesisitiza kuwa hajali kama wachezaji wa kikosi chake hawapendi kukosolewa hadharani na kuongeza anadhani msimu huu unaweza kuwa wa kwanza wa miaka ya furaha Old Trafford. Henrikh Mkhitaryan, Luke Shaw, Anthony Martial na Chris Smalling wote wamewahi kukosolewa na Mourinho hadharani msimu huu. Lakini meneja huyo amesisitiza kuwa mbinu yake hiyo ni kwa ajili ya timu na kuwataka wachezaji ambao wanaonekana kushuka viwango vya kwa mara nyingine kufuata mfano unaoonyeshwa na Marcus Rashford. Akizungumza na Sky Sports kuhusiana na suala hilo, Mourinho amesema yeye hajali kwani anajaribu kuwa yeye kwa kuongeza kile anachoona sio sahihi. Mourinho aliendelea kudai kuwa kama mchezaji anacheza kwa kiwango chake bora hakuna cha ziada atakachoomba kutoka kwake.

FA YAMSTAAFISHA MAPEMA MTUKUTU BURTON.

KIUNGO wa Burnley, Joey Burton amesema kuwa atalazimika kustaafu soka mapema baada ya kulimwa adhabu ya kufungiwa miezi 18 na Chama cha Soka cha Uingereza-FA kwa makosa ya kamari. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 34, ambaye pia ametozwa faini ya paundi 30,000, anatuhumiwa na FA kucheza kamari 1,260 katika kipindi cha miaka 10 kati ya Machi 2006 na Mei 2016. Barton ambaye amethibitisha nia yake ya kukata rufani kupinga ukubwa wa adhabu hiyo, amekubali kuwa alivunja sheria za FA lakini amedai chama hicho cha soka kimetoa adhabu kali mno na hawakuzingatia kuathirika kwake na kamari ambapo alipeleka mpaka taarifa za kupata msaada wa kitabibu. Katika taarifa yake aliyotoa kwenye tovuti yake, Burton amesema amesikitishw ana adhabu hiyo kali aliyopewa, jambo ambalo litamlazimu kustaafu mapema kucheza soka.

UWANJA WA AMSTERDAM ARENA KUPEWA JINA LA CRUYFF.

Yohan Cruyff
UWANJA wa Amsterdam Arena unatarajiwa kubadilishwa na kupewa jina la nguli wa zamani wa Uholanzi Johan Cruyff. Cruyff mmoja kati ya wanasoka bora kabisa na mwenye ushawishi zaidi na kocha aliyekuwa na maono, alifariki dunia zaidi ya mwaka mmoja uliopita baada ya kupambana miaka mitano na maradhi ya saratani ya mapafu, akiwa na umri wa miaka 68. Katika taarifa ya maafisa wa uwanja huyo iliyotumwa katika tovuti yao, imedai kuwa wamefikia uamuzi huo kwa kuupa jina la Johan Cruyff uwanja huo kutokana na mchango mkubwa aliotoa akiwa mchezaji na kocha. 
Mtoto wake wa kiume, Jordi amesema familia yao imefarijika kwa utambuzi huo ambao unatarajiwa kufanyika ndani ya kipindi cha miezi sita ijayo. Amsterdam Arena wenye uwezo wa kubeba mashabiki 54,000 ulijengwa mwaka 1996 na unamilikiwa kwa ushirikiano na klabu ya Ajax, halmashauri ya mji wa Amsterdam na kampuni inayosimamia uwanja huo.

RONALDO KUIKOSA DEPORTIVO.

MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo ameachwa katika kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya mchezo wao wa La Liga dhidi ya Deportivo La Coruna. Meneja wa Madrid, Zinedine Zidane ametaja kikosi cha wachezaji 19 kwa ajili ya mchezo huo huku Gareth Bale pia akiondolewa kutokana na majeruhi. Bale alipata majeruhi mwishoni mwa wiki iliyopita na anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki tatu. Huku Ronaldo na Bale wakikosekana, kuna uwezekano mkubwa kwa Zidane kuwatumia Karim benzema na Alvaro Morata katika safu ya ushambuliaji ya timu hiyo. Beki Sergio Ramos naye anatarajia kukosa mchezo huo utakaochezwa baadae leo akitumikia adhabu ya kukosa mechi moja baada ya kupewa kadi nyekundu katika mchezo wa El Clasico dhidi ya mahasimu wao Barcelona Jumapili iliyopita.

ORODHA YA WACHEZA SOKA WANAOLIPWA ZAIDI MAREKANI.

Kaka (Bra), Orlando City, £5.6m

Giovani dos Santos (Mex), LA Galaxy, £4.3m

Sebastian Giovinco (Ita), Toronto, £5.5m

Bastian Schweinsteiger (Ger), Chicago Fire, £4.2m


Michael Bradley (US), Toronto, £5.1m

Jozy Altidore (US), Toronto, £3.8m


Andrea Pirlo (Ita), New York City, £4.6m

Clint Dempsey (US), Seattle Sounders, £3m


David Villa (Spa), New York City, £4.4m

Diego Valeri (Arg), Portland Timbers, £2m

Tuesday, April 25, 2017

BALE KUIKOSA ATLETICO MADRID.

KLABU ya Real Madrid imethibitisha kuwa winga wao Gareth Bale atakosa mechi za nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Atletico Madrid kutokana na majeruhi yanayomsumbua. Klabu hiyo imedai kuwa nyota huyo anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa kipindi kisichopungua wiki tatu hivyo wanamtegemea kurejea uwanjani katikati ya mwezi Mei. Taarifa hiyo inamaanisha kuwa Bale mwenye umri wa miaka 27 atakosa mechi za mikondo yote miwili za Madrid hidi ya majirani zao Atletico. Katika taarifa ya klabu hiyo iliyotolewa kupitia tovuti yake imedai kuwa kufuatia vipimo alivyofanyiwa Bale amegundulika kuwa alipata majeruhi ya msuli wa kigimbi na maendeleo yake yatakuwa yakifuatiliwa kadri siku zinavyokwenda. Mbali na mechi za Ligi ya Mabingwa Ulaya, Bale pia atakosa mechi za La Liga ambazo Madrid watacheza Valencia, Granada, Sevilla na Malaga.

KIPIGO CHA BARCELONA CHAMCHANGANYA RONALDO, AMPIGA "BITI" MPENZI WAKE.

MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo amemuagiza mpenzi wake kuacha kumuandalia sherehe kufuatia kipigo cha mabao 3-2 walichopata kutoka kwa mahasimu wao wa La Liga Barcelona. Ronaldo angeweza kuwa na siku nzuri mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Madrid walipoiklaribisha Barcelona katika El Clasico, hata hivyo mambo hayakuwa mazuri kama yalivyotegemewa baada ya Lionel Messi kuibuka nyota wakati Barcelona wakiondoka na ushindi huo mnono. Badala ya kufurahia ushindi wa Madrid katika sherehe iliyoandaliwa na mpenzi wake Georgina Rodriguez, Ronaldo alitoka uwanjani akiwa kichwa chini baada ya kipigo hicho. Taarifa kutoka nchini Ureno zinadai kuwa, Rodriguez alikuwa ameandaa sherehe ya baada ya mechi nyumbani kwa Ronaldo jijini Madrid lakini shughuli hiyo ilibidi isitishwe kufuatia matokeo ya mwisho. Mbali na kusitisha sherehe hiyo fupi lakini Ronaldo mwenyewe anadaiwa kwenda mbali zaidi kwa kumkataza mpenzi wake huyo kumuandalia sherehe kama hizo siku za usoni. Wawili hao wamekuwa pamoja kwa miezi saba sasa, na walionekana pamoja katika sherehe za utoaji tuzo za FIFA Januari mwaka huu sambamba na mtoto wa Ronaldo, Crstiano Jr.

BARCELONA YAWEKA WAZI KUWA HAWANA MPANGO WA KUMUUZA NEYMAR.

KATIBU wa ufundi wa Barcelona, Roberto Fernandez ameondoa uwezekano wa kumuuza nyota wao Neymar huku apuuzia tetesi kuwa wana mpango wa kumsajili nyota wa Juventus Paul Dybala. Neymar mwenye umri wa miaka 25 amekuwa akihusishwa na tetesi kwa kipindi kirefu za kwenda kwa wakongwe wa Ligi Kuu Manchester United. Lakini Fernandez amesema hakuna nafasi kwa Neymar ambaye ana mkataba unaomalizika katikati ya 2021, kuondoka Camp Nou. Akizungumza na wanahabari kuhusiana na suala hilo, Fernandez amesema Neymar hauziki na kuongeza kuwa klabu zinazomuwani zinajisumbua kwasasa. Akizungumzia suala la Dybala, Fernandez amesema ni mchezaji mzuri lakini tayari Barcelona ina safu bora kabisa ya ushambuliaji hivyo hadhani kama uhamisho huo utawezekana.

MARTIN ATKINSON KUCHEZESHA MANCHESTER DERBY.

LIGI Kuu ya Uingereza imethibitisha mwamuzi Martin Atkinson ndio aliyechaguliwa kuchezesha mchezo wa Manchester derdy kesho kutwa. Atkinson mwenye umri wa miaka 46 anatarajiwa kuwa mwamuzi kiongozi wakati Manchester United itakapowafuata majirani zao Manchester City katika Uwanja wa Etihad.  Mwamuzi huyo kutoka West Yorkshire ameshachezesha mechi tatu za United msimu huu ikiwemo waliyofungwa mabao 4-0 na Chelsea Octoba 23 na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Sunderland Desemba 26 pamoja na ile ya Kombe la FA dhidi ya Blackburn Rovers Februari 19. Kwa upande wa City, Atkinson ameshachezesha mechi mbili ikiwemo ile waliyoshinda mabao 2-1 dhidi ya Arsenal Desemba 18 pamoja na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Sunderland Machi 5 mwaka huu. Atkinson pia aliwahi kuchezesha derby ambayo United walishinda katika msimu wa 2009-2010.

CONTE AZING'ONG'A KLABU ZA MANCHESTER.

MENEJA wa Chelsea, Antonio Conte amesema kutumia fedha nyingi kwa ajili ya wachezaji hakukupi uhakika wa mafanikio katika Ligi Kuu ya Uingereza. Meneja huyo raia wa Italia ametolea mfano klabu za Manchester baada ya Manchester United kutumia kiasi kilichovunja rekodi cha paundi milioni 89 kwa ajili ya kiungo Paul Pogba na Manchester City wakitumia paundi milioni 47 kwa beki John Stones. Chelsea wako kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama nne dhidi ya Tottenham Hotspurs wanaoshika nafasi pili huku pia wakitofautiana alama 11 na City na 12 kwa United zikiwa zimebaki mechi sita ligi kumalizika. Akizungumza na wanahabari, Conte amesema ni muhimu kuelewa kuwa sio mara zote wanaotumia fedha nyingi kwenye usajili hushinda. Meneja huyo aliendelea kudai kuwa msimu huu sio pekee klabu za Manchester kutumia fedha nyingi katika usajili, lakini mafanikio hayategemei fedha pekee.

WAKALA WA GRIEZMANN ATHIBITISHA NIA YA MAN UNITED KUMUWINDA NYOTA HUYO.

WAKALA wa mshambuliaji wa Atletico Madrid, Antoine Griezmann amesema Manchester United wameonyesha nia ya kumsajili nyota huyo. United ambao wanashikilia nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu, wamekuwa wakifunga mabao kadhaa dhidi ya timu zinazoshikilia nafasi sita za juu katika msimamo na bado wanataka kuongeza nguvu katika safu ya ushambuliaji kwa kumsajili Griezmann ambaye ameifungia Atletico mabao 25 msimu huu. Wakala huyo, Eric Olhats amesema kwasasa wako katika mpango wa kutafuta taarifa kutoka katika klabu ambazo zinataka kumsajili mteja wake huyo. Olhats aliendelea kudai kuwa kitenzi katika mkataba wa Griezmann ni euro milioni 100 hivyo kuna timu chache zilizoonyesha nia ikiwemo United, Manchester City, Chelsea, Barcelona na Real Madrid. Hata hivyo, Olhats amesema United ndio wamekuwa wa kwanza kuwafuata kuhusiana na suala hilo mpaka sasa.

WENGER ASISITIZA GIROUD HAENDI POPOTE.

MENEJA wa Arsenal, Arsene Wenger amepuuzia tetesi kuwa nyota wa kimataifa wa Ufaransa Olivier Giroud anaweza kuondoka katika klabu hiyo na kwenda Olympique Marseille mwishoni mwa msimu huu. Taarifa kutoka nchini Ufaransa zimedai kuwa Rudi Garcia alikuwa anataka kumrejesha Giroud nchini humo na walikuwa wamejipanga kutuma ofa Arsenal. Hata hivyo, Wenger amesisitiza kuwa mpaka sasa hajapata taarifa zozote kutoka katika klabu hiyo kuhusiana na suala hilo. Akizungumza na wanahabari kuelekea mchezo wa kesho dhidi ya Leicester City, Wenger amesema bado hajafuatwa na Marseille kuhusiana na suala hilo na kuongeza kuwa bado wanataka kuendelea kubakia na Giroud. Giroud alijiunga na Arsenal akitokea Montpellier mwaka 2012 na toka wakati huo ameshacheza mechi zaidi ya 200 na mkataba wake unatarajiwa kumalizika Juni mwaka 2019.

Friday, April 21, 2017

JESUS AREJEA KUIPA NGUVU MAN CITY.

MSHAMBULIAJI wa Manchester City, Gabriel Jesus anaweza kuanza katika mchezo wa nusu fainali ya michuano ya Kombe la FA dhidi ya Arsenal Jumapili hii. Jesus amekuwa nje ya uwanja toka alipovunjika mfupa wa mguu katika mchezo wa dhidi ya Bournemouth Februari 13 mwaka huu. Nyota huyo wa kimataifa wa Brazil alitua kwa kishindo City na kupewa nafasi ya kuanza badala ya Sergio Aguero na kufanikiw akufunga mabao matatu kwenye mechi nne alizocheza. Mapema wiki hii Jesus alirejea mazoezini na meneja Pep Guardiola amesema anaweza kumjumuisha katika kikosi chake kwa ajili ya mchezo wao huo wa Jumapili katika Uwanja wa Wembley.

HAJI MANARA KITANZINI TFF.

BAADA ya kutoa kauli zisizo nzuri kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) na kuitupia shutuma mbalimbali hatimaye kwa mujibu wa Katiba ya Shirikisho hilo limefanya maamuzi ya kumfikisha Msemaji wa Simba Hajji Manara mbele ya kamati ya maadili. TFF imeweka wazi kuwa kila mwanafamilia wa mpira wa miguu Tanzania analazimika kuheshimu na kufuata kanuni za maadili za shirikisho kama zilivyoainishwa kwenye kanuni zake mbali mbali. Katika Mkutano wa klabu ya Simba uliofanyika siku chache zilizopita ukiongozwa na msemaji wao Manara ulitoa shutma kwa TFF kuwa hauwatendei haki na una mpango wa kudhulumu haki yao na hata hivyo miaka minne ya Rais Jamal Malinzi umedhamiria kuhakikisha Simba hawachukui ubingwa. Manara alizidi kutoa shutuma kwa Rais wa TFF na kusema kuwa wanajua mahusiano yake na mwamuzi Jonesia Rukyaa ambaye alikuwepo katika kutoa ushahidi mbele ya kamati ya Katiba,Hadhi na wachezaji wakati wa kupitia hukumu ya saa 72 iliyotoa maamuzi ya Simba kupewa alama 3 na goli 3 dhidi ya Kagera baada ya kumchezesha Mohamed Fakhi akiwa na kadi za njano. Ili kutunza heshima ya mpira wa miguu Tanzania, wanafamilia wa mchezo huo katika kutimiza masharti ya kanuni za maadili za TFF, hawana budi kuheshimu na kufuata taratibu zote hizo ndani na nje ya uwanja. Taswira njema ya shirikisho inajenga imani ya wadau wakiwamo serikali, mashirika mbalimbali ya umma na binafsi, vyombo vya habari, vyama vya mpira vya kimataifa, NGO’s na watu binafsi kwa taasisi (TFF). Kinyume chake ni kulibomoa shirikisho. Dhima ya uongozi wa TFF ni pamoja na kulinda na kutunza heshima hii. Hivyo vitendo vyovyote vyenye viashiria vya uvunjaji wa maadili havitavumiliwa, na vikitokea hatua zitachukulia. Na kwa muktadha huu Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania, limemfungulia mashtaka ya kinidhamu Msemaji wa Simba Bw. Hajji Manara kwenye Kamati ya Maadili. Na leo hii Aprili 21, 2017 atapewa mashtaka yake na kujulishwa lini na wapi yatasikilizwa. TFF inaendelea kutoa rai kwa wadau wa mpira kuwa pamoja ni kwamba ni haki yao kushauri, kupendekeza, kukosoa lakini yote haya yafanyike kwa staha ili kutunza heshima ya mpira wetu.

MMOJA ASHITAKIWA KWA MILIPUKO BASI LA DORTMUND.

POLISI nchini Ujerumani wamemshitaki mtu mmoja kwa kuhusika na shambulio katika basi la timu ya Borussia Dortmund. Waendesha mashitaka wamedai kuwa mtu huyo ambaye ni mfanyabishara alifanya tukio hilo kwa lengo la kujipatia fedha kama bei za hisa ya timu hiyo zingeshuka. Mtu aliyejulikana kwa jina la Sergej W, mwenye umri wa miaka 18 alikuwa amteja katika hoteli ambayo timu hiyo ilifikia ambapo chumba chake kilikuwa kinetizamana na mtaa ambao milipuko ilitokea. Watu wawili walihitaji msaada wa kimatibabu baada ya mabomu matatu kulipuka karibu na basi la timu hiyo. Beki wa kimataifa wa Hispania, Marc Barta aliumia kiganja cha mkono na kufanyiwa upasuaji na afisa mmoja wa polisi naye alitibiwa kufuatia kupata mshituko.

BARCELONA KUIKATIA RUFANI ADHABU YA NEYMAR.


KLABU ya Barcelona inatarajiwa kwenda kukata rufani katika Mahakama Maalumu ya Michezo nchini Hispania-TAD, katika jitihada zao za kujaribu kupunguza adhabu ya kufungiwa mechi tatu aliyopea Neymar kuelekea mchezo wao wa Clasico. Nyota huyo wa kimataifa wa Brazil alitolewa nje kwa kupewa kadi mbili za njano katika mchezo wa dhidi ya Malaga, kabla ya kuongezewa adhabu ya mechi tatu na Shirikisho la Soka la nchi hiyo. Kawaida kadi mbili za njano alizopewa alitakiwa kukosa mechi moja lakini kutokana na na kumshambulia mwamuzi kwa maneno wakati alipopewa kadi nyekundu ndio kulikofanya aongezewe adhabu. Baada ya kukata rufani ya kwanza na kukataliwa Barcelona sasa wameamua kusogea mbele zaidi kwa kwenda TAD ili kujaribu kumpigania nyota wao huyo awepo katika mchezo huo wa Clasico dhidi ya mahasimu wao Real Madrid Jumapili hii.

RATIBA ZA NUSU FAINALI CHAMPIONS LEAGUE NA EUROPA LEAGUE.

RATIBA ya nusu fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya imepangwa baada ya kukamilika kwa hatua ya robo fainali na kupatikana timu nne zilizosonga mbele. Katika ratiba hiyo Real Madrid na majirani zao Atletico Madrid wamepangwa kucheza pamoja huku mchezo wa mkondo wa kwanza ukitarajiwa kuchezwa katika Uwanja wa Santiago Bernabeu. Mechi nyingine katika ratiba hiyo itawakutanisha AS Monaco ambao wataanzia nyumbani kupambana na mabingwa wa Serie A Juventus. Mechi za mkondo wa kwanza zinatarajiwa kuchezwa Mei 2 na 3 huku zile za marudiano zikitarajiwa kuchezwa Mei 9 na 10.
 Pia Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA limepanga ratiba ya nusu fainali ya michuano ya Europa League ambapo Manchester United wataanzia ugenini kupambana na Celta Vigo huku Ajax Amsterdam wao wakipangwa kucheza na Olympique Lyon ya Ufaransa.

SABA WAFARIKI WAKIANGALIA MPIRA WA MANCHESTER.

WATU saba wamefariki na wengine wengi kujeruhiwa baada ya kupigwa shoti ya umeme wakati wakitazama mechi kati ya Manchester United ya Uingereza na Anderlecht ya Ubelgiji nchini Nigeria. Mashabiki wa soka walikuwa wamekusanyika kwenye kituo cha kutazama mechi kupitia runinga katika mji wa Calabar kusini mwa nchi hiyo mkasa ulipotokea. Manchester United walishinda 2-1 kwenye mechi hiyo ya hatua ya robo fainali ya Europa League. Polisi nchini Nigeria wamesema watu saba walifariki na wengine 10 wakajeruhiwa na wamelazwa hospitalini. Mwandishi mmoja nchini humo ameambia BBC kwamba kisa hicho kilitokea baada ya waya wa umeme kuangukia jumba.

BEKI WA ZAMANI WA UINGEREZA AFARIKI.

BEKI wa kimataifa wa Uingereza na klabu ya Aston Villa, Ugo Ehiogu amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 44 baada ya kupata matatizo ya mshituko ya moyo wakati akiwa eneo la mazoezi la klabu ya Tottenham Hotspurs. Katika taarifa yake, Spurs wamedai kuwa Ehiogu alifariki dunia akiwa hospitali mapema leo. Ehiogu ambaye alikuwa kocha wa kikosi cha vijana chini ya umri wa miaka 23 cha Spurs, aliichezea Uingereza mechi nne. Ehiogu aliwahi kuichezea Villa zaidi ya mechi 200 kati ya mwaka 1991 na 200 na baadae kuja kuitumikia Middlesbrough kwa miaka saba.

Wednesday, April 19, 2017

ARSENAL YATHIBITISHA WILSHERE AMEVUNJIKA MGUU.

KLABU ya Arsenal imethibitisha kuwa Jack Wilshere ambaye yupo kwa mkopo Bournemouth, amevunjika mguu na anatarajiwa kukosa msimu wote uliosalia. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 25 aligongana na Harry Kane katika kipindi cha pili wakati Bournemouth walitandikwa mabao 4-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu na Tottenham Hotspurs Jumamosi iliyopita. Vipimo vimeonyesha kuwa Wilshere alivunjika mguu wake kama ilivyokuwa msimu uliopita na kusababisha kipindi kirefu kuwa nje ya uwanja. Katika taarifa yake, Arsenal walithibitisha taarifa hizo huku wakiongeza kuwa hataweza kurejea uwanjani mpaka msimu ujao.

MOURINHO AMUONYA MARTIAL.

MENEJA wa Manchester United, Jose Mourinho amemwambia Anthony Martial kuwa anatakiwa kufanya anachotaka kama anataka kufanikiwa kwenye klabu hiyo. Martial hakujumuishwa katika kikosi cha United kilichopambana na Chelsea mwishoni mwa wiki iliyopita ambapo kikosi cha Mourinho kiliibuka na ushindi mnono wa mabao 2-0 dhidi ya vinara hao wa Ligi Kuu ya Uingereza. Nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa amefanikiwa kucheza kwa dakika 90 mechi tatu pekee za ligi msimu huu na Mourinho sasa amemuonya kuwa anatakiwa kufuata maelekezo yake kama anataka kufanikiwa. Akizungumza na wanahabari, Mourinho amesema wamekuwa pamoja kwa miezi 10 sasa hivyo anawafahamu wachezaji vizuri zaidi hivi sasa na wachezaji nao wanapaswa kumuelewa vyema sasa. Mourinho aliendelea kudai kuwa wachezaji wanapswa kufahamu ni kitu gani anataka na wao kufuata utaratibu huo. United inakabiliwa na mchezo dhidi ya Anderlecht kesho ukiwa ni mchezo wao wa mkondo wa pili wa robo fainali ya Europa League baada ya kutoka sare ya bao 1-1 kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza huko Ubelgiji.

TERRY AGOMA KUSTAAFU PAMOJA NA KUONDOKA CHELSEA.

BEKI wa Chelsea, John Terry amesisitiza hana mpango wa kustaafu wakati atakapokamilisha uamuzi wake mgumu kuwahi kufanya maishani kwa kuondoka kwenye klabu hiyo mwishoni mwa msimu huu. Terry alibainisha mapema wiki hii kuwa ataondoka rasmi Chelsea baada ya kupita miaka 19 akiitumikia pindi msimu utakapomalizika. Uamuzi wa beki huyo mkongwe mwenye umri wa miaka 36 uliibua hisia kuwa anaweza kuamua kutundika daruga zake baada ya kucheza mechi tano pekee kwa Chelsea msimu huu. Hata hivyo, Terry alifafanua katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram kuwa uamuzi wa kuondoka Chelsea ulikuwa kufanya kwenye maisha yake lakini anadhani ulikuwa wakati sahihi kufanya hivyo. Kikubwa kilichomfanya kuondoka Chelsea ni uhakika wa kupata nafasi ya kucheza mara kwa mara kwani bado anadhani anataka kuendelea kucheza soka. Terry ameshinda mataji 14 akiwa na Chelsea huku akicheza mechi 713 toka alipojiunga kwa mara ya kwanza mara 1998.

RONALDO AWATAKA MASHABIKI WA MADRID KUMPA HESHIMA YAKE.

MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo amewataka mashabiki kumpa heshima zaidi baada ya kufunga hat-trick katika ushindi wa mabao 4-2 waliopata kwenye mchezo wao wa marudiano dhidi ya Bayern Munich jana. Katika wiki za karibuni Ronaldo alikuwa hafungi mabao kama ilivyozoeleka na kupeleka baadhi ya mashabiki kumzomea kwa kudhani kuwa hajitumi ipasavyo. Lakini jana mashabiki wote walikuwa wakishangilia jina lake mwishoni baada ya kuisaidia Madrid kupata ushindi huo ambao umewapeleka katika hatua ya nusu fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa jumla ya mabao 6-3. Akizungumza na wanahabari Ronaldo amesema hajawazi kuwaambia mashabiki wanyamaze, alichotaka kuwaambia yeye ni kuacha kuzomea kwasababu siku zote amekuwa akijituma kwa bidii ili kuisaidia timu.

NEUER KUKOSA MSIMU ULIOSALIA.

KIPA wa Bayern Munich, Manuel Neuer anatarajiwa kukosa msimu wote uliosailia baada ya kuumia mguu wake wa kushoto katika kipigo cha mabao 4-2 walichopata kutoka kwa Real Madrid jana. Nahodha huyo wa kimataifa wa Ujerumani alipata majeruhi hayo wakati akijaribu bila mafanikio kumzuia Ronaldo kufunga bao la tatu kwenye dakika ya 109 katika Uwanja wa Santiago Bernabeu. Ofisa mkuu wa Bayern , Karl-Heinz Rummenigge alithibitisha taarifa hizo mara baada ya mchezo huo uliokwamisha ndoto zao za kwenda nusu fainali. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 31 anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa wiki nane hivyo kuzusha hofu pia ya kuweza kuikosa michuano ya Kombe la Shirikisho inayotarajiwa kuanza Juni 17.

Monday, April 17, 2017

CHIELLINI AWAONYA WACHEZAJI WENZAKE KUHUSU MSN.

BEKI wa Juventus, Giorgio Chiellini ameonya kuwa nyota wa Barcelona Lionel Messi, Luis Suarez na Neymar ni kama papa ambao wanaweza kuwamaliza. Vigogo hao wa Turin wanaongoza kwa mabao 3-0 ushindi waliopata kwenye mchezo wao wa mkondo wa kwanza wa robo fainali wakati Paulo Dybala alipong’aa kwenye mchezo huo huku safu ya ushambuliaji wa Barcelona inayojuliakana kama MSN ikishindwa kutamba kabisa. Messi, Suarez na Neymar wote walifunga wakati Barcelona walipoweka historia katika hatua ya 16 bora baada ya kutoka nyuma wakiwa wamefungwa mabao 4-0 na Paris Saint-Germain na kuja kushinda mchezo wa marudiano Camp Nou kwa mabao 6-1. Chielini amewaonyesha wachezaji wenzake kufanya kila wawezalo kuhakikisha suala hilo halijirudii kwenye mchezo wao wa Jumatano. Akizungumza na wanahabari, Chiellini amesema kama wakifanikiwa kuwaweka nyota wa Barcelona mbali na eneo lao la hatari ni wazi wanaweza kuondoka na chochote kwenye mchezo huo. Chiellini aliendelea kudai kuwa Barcelona ina safu bora ya ushambuliaji duniani na kama wakinusa wakiona kuna uwoga fulani haraka wanaweza kukuadhibu kama papa anavyonusa harufu ya damu.

BALE KUIKOSA BAYERN.

MENEJA wa Real Madrid, Zinedine Zidane amethibitisha kuwa watamkosa winga wao Gareth Bale kwa ajili ya mchezo wa mkondo wa pili wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa kesho dhidi ya Bayern Munich. Bale alitolewa katika kipindi cha pili wiki iliyopita kwenye ushindi wa mabao 2-1 waliopata dhidi ya mabingwa hao wa Bundesliga kule Allianz Arena huku pia akikaa nje kwenye mchezo dhidi ya Sporting Gijon walioshinda mabao 3-2 Jumamosi iliyopita. Nyota huyo wa kimataifa wa Wales ameshakaa nje ya uwanja kwa kipindi cha miezi mitatu kutokana na majeruhi ya kifundo cha mguu. Akizungumza na wanahabari, Zidane amesema Bale amefanya jitihada kubwa za kurejea na kucheza baada ya kukaa nje kwa muda lakini amepata matatizo kidogo ndio maana ameamua kumpumzisha. Zidane aliendelea kudai kuwa ana matumaini ndani ya siku chache atakuwa fiti lakini kesho hatakuwa tayari.

CONTE AKUBALI LAWAMA KIPIGO CHA MAN UNITED.

MENEJA wa Chelsea, Antonio Conte amesema anakubali kulaumiwa kwa kushindwa kuwapa morari wachezaji wake kufuatia kipigo cha mabao 2-0 walichopata kutoka Manchester United jana. Kipigo hicho walichopata Old Trafford kinawafanya kutofautiana alama nne pekee dhidi ya Tottenham Hotspurs wanaoshikilia nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu. Conte amesema hawakucheza mchezo mzuri na United walistahili kushinda mchezo huo. Meneja huyo aliendelea kudai kuwa United walionyesha nia na ari zaidi kwenye mchezo huo jambo ambalo wao hawakufanya hivyo ndio maana anakubali lawama.

WES MORGAN AREJEA KUIOKOA LEICESTER.

NAHODHA wa Leicester City, Wes Morgan amefanya mazoezi na wachezaji wenzake mapema leo wakati wakijiandaa na mchezo wao wa mkondo wa pili wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Atletico Madrid. Morgan alikosa mchezo wa mkondo wa kwanza uliofanyika Vicente Calderon kufuatia kusumbuliwa na maumivu ya mgongo ambapo Leicester walifungwa bao 1-0. Hata hivyo, klabu hiyo ina matumaini kuwa beki huyo atarejea katika mchezo wa kesho, haswa kutokana na klabu hiyo kukumbwa na matatizo kwenye safu yao ya ushambuliaji. Robert Huth anatumikia adhabu na Younes Benalouane aliumia katika mchezo dhidi ya Crystal Palace Jumamosi iliyopita jambo ambalo linamfanya meneja Craig Shakespeare kupata wakati mgumu kwenye safu yake ya ulinzi.

MARC BARTA APATA UGENI WA WASHIKAJI.

BEKI mahiri wa Borussia Dortmund Marc Barta mwishoni mwa wiki hii amepata ugeni muhimu baada ya kutembelewa na wachezaji wenzake wa zamani wa Barcelona Jordi Alba na Sergio Busquets. Beki huyo wa kimataifa wa Hispania ndio pekee aliyeumia wakati basi la Dortmund liliposhambuliwa na mabomu wakati wkaiwa njiani kuelekea katika mchezo wao dhidi ya Monaco Jumanne iliyopita. Barta alifanyiwa upasuaji wa mkono na anatarajiwa kukosa mechi zote zilizosalia msimu huu kutokana na tukio hilo, lakini wakati akiwa kwenye wakati huo mgumu marafiki zake wawili wa karibu waliamua kumtembelea na kumjulia hali. Alba ambaye ametokea katika akademi ya Barcelona sambamba na Barta na Busquets, alituma picha ukurasa kwenye ukurasa wake wa Instagram wakiwa pamoja. Alba aliandika kwenye ukurasa wake huo kuwa anajisikia furaha kumuona rafiki yake na kucheka pamoja naye.

Friday, April 14, 2017

ZIDANE KUMPUMZISHA BALE.

WINGA wa Real Madrid, Gareth Bale anatarajiwa kukosa mchezo wa La Liga dhidi ya Sporting Gijon kesho kutokana na kutokuwa fiti. Kikosi cha Madrid kitakwenda kucheza mechi hiyo ya ugenini, mchezo ambao utafuatiwa na mechi mbili muhimu katika kipindi cha wiki moja. Mchezo wa mkondo wa pili war obo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Bayern Munich utafuatiwa siku tatu baadae, kabla ya Barcelona hawajakwenda Santiago Bernabeu kwa ajili ya El Clasico Jumapili ya Aprili 23. Bado alipata majeruhi madogo katika mchezo wa mkondo wa kwanza walioshinda mabao 2-1 Allianz Arena na meneja Zinedine Zidane ameamua kumpumzisha ili kupona kabisa kabla ya mechi hizo mbili kubwa zijazo.