Friday, March 30, 2012

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

LWIZA KUSIMAMIA EL MERREIKH, PLATINUM CL
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limemteua Alfred Kisongole Lwiza kuwa Kamishna wa mechiya Ligi ya Mabingwa (CL) kati ya El Merreikh ya Sudan na FC Platinum ya Zimbabwe. Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya kwanza itachezwa Aprili 7 mwaka huu kwenye Uwanja wa El Merreikh jijini Khartoum, Sudan kuanzia saa 2 kamili usiku. Katika mechi ya kwanza iliyochezwa wikiendi hii jijini Harare timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2. El Merreikh ni moja ya timu ambazo CAF iliziingiza moja kwa moja katika raundi ya kwanza. FC Platinum iliingia raundi ya kwanza baada ya kuing’oa Green Mamba ya Swaziland katika raundi ya awali.

ZIMBABWE YAITAKA TWIGA STARS
Chama cha Mpira wa Miguu Zimbabwe (ZIFA) kimeomba mechi ya kirafiki kati ya timu yake ya Taifa ya wanawake na Twiga Stars. Mechi hiyo itakayochezwa kati ya Aprili 28 au 29 mwaka huu jijini Harare. Mechi hiyo ni sehemu ya maandalizi ya timu ya Zimbabwe kwa ajili ya kutafuta tiketi ya kucheza Fainali zaNane za Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) zitakazofanyika Novemba mwaka huu nchini EquatorialGuinea. Twiga Stars ambayo iko kambini mkoani Pwani tangu Machi 25 mwaka huu chini ya Kocha Charles Boniface Mkwasa nayo inajiwinda kwa fainali hizo ambapo itacheza mechi ya kwanza Mei 26 mwaka huu jijini Addis Ababa dhidi ya Ethiopia. Zimbabwe yenyewe inacheza na Senegal. Machi 10 mwaka huu, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara alizindua akaunti ya Twiga Stars kupitia Tigo Pesa kuichangia timu hiyo ili ishiriki vyema michuano ya AWC. Wachangiaji wa Twiga Stars wanatakiwa kutuma mchango wao kwenda namba 13389 ambapo kiwango cha juu kinachoweza kutumwa kwa muhamala (transaction) mmoja ni sh. 500,000. Katika uzinduzi huo, Waziri Dk. Mukangara alichangia sh. milioni moja.

MTIHANI WA MAWAKALA WA WACHEZAJI
Mtihani kwa ajili ya mawakala wa wachezaji wanaotambuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utafanyika Machi 31 mwaka huu saa 4 kamili asubuhi ofisi za Shirikisho la Mpira wa MiguuTanzania (FIFA). Watu watatu wamejitokeza kufanya mtihani huo utakaokuwa na sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni maswali kutoka FIFA wakati nyingine ni kutoka TFF.

SIMBA, YANGA ZASAKA POINTI VPL
Yanga na Simba ni miongoni mwa timu nne zitakazokuwa viwanjani kesho (Machi 31 mwaka huu) kusaka pointi tatu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) ambayo iko katika raundi ya 22. Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga utakuwa mwenyeji wa mechi namba 148 kati ya Coastal Union na Yanga. Mechi hiyo itachezeshwa na mwamuzi Rashid Msangi wa Dodoma ambaye atasaidiwa na Rashid Lwena (Ruvuma) na Issa Malimali (Ruvuma). Mwamuzi Amon Paul wa Musoma ndiye atakayechezesha mechi namba 151 kati ya African Lyon na Simba itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Viingilio kwenye mechi ya African Lyon na Simba ni sh. 3,000 kwa viti vya kijani na bluu, sh. 5,000 viti vya rangi ya chungwa, sh. 10,000 kwa VIP C na B wakati VIP A ni sh. 15,000. Aprili Mosi mwaka huu kutakuwa na mechi ya VPL kati ya Azam na Ruvu JKT itakayochezwa Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Kiingilio katika mechi hiyo kitakuwa sh. 1,000 kwa mzunguko na sh. 5,000 jukwaa kuu.

SENEGAL MGUU NJE MGUU NDANO OLIMPIKI.

SIMBA wa Teranga, Senegal watamenyana na Oman katika mechi maalum ya kuwania tiketi ya kucheza Olimpiki mwaka huu, London, mchezo utakaofanyika Aprili 23 mjini Coventry. Mechi hiyo itaamua timu ya mwisho ya kukamilisha idadi ya timu 16 za kucheza Olimpiki inayotarajiwa kuanza Julai 26 hadi Agosti 11, mwaka huu. Simba wa Teranga wamepata nafasi hiyo baada ya kushika nafasi ya nne katika michuano ya Afrika ya vijana chini ya umri wa miaka 23 iliyofanyika Morocco Desemba mwaka jana. Oman inayofundishwa na Mfaransa, Paul Le Guen walipata nafasi hiyo baada ya kuifunga Uzbekistan 2-0 Alhamisi katika mechi ya mwisho ya kuwania kufuzu kucheza fainali hizo kwa bara la Asia. Gabon, Morocco Misri ni wawakilishi wengine wa Afrika kwenye Olimpiki ya mwaka huu. Timu nyingine zilizofuzu ni mbali na wenyeji Uingereza, ni kwa upande wa bara ya Asia ni Korea Kusini, Japan, Falme za Kiarabu, huku Brazil na Uruguay ikiwakilisha Amerika Kusini, wakati Uswisi, Hispania na Belarus wakiwakilisha Ulaya na New Zealand wakiwakilisha OCEANIA. Wawakilishi wengine wawili watatoka Amerika Kaskazini, michuano yao inatarajiwa kumalizika Jumatatu ijayo.

MADRID KUFUNGUA ACADEMY CHINA.

VIGOGO wa Ulaya, Real Madrid wako mbioni kufungua shule ya soka nchini China mwakani, wakiungana na klabu ya Ligi Kuu ya China, Guangzhou Evergrande, taarifa ambayo imetolewa na mmiliki klabu hiyo ya China katika tovuti yake. Madrid, ambao ni mabingwa mara nyingi zaidi Ulaya, wakiwa wameshinda kombe hilo mara tisa, wako katika mpango wa kujitangaza zaidi na wameingia China, ambayo inavutia klabu nyingine kubwa Ulaya. Shule hiyo itakayokuwa kusini mwa jiji la Guangzhou, itakuwa na wachezaji wapatao 3,000 katika mwaka wa kwanza, watakaokuwa wakitumia vifaa na kufundishwa kwa ubora ule ule wa shule ya Real Madrid nchini Hispania. Kocha wa vijana wa klabu hiyo ya Hispania, Fernando Sanchez Cipitria ameteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Ufundi.

BERLUSCONI AKIRUDIA KITI CHAKE MILAN.

WAZIRI Mkuu wa zamani wa Italia Silvio Berlusconi amekalia rasmi kiti chake cha urais wa klabu ya AC Milan ya nchini humo baada ya kujiuzulu uongozi wan chi hiyo Novemba mwaka jana. Taarifa kutoka klabuni hapo imetangaza kuwa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo ilimteua Berlusconi kama rais wa heshima wa klabu hiyo. Siku zote Berlusconi amekuwa akikaimu nafasi ya urais wa klabu hiyo, ingawa makamu wa rais Adriano Galliani amekuwa akiiendesha klabu hiyo kwa shughuli za kila siku. Kiongozi huyo wa zamani wa nchi hiyo ambaye alijiuzulu kutokana na matatizo ya kiuchumi yaliyoikumba Italia mwaka jana amewahi kuwa rais wa Milan kutoka mwaka 1986 mpaka 2004 na kurudia tena nafasi hiyo mwaka 2006 mpaka 2008. Katika hatua nyingine mshambuliaji wa klabu hiyo Antonio Cassano ameanza kufanya mazoezi na wachezaji wenzake kwa mara ya kwanza toka alipofanyiwa upasuaji mdogo wa moyo Novemba mwaka jana ingawa bado anahitaji kupona zaidi ili aweze kucheza na hata kuwa na muda wa kujiunga na kikosi hicho katika michuano ya Klabu Bingwa ya Ulaya.

MARADONA BLASTS 'COWARDS' AFTER WIFE ATTACK.

KOCHA wa klabu ya Al Wasl ya Muungano wa Falme za Kiarabu-UAE amewashambulia mashabiki wa huko na kuwaita waoga baada ya kulazimika kukimbilia jukwaani kumuokoa rafiki yake wa kike ambaye alikuwa akishambuliwa na mashabiki wenye hasira. Nguli huyo wa soka wa zamani kutoka Argentina alishuhudia timu yake hiyo ikipoteza mchezo dhidi ya Al Shabab kwa mabao 2-0 katika Ligi Kuu ya UAE wakati wake na marafiki wa kike wa wachezaji wakilazimika kuzindikizwa kutoka nje ya Uwanja wa Al Mamzar, Dubai. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na luninga moja maarfu nchini humo ya Gulf ilisema kuwa vurugu hizo zilianza wakati mshambuliaji wa Mbrazil wa Al Shabab aitwae Ciel ambaye alifunga mojawapo ya mabao ya timu yake mashabiki wa Al Wasl. Mashabiki wa Al Shabab nao wakajibu mapigo kwa kumgeukia rafiki yake wa kike Maradona na aitwae Veronica Ojeda na kuanza kumtupia maneno ya kumdhalilisha. Akihojiwa mara baada ya tukio Maradona amesema kuwa kitendo hicho kimemsononesha sana kwakuwa hakutegemea mashabiki hao wangekuwa waoga kiasi hadi kupelekea kuwashambulia wanawake badala ya kumshambulia yeye mwenyewe.

Wednesday, March 28, 2012

MANCHESTER UNITED ENJOY REFEREEING 'ADVANTAGE' - VIERA.

MCHEZAJI wa zamani wa kimataifa wa Ufaransa ambaye kwasasa ni mmoja wa maofisa wa klabu ya Manchester City, Patrick Viera amesema kuwa wapinzani wao katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza Manchester United wanasaidiwa na makosa ya waamuzi. Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku mbili baada ya timu ya Fulham kukataliwa penati katika dakika za mwisho katika mchezo baina ya United na timu hiyo uliochezwa katika Uwanja wa Old Trafford ambapo wenyeji waliibuka na ushindi wa bao 1-0. Matokeo hayo yanaifanya United kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo wakiwa na alama tatu zaidi ya wapinzani wao City. Akihojiwa Viera amesema kuwa United wakati wanacheza nyumbani wanapata faida kama hizo ambazo timu zingine hazipati na sio United pekee hata ukicheza na Real Madrid, Barcelona au AC Milan matatizo kama hayo huwa yanatokea. Aliendelea kusema kuwa faida kama hizo huwa zinapata timu ambazo zimezoea kupata ushindi mara zote hivyo na wao wanahitaji kushinda michezo mingi zaidi ili waweze kupata faida kama hizo huko mbeleni. Wakiwa wamebakisha michezo nane, City wamejikuta wakiwa nyuma ya United kwa alama tatu lakini Viera ambaye amechukua nafasi kama Ofisa wa Maendeleo wa klabu hiyo baada ya kustaafu kucheza anaamini kuwa City wanastahili kuwa mabingwa.

SHEIKH KHALIFA WA UAE AMWAGA MINOTI KWA VIJANA WAKE.

RAIS wa Falme za Kiarabu-UAE Sheikh Khalifa bin Zayed ameipa timu ya taifa ya nchi hiyo ya vijana chini ya miaka 23 ambao wamefanikiwa kufuzu michuano ya Olimpiki inayotarajiwa kufanyika jijini London mwaka huu euro 100,000 kila mmoja. Timu hiyo imefanikiwa kukata tiketi ya kucheza michuano hiyo kwa mara ya kwanza katika historia ya mpira ya nchi hiyo kwa kuifunga Uzbekistan kwa mabao 3-2 mapema mwezi huu. Hayo ni mafanikio makubwa kabisa katika historia ya soka ya nchi hiyo yenye utajiri mkubwa wa mafuta toka timu ya wakubwa ya nchi hiyo ilipofanikiwa kukata tiketi ya kushiriki michuano ya Kombe la Dunia mwaka 1990 kwa mara ya kwanza. Sheikh Khalifa aliwapokea wachezaji wa timu hiyo pamoja na viongozi wao katika kasri lake la Dhiyafa lililopo Abu Dhabi mapema wiki hii kabla ya kuwakabidhi zawadi hiyo.

KOREA KUSINI KUJIPIMA NGUVU NA HISPANIA.

CHAMA cha Soka cha Korea Kusini-KFA kimetangaza mkakati wake wa kupambana na mabingwa wa dunia Hispania Mei 30 mwaka huu. Timu ya taifa ya Korea inajipanga kumaliza mzunguko wake wa mwisho wa mechi za kufuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 mwezi Juni mwaka huu hivyo mchezo huo utakuwa mahsusi kwa ajili ya maandalizi ya michezo hiyo. Korea ambao wanajulikana kwa jina la utani la Taeguk Warriors wako katika kundi A wakiwa na timu za Iran, Uzbekistan, Qatar na Lebanon ambapo wanatarajia kucheza mchezo wao wa mzunguko wa nne jijini Doha Juni 8 mwaka huu. Kwa upande wa Hispania wao watatumia mchezo huo kama maandalizi ya michuano ya Ulaya ambayo inatarajiwa kuchezwa Juni mwaka huu huko Poland na Ukraine ambapo mabingwa hao watetezi wa michuano hiyo wamepangwa kundi C wakiwa na timu za Italia, Jamhuri ya Ireland na Croatia.

HEART SPECIALIST: MUAMBA UNLIKELY TO RETURN.

BAADA ya moyo kushindwa kufanya kazi wakati wa mchezo wa Kombe la FA kati ya Bolton Wanderers na Tottenham Hotspurs katikati ya mwezi huu Fabrice Muamba hatarajiwi kucheza soka tena kwa mujibu wa daktari bingwa wa magonjwa ya moyo. Mkurugenzi mtabibu wa Mfuko wa Magonjwa ya Moyo Peter Weissberg amekiri kuwa itakuwa sio suala sahihi kwa mtu kumshauri mchezaji huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Uingereza ya vijana chini ya miaka 21 kuendelea kucheza soka. Weissberg anaelewa kuwa suala la Muamba kucheza soka tena sio rahisi kwa sababu tatizo la kusimama kwa moyo wake kufanya kazi limechangiwa kwa kiasi kikubwa na na mazoezi anayofanya hivyo itakuwa sio busara mchezaji huyo kurejea uwanjani tena. Akihojiwa Weissberg amesema kuwa sio rahisi kusema kwasasa lakini anafikiri mchezaji atashauriwa kutocheza soka tena kwasababu tatizo hilo lililomkumba linachangiwa kwa kiasi kikubwa na mazoezi magumu anayofanya. Tatizo la moyo kwa wachezaji mpira limekuwa ni la kawaida kutokana na matukio mengi kuwa yanatokea katika miaka ya hivi karibuni wakiwemo wachezaji kama Ruben de la Red na Sergio Sanchez kupumzika kucheza kutokana na matatizo hayo wakati Marc Vivien Foe, Antonio Puerta na Dani Jargue wote walikufa kutokana na matatizo ya moyo.

Tuesday, March 27, 2012

MADRID, CHELSEA ZATENGENEZA MAZINGIRA MAZURI YA KUSONGA MBELE.

KLABU za Chelsea na Real Madrid jana usiku zimefanikiwa kushinda michezo yao ya kwanza ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kutinga Nusu Fainali. Salomon Kalou aliunganisha krosi ya Fernando Torres dakika ya 75, kuipatia Chelsea ushindi wa 1-0 dhidi ya Benfica jijini Lisbon, Ureno, huo ukiwa ushindi wa kwanza ugenini kwa timu hiyo kwenye mashindano hayo msimu huu. Nchini Cyprus, Karim Benzema alifunga bao la kichwa dakika ya 74 akimalizia krosi safi iliyopigwa na Kaka, huku Kaka nae akifunga bao la pili wakati Benzema alipoongeza lingine dakika ya 82 na kuihakikishia ushindi Real Madrid wa mabao 3-0 dhidi ya APOEL Nicosia. Michezo ya marudiano baina ya timu hizo itapigwa Aprili 4 mwaka huu ambapo Chelsea wataikaribisha Benfica katika Uwanja wa Stamford Bridge huku Madrid wakiwakaribisha APOEL katika Uwanja wa Santiago Bernabeu nchini Hispania. Michezo mingine ya kwanza ya robo fainali inatarajiwa kuendelea tena leo ambapo mabingwa watetezi wa michuano hiyo Barcelona watachuana na AC Milan huku Olympic Marseille wakiikaribisha Bayern Munich huko Ufaransa.

CHELSEA YAJITENGENEZEA MAZINGIRA MAZURI YA KUSONGA MBELE CHAMPIONS LEAGUE.

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

VITA VPL YAHAMIA MORO UNITED, VILLA
Timu za Moro United na Villa Squad ambazo ziko kwenye vita ya kukwepa kushuka daraja katika Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) zinapambana kesho (Machi 28 mwaka huu) kwenye moja kati ya mechi mbili za siku hiyo. Mechi hiyo namba 153 itachezwa kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili. Moro United iko nafasi ya 11 ikiwa na pointi 18 wakati Villa Squad iko nafasi ya 14 kwa pointi zake 14. Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 1,000 kwa mzunguko na sh. 5,000 kwa jukwaa kuu. Mwamuzi atakuwa Andrew Shamba akisaidiwa na Samson Kobe na Idd Mikongoti wote wa Dar es Salaam. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Arthur Mambeta wa Dar es Salaam wakati mtathmini wa waamuzi (referees assessor) ni Emmanuel Chaula kutoka mkoani Rukwa. Mechi nyingine ya Machi 28 mwaka huu itakayochezeshwa na mwamuzi Judith Gamba wa Arusha itakuwa kati ya Ruvu Shooting itakayoikaribisha Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani. Gamba katika mechi hiyo namba 150 atasaidiwa na Saada Tibabimale kutoka Mwanza na Hellen Mduma wa Dar es Salaam. Mwamuzi wa akiba ni Juma Safisha wa Pwani wakati Kamishna ni Hamis Kissiwa wa Dar es Salaam. Mechi za Machi 31 mwaka huu ni Coastal Union dhidi ya Yanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, wakati Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utakuwa mwenyeji wa mechi ya African Lyon na Simba.

RHINO, POLISI DAR KUANZA FAINALI FDL
Timu za Rhino Rangers ya Tabora na Polisi Dar es Salaam zitapambana Machi 31 mwaka huu katika moja ya mechi za ufunguzi wa fainali za Ligi Daraja la Kwanza zitakazochezwa Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro. Kila siku zitachezwa mechi mbili, moja ikianza saa 8 mchana wakati ya pili ni saa 10 jioni ambapo fainali hiyo itamalizika Aprili 22 mwaka huu kwa timu tatu za kwanza kupanda Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao- 2012/2013. Morogoro imepewa uenyeji baada ya kulipa sh. milioni 20.5 kati ya sh. milioni 25 zilizotakiwa. Sh. milioni 4.5 zilizobakia imekubaliana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuwa itazilipa moja kwa moja kwenye huduma zitakazotumiwa na wasimamizi wa fainali hizo. Mkoa mwingine ulioomba uenyeji ulikuwa Mbeya. Lakini wenyewe hadi Machi 26 mwaka huu ambayo ilikuwa siku ya mwisho kufanya malipo ulikuwa umeingiza kwenye akaunti ya TFF sh. milioni 15. Upangaji ratiba (draw) ulifanyika jana (Machi 26 mwaka huu) kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kushuhudiwa na viongozi wa timu saba kati ya tisa zinazocheza fainali hizo. Mechi ya pili siku ya ufunguzi itakuwa kati ya Trans Camp na Mbeya City Council. Aprili Mosi ni Tanzania Prisons na Polisi Morogoro zitakazocheza mchana wakati jioni ni Mgambo Shooting na Mlale JKT. Aprili 2 mwaka huu ni Polisi Tabora vs Rhino Rangers (mchana) na Polisi Dar es Salaam vs Trans Camp (jioni). Aprili 3 mwaka huu ni Mbeya City Council vs Tanzania Prisons (mchana) na Polisi Morogoro vs Mgambo Shooting (jioni). Aprili 5 mwaka huu ni Polisi Tabora vs Mlale JKT (mchana) wakati jioni ni Rhino Rangers vs Trans Camp. Aprili 6 mwaka huu Polisi Dar es Salaam vs Mbeya City Council (mchana) wakati jioni ni Tanzania Prisons vs Mgambo Shooting. April 8 mwaka huu ni Mlale JKT vs Polisi Morogoro (mchana) wakati jioni itakuwa Polisi Tabora vs Polisi Dar es Salaam. Aprili 9 mwaka huu ni Mgambo Shooting vs Rhino Rangers (mchana) wakati jioni ni Trans Camp vs Tanzania Prisons. Aprili 11 mwaka huu ni Mbeya City Council vs Polisi Tabora (mchana) na Mlale JKT vs Rhino Rangers (jioni). Aprili 12 mwaka huu Polisi Dar es Salaam vs Mgambo Shooting (mchana) na Polisi Morogoro vs Trans Camp (jioni).

LIGI YA TAIFA KUANZA APRILI 22
Kamati ya Mashindano ya TFF iliyokutana Machi 24 mwaka huu imepitisha michuano ya Ligi ya Taifa Ngazi ya Taifa inayoshirikisha mabingwa wa mikoa ianze Aprili 22 mwaka huu kwenye vituo vitatu tofauti. Wakati Machi 26 mwaka huu ndiyo ilikuwa mwisho kwa vyama vya mikoa kuwasilisha TFF majina ya mabingwa wao, ni mikoa minne tu iliyomudu kufanya hivyo kwa mujibu wa kalenda ya matukio ya TFF. Mikoa hiyo na mabingwa wake kwenye mabano ni Kigoma (Kanembwa FC ya Kibondo), Ruvuma (Mighty Elephant ya Songea), Kilimanjaro (Forest FC ya Siha) na Dodoma (CDA ya Dodoma Mjini).Hivyo Kamati ya Mashindano imeongeza muda hadi Aprili 9 mwaka huu kwa mikoa  ambayo haijawasilisha majina ya mabingwa wao iwe imefanya hivyo. Kwa itakayoshindwa ndani ya muda hiyo, mabingwa wao hawatapata fursa ya kucheza ligi hiyo. Kamati imetoa pongezi kwa mikoa hiyo minne kwa kuhakikisha imechezesha ligi yao kwa mujibu wa kalenda ya matukio ya TFF. Pia imepanga makundi matatu ya ligi hiyo. Kundi A lina mikoa ya Rukwa, Mbeya, Ruvuma, Iringa, Morogoro, Lindi na Mtwara. Kundi B lina mabingwa wa mikoa ya Kigoma, Tabora, Shinyanga, Mwanza, Mara, Kagera, Singida na Dodoma. Kundi C ni Dar 1, Dar 2, Dar 3, Pwani, Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara. TFF inakaribisha maombi ya uenyeji kwa kila kundi. Taarifa rasmi itatumwa kwa vyama mikoa kueleza masharti ya kutimiza kabla ya mkoa kupewa kituo cha ligi hiyo. Mshindi katika kila kundi na washindwa bora (best losers) wawili kutoka kwenye makundi yenye timu nane watapanda daraja msimu ujao kucheza Ligi Daraja la Kwanza (FDL). Pia timu zinatakiwa ziwe zimefanya usajili wa wachezaji kufikia Aprili 10 mwaka huu wakati Aprili 11-18 itakuwa ni kipindi cha kutangaza majina na pingamizi.

KOMBE LA FA KUANZA TENA MSIMU UJAO
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limerejesha tena mashindano ya Kombe la FA (TFF) kuanzia msimu ujao 2012/2013 ambapo bingwa wa michuano hiyo ataiwakilisha Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho. Timu zinazotakiwa kushiriki michuano hiyo itakayochezwa kwa mtindo wa mtoano ni zilizosajiliwa ambapo katika maombi yao ni lazima ziambatanishe nakala ya hati ya usajili wa klabu ambayo itatakiwa kuidhinishwa na chama cha mpira wa miguu cha wilaya. Ada ya fomu ya maombi ya kushiriki ni sh. 20,000 wakati ada ya mashindano ni sh. 200,000. Usajili wa wachezaji katika Kombe la FA ni ule ule mmoja wa kalenda ya usajili ya TFF ambapo unaanza Juni Mosi na kumalizika Septemba 10.

BECKHAM KUUZA MAGARI YAKE YA KIFAHARI.

Moja ya magari ya kifahari ya David Beckham.
HIVI ni kweli Beckham atakuwa ameishiwa? Hapana, inaweza isiwe hivyo. Lakini hilo linaweza kufafanua ni kwanini ameripotiwa kuuza magari yake matano ya kifahari aliyonayo. Gazeti moja la udaku nchini Uingereza la The Sun limeripoti kuwa David Beckham mwenye umri wa miaka 36 ameamua kuuza magari yake ya kifahari ambayo ni mawili aina ya Bentleys, BMW 645, Range Rover Sport pamoja na lingine aina ya Lamborghini Gallardo ambayo yamepaki katika jumba lake la kifahari la Sawbridgeworth. Gari la Lamborghini peke yake lina thamani ya paundi 170,000 au kwa lugha nyingine unaweza kusema mshahara wa siku 10 wa mchezaji huyo. 
Hivi karibuni Beckham alionekana katika jiji la Los Angeles akitumia pikipiki katika matembezi yake maeneo mbalimbali ya mji huo.

ABIDAL KUPIGWA KISU.

BEKI wa Barcelona, Eric Abidal anatarajiwa kufanyiawa upasuaji wa kupandikiza ini katika hospitali moja nchini Barcelona. Taarifa zilizotolea na klabu hiy zinasema kwamba mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa amechangiwa ini hilo atalopandikizwa kutoka kwa rafiki yake wa karibu ambaye wamekuwa wote toka utotoni. Kulikuwa kuna wasiwasi kwamba Abidal asingecheza tena soka ya ushindani baada ya upasuaji kama huo mwaka jana, lakini Mfaransa huyo alipona na kurudi kazini akicheza soka safi katika ushindi wa 3-1 wa Barca dhidi ya Manchester United katika fainali ya Ligi ya Mabingwa kwenye Uwanja wa Wembley. Abidal pia hivi karibuni alisaini mkataba mpya na Barcelona ambao haujaweka wazi ni kwa muda gani mchezaji huyo ataitumikia klabu hiyo..

REAL MADRID, CHELSEA KIBARUANI ULAYA LEO.

MICHUANO ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya inaendelea tena leo ambapo viwanja viwili vitawaka moto katika michezo ya robo fainali ya michuano hiyo. Katika michezo ya leo timu ya APOEL Nicosia itakuwa na kibarua kigumu wakati itapoikaribisha timu ya Real Madrid katika wake wa nyumbani nchini Ugiriki huku wpinzani wao hao wakipewa nafasi kubwa ya kushinda mchezo huo. Kocha wa Madrid Jose Mourinho amewatahadharisha wachezaji wake kuwa mchezo huo hautakuwa rahisi hivyo wajizatiti na kucheza katika kiwango chao cha juu baada ya siku za hivi karibuni kuonekana wakilegalega katika Ligi Kuu nchini Hispania kwa kupoteza baadhi ya pointi. Mchezo mwingine ambao nao unatarajiwa kuwa mgumu utakuwa ni kati ya Benfica ya Ureno ambao wataikaribisha Chelsea katika uwanja wao wa nyumbani ambapo ushindi wataoupata katika mchezo huu wa kwanza utawaweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele. Chelsea itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu nzuri ya kuitoa Napoli kwa ushindi wa kushangaza chini ya kocha wake Roberto Di Matteo ambaye toka alipoanza kuinoa klabu hiyo imeonekana kurudi kwenye kiwango kizuri licha ya kufungwa na Manchester City katika mchezo wa LIgi Kuu nchini Uingereza.

MUAMBA AIZINDUA FIFA.

Jiri Dvorak.
SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa-FIFA, inafanya uchunguzi juu ya matatizo ya moyo yanayowakumba wachezaji ili kubaini kiini cha matatizo hayo. Hatua hiyo inafuatia kiungo mwenye asili ya DRC, Fabrice Muamba kuanguka uwanjani na kuzimia na hadi sasa amelazwa, ingawa ameanza kupata nafuu. Ofisa Mkuu wa Tiba wa FIFA, Jiri Dvorak, amesema leo kwamba mpango huo utafanyika katika mkutano wa tiba Mei 23 na 24 mjini Budapest, Hungary. Dvorak amesema kuwa katika mkutano wamewaalika madokta wote wa timu za taifa ili kuangalia kwa kina matatizo hayo ya moyo yanayowakumba wachezaji. Kwasasa Muamba mwenye miaka 23 hali yake inaendelea vizuri ingawa bado yuko katika uangalizi maalumu katika hospitali ya London Chest nchini Uingereza ambapo amelazwa toka alipoanguka wakati wa mchezo war obo fainali ya Kombe la FA.

HAVELANGE HALI TETE.

RAIS wa zamani wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Joao Havelange ameingia katika wiki ya pili tangu alazwe katika hospitali ya Samaritano na yuko katika hali mbaya kwa sababu ya madhara yanayomsibu kwenye kifundo cha mguu wake wa kulia. Taarifa ya hospital ya Samaritano imesema juana kwamba babu huyo mwenye umri wa miaka 95 sasa, Havelange anatibiwa kwa dawa za antibiotics na afya kwa hakika si njema. Havelange alilazwa Machi 18 kutokabna na matatizo yake hiyo yanayosababisha kudhoofu kwa kiungo, ingawa anapumua bila msaada wa mashine. Alistaafu kwenye Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki mwaka jana, kwa sababu za kiafya. Havelange alikuwa rais wa FIFA tangu 1974-98.

Saturday, March 24, 2012

VURUGU ZAISABABISHIA ADHABU GOR MAHIA.

BODI ya Viwanja vya Michezo nchini Kenya (SSMB) imeifungia klabu ya Gor Mahia kutumia Viwanja vya Nyayo na Moi International Sports Centre Kasarani. Hatua hiyo inakuja baada ya vurugu za mwishoni mwa wiki katika mechi yao na wapinzani wao wa jadi, AFC Leopards ambayo ilivunjika baada ya dakika 26 tu. Uamuzi huo umefikiwa kutangazwa na Mwenyekiti wa bodi hiyo, Generali Mstaafu Daniel Opande. Pamoja na hayo, uamuzi hao haupokewa vizuri na Gor Mahia ambayo imechukuliwa kama ni wa haraka. Kifungo hicho kinawafanya Gor Mahia wawe na Uwanja mmoja tu wa kutumia, City ambao hauendani na idadi kubwa ya mashabiki wao

Friday, March 23, 2012

WENGER WANT QUALITY NOT QUANTITY.

KOCHA wa Arsenal amewaonya mashabiki wa timu hiyo kuwa wasitegemee mabadiliko makubwa katika klabu yake mwishoni mwa msimu huu kwasababu amepanga kununua wachezaji wenye majina makubwa. Mashabiki klabu hiyo wamekuwa na hasira na kocha huyo kutokana na kushindwa kusajili wachezaji ambao watakata kiu ya timu hiyo kukosa vikombe kwa miaka saba sasa nab ado wamendelea kumhimiza kutafuta wachezaji wazuri msimu ujao. Lakini Wenger ambaye Ijumaa alikataa taarifa kwamba mshambuliaji wa kimataifa kutoka Ujerumani Lukas Podolski amefanyia vipimo vya afya katika harakati za kujiunga na klabu hiyo ameamua kusajili wachezaji ambao anaamini kuwa watakuwa na kipaji kulingana fungu atakalokuwa nalo. Akihojiwa Wenger amesema kuwa kwasasa wana idadi ya wachezaji 25 huku wengine wengi wakiwa wancheza kwa mkopo katika klabu zingine na pia wamecheza bila Jack Wilshere na Abou Diaby karibu msimu mzima kutoka majeraha waliyonayo ambapo kama wachezaji hao wakirudi na kikosi kitaimarika zaidi kwani hata sasa wako katika nafasi nzuri bila kuwa na hao wachezaji. Kwasasa kocha huyo anakiwa kuhakikisha timu hiyo inamaliza ikiwa juu ya Tottenham Hotspurs na Chelsea katika nafasi ya tatu mwa msimamo wa Ligi Kuu nchini Uingereza ili kujihakikishia nafasi ya moja kwa moja kushiriki michuano ya Klabu Bingwa ya Ulaya msimu ujao.

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

KUONA MORO UNITED, AFRICAN LYON 1,000/-
Viingilio kwenye mechi namba 149 ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Moro United na African Lyon itakayochezwa kesho (Machi 24 mwaka huu) Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam ni sh. 1,000 kwa mzunguko na sh. 5,000 kwa jukwaa kuu. Mwamuzi Hashim Abdallah wa Dar es Salaam ndiye atakayechezesha mechi hiyo akisaidiwa na Ephraim Ndissa na Abdallah Selega wakati mwamuzi wa akiba ni Oden Mbaga. Wote pia wanatoka Dar es Salaam. Kamishna wa mechi hiyo ni James Mhagama kutoka mkoani Ruvuma. Pia viingilio hivyo ndivyo vinavyotumika kwa mechi zote za Ligi Kuu ya Vodacom zinazochezwa Uwanja wa Chamazi zisizohusisha timu za Simba na Yanga. VPL itaendelea tena Machi 28 mwaka huu kwa mechi kati ya Ruvu Shooting Stars itakayocheza na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mabatini mjini Mlandizi wakati Moro United itakuwa mwenyeji wa Villa Squad katika mechi namba 153 itakayofanyika Uwanja wa Chamazi.

MMOJA AONGEZWA TWIGA STARS
Kocha Charles Boniface Mkwasa wa Twiga Stars amemuongeza mshambuliaji Rehema Salum wa Shule ya Sekondari Lord Baden ya mkoani Pwani kwenye kikosi hicho kitakachoingia kambini Machi 25 mwaka huu. Rehema aliibuka mfungaji bora kwenye mashindano maalumu ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyoshirikisha shule nane za sekondari za Mkoa wa Dar es Salaam na kuhitimishwa Machi 8 mwaka huu. Twiga Stars itaingia kambini kwenye kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) iliyoko Ruvu mkoani Pwani ikiwa ni sehemu ya maandalizi kwa ajili ya mechi ya mchujo ya Fainali za Wanawake Afrika (AWC) zitakazofanyika Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea. Timu hiyo itacheza na Ethiopia kusaka tiketi ya kwenda Equatorial Guinea ikianzia ugenini Addis Ababa kwa mechi itakayochezwa Mei 26 mwaka huu. Timu hizo zitarudiana wiki mbili baadaye jijini Dar es Salaam. Katika raundi ya kwanza, Twiga Stars iliitoa Namibia kwa jumla ya mabao 7-2. Ilishinda ugenini 2-0 na kuibuka na ushindi mnono nyumbani wa mabao 5-2. Machi 10 mwaka huu, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara alizindua akaunti ya Twiga Stars kupitia Tigo Pesa kuichangia timu hiyo ili ishiriki vyema michuano ya AWC. Wachangiaji wa Twiga Stars wanatakiwa kutuma mchango wao kwenda namba 13389 ambapo kiwango cha juu kinachoweza kutumwa kwa muhamala (transaction) mmoja ni sh. 500,000. Katika uzinduzi huo, Waziri Dk. Mukangara alichangia sh. milioni moja.

MTIHANI WA MAWAKALA WA WACHEZAJI
Mtihani kwa kwa ajili ya watu wanaotaka kuwa mawakala wa wachezaji na mechi wanaotambuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utafanyika Machi 31 mwaka huu saa 4 kamili asubuhi ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (FIFA). Kwa wanaotaka uwakala huo wanatakiwa kujisajili ambapo watapewa kanuni mbalimbali za FIFA na TFF ili waweze kujiandaa kikamilifu kwa mtihani huo utakaokuwa na sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ya mtihani huo ni maswali kutoka FIFA wakati nyingine ni kutoka TFF.

Thursday, March 22, 2012

STEVANOVIC KUIBURUZA GHANA FA FIFA.

BAADA ya kutimuliwa kukinoa kikosi cha timu ya taifa ya Ghana aliyekuwa kocha wa timu hiyo Goran Stevanovic amelitahadharisha Shirikisho la Soka la Ghana-GFA kuhusu malipo yake mara baada ya kuvunja mkataba wake. Kocha huyo raia wa Serbia amewapa siku 14 mabosi wake hao kumlipa fedha zake zote na kama wakishindwa kufanya hivyo basi atawashitaki GFA kwa Shirikisho la Soka duniani-FIFA. Katika barua hiyo iliyotumwa kwa GFA imeweka wazi kuwa hakubaliani na ombi la shrikisho hilo kumlipa mshahara wa miezi mitatu na badala yake wanahitaji mshahara wote wa miezi 24 kama walivyokubaliana wakati anasaini mkataba. Barua hiyo iliendelea kusema kuwa kama GFA haitatimiza hilo suala ndani ya siku 14 basi watalipeleka suala hilo ikaamuliwe FIFA. Jumatatu iliyopita Stevanovic alitimuliwa kibarua cha kukinoa kikosi hicho ambacho alianza kukifundisha Januari mwaka 2011 ambapo alikuwa akilipwa kiasi cha euro 30,000 kwa mwezi na nafasi yake imechukuliwa na msaidizi wake Kwesi Appiah ambaye atakaimu nafasi hiyo mpaka atakapopatikana kocha wakudumu.

MANCINI AFUNGUKA KUHUSU TEVEZ.

KOCHA wa Manchester City, Roberto Mancini anatarajia Carlos Tevez atasaidia sana klabu yake kutimiza ndoto za kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England baada ya kuanza kazi rasmi jana. Tevez alikuwa kivutio kwenye ushindi wa 2-1 dhidi ya Chelsea akirejea kwa mara ya kwanza tangu Septemba usiku wa jana Uwanja wa Eastlands, ingawa alianzia benchi. Mshambuliaji huyo wa Argentina alitengeneza bao la ushindi lilifungwa na Samir Nasri na kuifanya timu yake ipunguze pengo la pointi hadi kubaki moja dhidi ya vinara wa ligi hiyo, Manchester United. Sergio Aguero alisawazisha kwa penalti dakika chache tu baada ya Tevez kuingia hivyo kufanya mchezo uwe 1-1 baada ya Gary Cahill kutangulia kuifungia Chelsea. Akihojiwa mara baada a mchezo huo Mancini amesema kuwa Carlos alifanya vizuri kutoa pasi ya mwisho ambayo Nasri alifunga na mashabiki walifurahia hilo ila mchezaji huyo anahitaji muda zaidi na haitakuwa kazi rahisi lakini pengine baada ya muda wa wiki mbili huko mbele atakuwa katika kiwango kizuri zaidi.

HALI YA HAVELANGE BADO TETE.

Former FIFA President and former IOC member Joai Havelange.
RAIS wa zamani wa Shirikisho la Soka Dunia-FIFA na Mjumbe wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki-IOC Joai Havelange bado anaendelea kupata matibabu akitibu maambukizi aliyopata kwenye kidonda alichopata katika kifundo cha mguu wake wa kulia. Taarifa iliyotoka katika Hospitali ya Samaritano iliyopo katika jiji la Rio de Janeiro imesema kuwa Havelange ambaye ana umri wa miaka 95 hali yake bado si nzuri taarifa ambayo ilipingana na ile iliyotolewa na Shrikisho la Soka nchini humo iliyosema kwamba Havelange anaendelea vizuri. Havelange amewahi kuliongoza shirikisho la soka la Brazil kwa karibu miongo miwili ikiwemo miaka ambayo nchi hiyo ilifanikiwa kunyakuwa Kombe la Dunia mara tatu katika miaka ya 1958, 1962, na 1970. Havelange amekalia kiti cha urais cha FIFA kuanzia mwaka 1974 mpaka 1998 na kubakia kuwa rais wa heshima wa shirikisho hilo ambapo yeye ndio rais wa mwisho kabla ya rais wa sasa Sepp Blatter kushika madaraka hayo.

"CARDIAC ARREST" YAMUUA MCHEZAJI INDIA.

Baadhi ya wachezaji na watu wa huduma ya kwanza wakimbeba D Venkatesh ili kumuwahisha hospitalini.
MCHEZA soka nchini India amefariki dunia baada ya kuanguka na kuzirai wakati akicheza mpira ikiwa ni siku chache baada ya mchezaji wa Bolton Wanderers Fabrice Muamba kukumbwa na tatizo kama hilo katika mchezo wa Kombe la FA nchini Uingereza Jumamosi iliyopita. Mchezaji huyo anayeitwa D Venkatesh mwenye umri wa miaka 28 alianguka baada ya moyo wake kusimama kufanya kazi ikiwa ni muda mfupi baada ya kuingia uwanjani kama mchezaji wa akiba wakati wa mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza kati ya timu yake ya Bangalore Mars dhidi ya South Western Railway. Vyombo vya habari nchini humo vimesema kuwa hakukuwa na na gari la wagonjwa uwanjani hapo wakati tukio hilo lilikitokea hivyo kupelekea mchezaji huyo kukimbizwa hospitali na pikipiki za miguu mitatu maarufu kama Bajaj. Taarifa hiyo pia ilithibitishwa na Shrikisho la Soka nchini India-AIFF juu ya kifo cha mchezaji huyo ambaye alifariki wakati akifikishwa hospitalini.

MUAMBA ALIKUFA KWA DAKIKA 78-DAKTARI.

Dr Jonathan Tobin
DAKTARI wa klabu ya Bolton Wanderers Jonathan Tobin amebainisha kuwa mchezaji wa klabu hiyo Fabrice Muamba katika dakika 78 toka alipozirai uwanjani ni kama likuwa amekufa. Jopo la madaktari wanaomtibu mchezaji huyo katika Hospitali ya London Chest nchini Uingereza wamesema kuwa kwasasa bado ni mapema mno kutabiri kama ataweza kucheza soka tena. Lakini Tobin amesema kuwa ameshangazwa na jinsi mchezaji mwenye umri wa miaka 23 alivyoweza kupata nafuu mpaka muda huu. Akihojiwa kwa masikitiko Tobin aliendelea kusema kuwa wao wenyewe hawakutegemea kama mchezaji huyo anaweza kupata nafuu kama aliyonayo sasa kwani fikra zao zilikuwa zimewaza mengine kabisa. Amesema kuwa walijitahidi kuinua moyo wa Muamba ili ufanye kazi mara moja uwanjani na mara nyingine wakati akipelekwa katika gari la wagonjwa na akiwa katika gari hilo walijaribu karibu mara 12 lakini hawakufanikiwa kuustua moyo wake. Moyo wa Muamba ulianza kufanya kazi akiwa hospitalini baada ya dakika 78 toka usimame kufanya kazi hivyo ni kama maajabu lakini jambo muhimu ni jinsi alivyopata huduma ya kwanza mara tu alipoanguka uwanjani na kuzirai na majaribio yaliokuwa yakifanywa kuamsha moyo wake.

REAL MADRID YAVUTWA SHATI TENA, HUMU MOURINHO NA OZIL WAKIPEWA RED CARD.

Wednesday, March 21, 2012

TAARIFA KUTOKA TFF LEO.

FAINALI DARAJA LA KWANZA KUCHEZWA MOROGORO
Mji wa Morogoro ndiyo utakaokuwa mwenyeji wa kituo cha Fainali ya Tisa Bora ya Ligi Daraja la Kwanza kuwania nafasi tatu za kucheza Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2012/2013 itakayoanza Machi 31 mwaka huu. Chama cha Mpira wa Miguu wa Morogoro (MRFA) ni baadhi ya vyama vya mikoa vilivyokuwa vimeomba kuwa mwenyeji wa fainali hizo huku chenyewe kikitimiza sehemu kubwa ya vigezo vilivyowekwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Vyama vingine vya mpira wa miguu vilivyokuwa vimeomba kuwa mwenyeji wa fainali hizo zinazoshirikisha timu tisa vilikuwa vya mikoa ya Mbeya, Mwanza, Ruvuma na Tabora. Fainali hizo zitafanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini humo chini ya usimamizi wa TFF. Timu zilizofuzu kucheza hatua ya fainali kutoka kundi A ni Polisi ya Dar es Salaam, Mgambo Shooting ya Tanga na Transit Camp ya Dar es Salaam. Kundi B ni Mbeya City Council, Mlale JKT ya Ruvuma na Tanzania Prisons ya Mbeya wakati kundi C ni Polisi ya Tabora, Polisi ya Morogoro na Rhino Rangers ya Tabora. Wakati huo huo, mechi kati ya Temeke United na Small Kids kupata timu moja ambayo itakabaki Ligi Daraja la Kwanza na nyingine itakayoshuka itachezwa Machi 31 mwaka huu Uwanja wa Jamhuri, mjini Dodoma. Kamati ya Ligi ya TFF iliyokutana Machi 12 mwaka huu iliamua timu hizo ambazo zilishika nafasi ya mwisho katika makundi yao ya A na B zicheze ili kupata moja itakayoungana na AFC ya Arusha na Manyoni SC ya Singida kushuka daraja. AFC na Manyoni tayari zimeshuka kutokana na kushindwa kucheza mechi zao za ligi hiyo katika hatua ya makundi. Kwa mujibu wa Kanuni ya 4 ya Ligi Daraja la Kwanza timu tatu zitashuka daraja. Baada ya kumalizika hatua ya kwanza ya ligi hiyo, timu tisa zimefanikiwa kucheza fainali wakati nyingine tano za Burkina Faso ya Morogoro, Morani ya Manyara, Polisi ya Iringa, Majimaji ya Songea na Green Warriors (94KJ) ya Dar es Salaam zimefanikiwa kubaki Ligi Daraja la Kwanza.

FAINALI UEFA CHAMPIONS LEAGUE 2013/14 KUPIGWA ESTADIO DA LUZ, LISBON, URENO.

Estadio da Luz
KAMATI ya Utendaji ya Shirikisho la Soka barani Ulaya-UEFA limeuteua Estadio da Luz au Uwanja wa Taa uliopo katika jiji la Lisbon, Ureno kutumika mchezo wa fainali ya Kombe la Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu wa 2013-2014. Kwa mara ya mwisho jiji hilo kuandaa fainali hiyo ilikuwa ni mwaka 1967 enzi hizo kombe hilo likiitwa Kombe la Ulaya mwaka 1967 ambapo Celtic iliichabanga Inter Milan mabao 2-1 katika mchezo wa fainali ya michuano hiyo. Fainali za Ligi ya Ulaya au Europa League msimu wa mwaka 2013-2014 itafanyika katika jiji la Turin nyumbani kwa timu ya Juventus ya Italia ambapo fainali hiyo itwapigwa katika uwanja mpya wa klabu hiyo ambao umefunguliwa mapema msimu huu. Wakati michuano ya Kombe la Mataifa ya Ulaya mwaka 2015 kwa vijana chini ya umri wa miaka 21 itafanyika Jamhuri ya Czech.

COYLE AZUNGUMZA NA MUAMBA.

MENEJA wa klabu ya Bolton Wanderers Owen Coyle amesema amezungumza kwa ufupi na mchezaji Fabrice Muamba mwa mara ya kwanza toka alipopoteza fahamu Jumamosi iliyopita kutokana na matatizo ya moyo. Mchezaji huyo amelazwa katika Hospitali ya London Chest baada ya kuanguka na kupoteza fahamu katika mchezo baina ya timu hiyo na Tottenham Hotspurs wa robo fainali ya Kombe la Chama cha Soka nchini Uingereza-FA. Coyle amesema kuwa mchezaji huyo bado ana safari ndefu ya kupona kabisa lakini maendeleo yake yanatia moyo ukilinganisha na hali aliyokuwa nayo Jumamosi wakati tukio hilo lilipotokea. Madaktari wanaomhudumia Muamba ambaye ameshawahi kucheza katika kikosi cha timu ya taifa ya Uingereza cha vijana chini ya umri wa miaka 21 wamesema kuwa hali yake inaendelea vizuri ingawa bado wataendelea kumuangalia kwa karibu ili kujua maendeleo yake.

MESSI, FROM SCRAWNY KID TO WORLD'S BEST.

MSHAMBULIAJI wa kimataifa kutoka Argentina Lionel Messi amefanikiwa kuwa mfungaji bora wa kihistoria wa klabu ya Barcelona baada ya kuisaidia timu hiyo kushinda mabao 5-3 katika mchezo wa Ligi Kuu nchini Hispania dhidi Granada huku yeye akifunga mabao matatu-hat trick katika mchezo huo. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo meneja wa timu hiyo Pep Guardiola amesema kuwa mchezaji huyo anastahili kila kitu ambacho mwanasoka anatakiwa kuwa nacho na amefanya hivyo kila baada ya siku tatu kwa kuonyesha kiwango cha kipekee. Messi ambaye katika mchezo alifunga hat trick yake ya 18 toka aanze kuichezea klabu hiyo na kupelekea kuvunja rekodi ya nyota wa zamani wa klabu hiyo Cecar Rodriguez aliyefunga mabao 232 rekodi ambayo imedumu kwa muda wa miaka 57. 
Wakati Rodriguez akiweka rekodi hiyo ndani ya miaka 13 kuanzia mwaka 1942 mpaka 1955, Messi ambaye ana umri wa miaka 24 sasa ametumia misimu nane tu aliyochezea Barcelona kuvunja rekodi hiyo. Messi ambaye pia ni mwanasoka bora wa dunia mara tatu mfululizo sasa amefikisha mabao 54 kwenye mashindano yote aliyocheza msimu huu yakiwemo mabao matano aliyoshinda na kuweka rekodi nyingine katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya wiki mbili zilizopita ambapo kwasasa amemzidi hasimu wake Cristiano Ronaldo mabao mawili.

HAT TRICK ALIYOPIGA MESSI DHIDI YA GRANADA NA KUVUNJA REKODI YA CESAR RODRIGUEZ BARCELONA.

MESSI MFUNGAJI WA KIHISTORIA BARCELONA.

1. Lionel Messi (Argentina) 2005- 234
2. Cesar Rodriguez (Spain) 1942-55 232
3. Ladislao Kubala (Hungary) 1951-61 194
4. Josep Samitier (Spain) 1919-32 178
5. Josep Escola (Spain) 1934-49 167
6. Paulino Alcantara (Philippines) 1912-27 137
7. Angel Arocha (Spain) 1926-33 134
8. Samuel Eto'o (Cameroon) 2004-09 130
9. Rivaldo (Brazil) 1997-02 130
10. Mariano Martin (Spain) 1940-48 124
*Alcantara scored 357 goals in total for Barcelona, but over 200 of those strikes came in friendly matches

Tuesday, March 20, 2012

RONALDO AITAMANI NAFASI YA URAIS CBF.

NYOTA wa zamani wa Brazil Ronaldo de Lima ambaye kwasasa ni mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya Kombe la Dunia nchini Brazil 2014 ameonyesha nia ya kugombania nafasi ya urais wa Shrikisho la Soka nchini humo. Akinukuliwa na gazeti maarufu nchini humo liitwalo Folha de Sao Paulo Ronaldo amesema kuwa angependa kuanza zake za kisiasa katika soka na anahitaji kuongoza soka hivi sasa baada ya kucheza kwa kipindi kirefu. Aliyekuwa rais wa CBF Ricardo Teixeira ambaye ameliongoza shirikisho hilo kuanzia mwaka 1989 alijiuzulu wadhifa wake huo kutokana na matatizo ya kiafya na pia alijiuzulu nafasi ya ujumbe katika kamati ya maandalizi ya nchi hiyo. Katika kipindi cha miaka 22 ambacho Teixeira ameliongoza shirikisho hilo alikuwa amejitahidi kukuza soka la nchi hiyo lakini katika kipindi cha karibuni kabla ya kujiuzulu CBF imekuwa ikikumbwa na shutuma mbalimbali za uadilifu. Ronaldo ambaye alikiongoza kikosi cha nchi hiyo kunyakuwa taji la Kombe la Dunia mwaka 2002 amesema kuwa hajajua kama atakuwa mgombea wa nafasi ya urais lakini kama CBF wakimhitaji kufanya hivyo atakubali kugombea.

25 WAITWA KAMBINI TWIGA STARS.

Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Wanawake (Twiga Stars), Charles Boniface Mkwasa ametaja kikosi cha wachezaji 25 kitakachoingia kambini Machi 25 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya program yake ya maandalizi kabla ya mechi dhidi ya Ethiopia. Wachezaji walioitwa kambini ni Amina Salum (Lord Baden Sekondari, Pwani), Asha Rashid (Mburahati Queens), Aziza Mwadini (New Generation, Zanzibar), Esther Mayala (Street Girls, Mwanza), Evelyn Senkubo (Mburahati Queens), Fadhila Hamad (Uzuri Queens) na Fatuma Bashiri (Simba Queens). Wengine ni Fatuma Gotagota (Mburahati Queens), Fatuma Khatib (Mburahati Queens), Fatuma Mustafa (Sayari), Fatuma Omari (Sayari), Hanifa Idd (Uzuri Queens), Maimuna Said (JKT), Mwajuma Abdallah (JKT), Mwanahamisi Omari (Mburahati Queens) na Mwanaidi Khamis (Uzuri Queens). Mwapewa Mtumwa (Temeke), Rukia Khamis (Sayari), Semeni Abeid (Tanzanite), Siajabu Hassan (Evergreen), Tatu Salum (Makongo Sekondari), Upendo Jeremiah (Pangani, Tanga), Veneranda Mbano (Tanzanite), Zena Khamis (Mburahati Queens) na Zena Said (Uzuri Queens).

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF.

MKUTANO MKUU TFF APRILI 21
Mkutano Mkuu wa kawaida wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) uliokuwa ufanyike Machi 24 na 25 mwaka huu jijini Dar es Salaam umesogezwa mbele hadi Aprili 21 na 22 mwaka huu. Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana Machi 10 mwaka huu jijini Dar es Salaam chini ya uenyekiti wa Rais Leodegar Tenga uliamua kusogeza mbele Mkutano Mkuu kutokana na mtiririko wa matukio ndani ya TFF katika kipindi hicho. Ajenda katika Mkutano Mkuu huo wa kawaida wa TFF kufungua kikao, kuthibitishwa kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu, kuthibitisha muhtasari wa Mkutano Mkuu uliopita, yatokanayo na muhtasari wa kikao kilichopita, hotuba ya Rais, kupokea taarifa za utekelezaji za wanachama na kupokea taarifa ya utekelezaji ya Kamati ya Utendaji. Nyingine ni kupitisha taarifa ya ukaguzi wa hesabu za mwaka uliopita, kupitisha taarifa ya wakaguzi wa hesabu na hatua zilizochukuliwa, kupitisha bajeti ya mwaka 2012, kupitisha mapendekezo ya marekebisho ya Katiba ya TFF, kujadili mapendekezo yaliyowasilishwa na Wanachama au Kamati ya Utendaji, mengineo na kufunga kikao.

MTIBWA SUGAR, SIMBA ZAINGIZA MIL 31/-

Mechi namba 146 ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Mtibwa Sugar na Simba iliyochezwa Machi 18 mwaka huu Uwanja wa Jamhuri, Morogoro imeingiza sh. 31,230,000. Jumla ya watazamaji 10,410 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 3,000. Baada ya kuondoa gharama za awali za mchezo na asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ni sh. 4,763,898.31 kila timu ilipata sh. 6,508,230.51, uwanja sh. 2,169,410.17.  Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Morogoro (MRFA) sh. 867,764.07, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 2,169,410.17, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,084,705.08, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) sh. 216,941.02 na asilimia 10 ya gharama za mechi sh. 2,169,410.17. Gharama za awali za mechi zilikuwa nauli ya ndani kwa waamuzi sh. 10,000, nauli ya ndani kwa kamishna wa mchezo sh. 10,000. mwamuzi wa akiba sh. 30,000, posho ya kujikimu kwa waamuzi sh. 120,000 na tiketi sh. 2,480,000.  Gharama nyingine ni Jichangie ambayo ni sh. 200 kwa kila tiketi; kila klabu ilipata sh. 728,700 wakati Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Morogoro (MRFA) kilipata sh. 624,600.

VILLA, JKT KUHITIMISHA RAUNDI YA 21 MACHI 21

Mzunguko wa 21 wa Ligi Kuu ya Vodacom unakamilika Machi 21 mwaka huu kwa mechi namba 147 kati ya Villa Squad na JKT Ruvu itakayochezwa Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Machi 24 mwaka huu kutakuwa na mechi ya ligi hiyo kati ya Moro United na African Lyon. Mechi hiyo namba 149 itafanyika Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Mechi za Machi 28 mwaka huu ni Ruvu Shooting Stars itakayocheza na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mabatini mjini Mlandizi wakati Moro United itakuwa mwenyeji wa Villa Squad katika mechi namba 153 itakayofanyika Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.

35 ES SETIF KUWASILI MACHI 21

Kikosi cha watu 35 cha timu ya ES Setif ya Algeria kinatarajiwa kuwasili nchini kesho (Machi 21 mwaka huu) saa 12 alfajiri kwa ndege ya EgyptAir kwa ajili ya mechi ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Simba itakayochezwa Machi 25 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Msafara huo una wachezaji, benchi la ufundi, viongozi wa timu, kiongozi wa msafara kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu la Algeria (FAF) wakati watatu ni waandishi wa habari. Wachezaji 20 katika msafara huo ni Mohamed Benhamou, Sofiane Bengorine, Riadh Benchadi, Smain Diss, Farouk Belkaid, Khaled Gourmi, Mourad Delhoum, Said Arroussi, Mokhtar Benmoussa, Tarek Berguiga, Mohamed Aoudi na Amir Karaoui. Wengine ni Mohamed El Amine Tiouli, Racid Ferrahi, Youcef Ghezzali, Youssef Sofiane, Mokhtar Megueni, Rachid Nadji, Abderrahmane Hachoud na Akram Djahnit. Kocha wa timu hiyo ni Alain Norbert Geiger ambaye ni raia wa Uswisi.




MESSI KINARA WACHEZAJI WANAOLIPWA ZAIDI DUNIANI.

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Barcelona Lionel Messi ndiye mchezaji wa mpira anayelipwa zaidi duniani akifuatiwa na David Beckham wa Uingereza na Cristiano Ronaldo wa Ureno. Messi ambaye anacheza katika klabu ya Barcelona anakunja kitita cha euro milioni 33 ikiwemo euro milioni 10.5 za mshahara wake, euro milioni 1.5 kama motisha na euro milioni 21 za matangazo na mikataba mingine. Kiungo wa zamani wa Manchester United ambaye kwasasa anakipiga katika klabu ya Los Angeles Galaxy ya Marekani, David Beckham anakunja kitita cha euro milioni 31.5 sehemu kubwa ya fedha hizo ambazo ni kiasi cha euro milioni 26 za matangazo na mikataba mbalimbali ambayo amesaini. Ronaldo ambaye ni mshambuliaji wa klabu ya Real Madrid anashika nafasi ya tatu katika orodha orodha ya wachezaji wanaolipwa zaidi kwa kujikusanyia kiasi cha euro 29.2, ambapo euro milioni 13 ni za mshahara wake kwa mwaka na euro milioni 15.5 ni matangazo na mikataba mingine mbalimbali.

WAJUE MAKOCHA WANAOLIPWA PESA NYINGI ZAIDI DUNIANI.

MENEJA wa klabu ya Real Madrid Jose Mourinho ndiye kocha anayelipwa hela nyingi zaidi duniani kwa mujibu wa orodha iliyotolewa na gazeti moja la michezo nchini Ufaransa. Mourinho ambaye pia amewahi kuinoa klabu ya Chelsea ya nchini Uingereza kwa mwaka anakusanya kiasi cha euro milioni 14.8 wakati makocha wawili ambao nao pia wamewahi kuinoa Chelsea pia wamo katika orodha hiyo. Katika orodha hiyo Carlo Ancelotti ambaye anainoa klabu ya Paris Saint-Germain ya Ufaransa ndiye anashika nafasi ya pili katika makocha wanaolipwa zaidi akikunja kiasi cha euro milioni 13.5 kwa mwaka akifuatiwa na Pep Guardiola katika nafasi ya tatu akikunja kiasi cha euro 9.5. 
Meneja wa Arsenal Arsene Wenger ndiye anashika nafasi ya nne katika orodha hiyo akipokea kiasi cha euro milioni tisa akifuatiwa na Guus Hiddink ambaye kwasasa anakinoa kikosi cha Anzhi Makhachkala yeye anapokea euro 8.6 kwa mwaka. Wengine ni meneja wa zamani wa timu ya taifa ya Uingereza Fabio Capello ambaye anaweka kibindoni kiasi cha euro milioni 8.5 akifuatiwa na Sir Alex Ferguson ambaye anakunja kitita cha euro milioni nane. Pia wapo Dick Advocaat kocha timu ya taifa ya Urusi euro milioni saba, Antonio Camacho kocha timu ya taifa ya China euro milioni 6.1 na orodha hiyo inafungwa na kocha wa Manchester City Roberto Mancini ambaye anakunja kitita cha euro milioni 5.9.

MUAMBA AANZA KUTAMBUA NDUGU.

KIUNGO wa klabu ya Bolton Wanderers Fabrice Muamba ameanza kupumua bila kutumia msaada wa mashine na ameanza kutambua baadhi ya watu wa karibu wa familia yake hivyo kuonyesha dalili za kupona baada ya moyo wake kushindwa kufanya kazi ghafla Jumamosi. Kiungo huyo huyo wa kimatiga kutoka Congo ambaye ana umri wa miaka 23 alianguka uwanjani muda kidogo kabla ya mapumziko wakati wa mchezo baina ya timu yake na Tottenham Hotspurs ambapo juhudi za kuuzindua moyo wake hapo uwanjani zilishindikana na kupelekea kukimbizwa hospitalini. Kwa mujibu wa taarifa ya madaktari moyo wa Muamba ulianza kufanyakazi baadae akiwa hospitalini hapo na kuendelea kuwekwa chini ya uangalizi maalumu huku akitumia mashine za kumsaidia kupumua kwa muda wa siku mbili. Lakini mchezaji huyo hali yake iliendelea vizuri hadi jana ambapo madaktari wanaomtibu wamesema kuwa hali yake imetengemaa ilipofika jana jioni lakini bado ataendelea kuwepo hospitalini hapo mpaka hapo madaktari watapojiridhisha kwamba amepona kabisa. Mchumba wa mchezaji huyo ambaye alimchumbia wakati wa sherehe za wapendanao Februari mwaka huu aitwae Shauna Muamba amewashukuru watu wote waliokuwa wakimuombea mchumba wake huyo kwani maombi yao yamesikilizwa, aliandika Shauna katika mtandao wa kijamii wa twitter.

Sunday, March 18, 2012

KLINSMANN AICHOMOLEA TOTTENHAM.

KOCHA Mkuu wa timu ya taifa ya Marekani Jurgen Klinsmann amesema hawezi kuachia nafasi yake hiyo kwenda Uingereza kuifundisha klabu ya Tottenham Hotspurs. Meneja wa sasa wa Tottenham Harry Redknapp ndio anapewa nafasi kubwa ya kuwa kocha mpya wa timu ya taifa ya Uingereza baada ya aliyekuwa kocha wa klabu hiyo Fabio Capello kujiuzulu Februari mwaka huu. Pamoja na klabu hiyo kumuweka kocha huyo katika orodha ya watu ambao watamrithi Redknapp kama akiondoka, Klinsmann ambaye amewahi kuitumikia klabu hiyo katikati ya miaka ya 90 amesisitiza kuwa hana mpango wa kuondoka Marekani kwasasa. Klinsmann alipewa mikoba ya kuinoa timu ya Marekani katika mkataba wa miaka mitatu akichukua nafasi ya Bob Bradley Julai mwaka jana.

VIBIBI KIZEE VYA TURIN VYAZINDUKA.

TIMU ya Juventus maarufu kama Kibibi kizee cha Turin jana ilimaliza ukame wa kucheza michezo minne bila ushindi baada ya kuigaragaza bila ya huruma Fiorentina kwa mabao 5-0. KIBIBI kizee cha Turin, Juventus jana kilizima gundu la kucheza mechi nne bila ya kushinda, baada ya kuirarua 5-0 Fiorentina, ambayo ilicheza zaidi ya saa moja na wachezaji 10. Ikiwa bado haijafungwa msimu huu, Juventus iko nafasi ya pili ikiwa inazidiwa pointi nne na vinara AC Milan baada ya vinara hao kushinda 2-0 dhidi ya Parma, mabao ya Zlatan Ibrahimovic kwa penalti na Urby Emanuelson. Milan, ambayo ilimuingiza uwanjani Gennaro Gattuso mwishoni mwa mchezo kwa mara ya kwanza tangu apate matatizo ya macho Septemba, mwaka jana sasa ina pointi 60 kutokana na mechi 28.

Mabao ya Juventus yalifungwa na Mirko Vucinic dakika ya 5, Chilean Arturo Vidal kabla ya mapumziko, Claudio Marchisio, Andrea Pirlo Simone Padoin walifunga mabao mengine

MESSI, XAVI WAIPAISHA BARCELONA.

MABAO ya Xavi aliyefunga kwa mpira wa adhabu na lingine la Lionel Messi yalitosha kuipa Barcelona ushindi wa 2-0 jana dhidi ya Sevilla na kupunguza idadi ya alama wanazozidwa na Real Madrid. Xavi alipiga bao hilo dakika ya 18 na Mwanasoka Bora wa Dunia, Messi akafunga bao lake la 31 kwenye La Liga msimu huu baadaye kidogo. Mabingwa hao watetezi sasa wana pointi 63 kutokana na mechi 27, wakati Jose Mourinho ameiweka kileleni kwa mbali Real, yenye pointi 70 na leo inaweza kutudisha pointi 10 za kuizidi Barca iwapo itashinda dhidi ya Malaga Uwanja wa Bernabeu. Katika mechi nyingine, Osasuna ilipanda hadi nafasi ya tano kwa kufikisha pointi 39 baada ya kupata bao la kusawazisha dakika za lala salama na kufanya sare ya 1-1 na Real Zaragoza.

Rayo Vallecano ilipanda hadi nafasi ya nane kwa kufikisha pointi 37 baada ya kuifunga Real Betis 3-0. Zaragoza inabakiwa nafasi ya 20 kwa pointi zake 19.

REACTION TO MUAMBA COLLAPSE.

Bolton Wanderers midfielder Fabrice Muamba was critically ill in hospital after collapsing on the pitch during the FA Cup quarterfinal at Tottenham Hotspur on Saturday.

Players, clubs and fans showed their support for Muamba on Twitter.

Tottenham manager Harry Redknapp:
"Praying for Fabrice Muamba. A very very sad day. Hope the young lad pulls through."

Arsenal captain Robin van Persie:
"I'm so sad about what happened to Fabrice Muamba today. Played with him 4 a couple of years. What a great guy. Always a smile on his face."

Former Bolton goalkeeper Ali Al-Habsi:
"All our hearts with Fabrice Muamba, one of my closest friends at Bolton.. Im shocked, wishing him a fast recovery."

Juventus midfielder Andrea Pirlo dedicated his side's 5-0 win over Fiorentina to Muamba:
"He's our colleague, we pray he gets well soon."

Barcelona midfielder and former Arsenal captain Cesc Fabregas:
"My thoughts are with Fabrice and his family. Stay strong mate. Our prayers are with you."

Manchester United and England striker Wayne Rooney:
"Hope Fabrice Muamba is ok. Praying for him and his family. Still in shock."

Tottenham defender Kyle Walker, who scored in the match against Bolton to make it 1-1:
"Doesn't matter who you support..Doesn't matter if you aren't a football fan. Doesn't matter if you aren't religious..Pray for Fabrice Muamba."

Manchester City captain Vincent Kompany:
"Critically ill and intensive care" I really hope that this nightmare will be soon over and I wish for Fabrice Muamba to recover fully."

Former Chelsea and Germany midfielder Michael Ballack:
"We want to send our prayers to Fabrice Muamba, his family, his friends and all at Bolton Wanderers."

Friday, March 16, 2012

CHAMPIONS LEAGUE DRAW.

TIMU ya AC Milan ya Italia imepangwa kukutana na Barcelona ya Hispania katika robo fainali ya michuano ya Kombe la Klabu Bingwa ya Ulaya. Katika droo hiyo iliyopangwa leo na Shrikisho la Soka Barani Ulaya Real Madrid itakutana kwa mara ya kwanza na timu ngeni katika hatua ya Apoel Nicosia ya Ugiriki huku Olympic Marseille ya Ufaransa nayo kwa mara kwanza itaikaribisha Bayern Munich katika mchezo wa kwanza wa michuano hiyo. Timu pekee ya Uingereza katika hatua hiyo msimu huu Chelsea wao wataanzia ugenini katika mchezo wa kwanza wakicheza na Benfica ya Ureno. Mshindi kati ya Chelsea na Benfica atakutana na mshindi kati AC Milan au Barcelona katika hatua ya nusu fainali huku mshindi kati ya Real Madrid na APOEL atakutana na mshindi kati ya Marseille na Bayern Munich kwenye hatua kama hiyo.

ABIDAL KUPANDIKIZWA INI JINGINE.

MCHEZAJI wa Barcelona Eric Abidal anatarajiwa kufanyiwa upasuaji wa kupandikiza ini katika wiki chache zijazo ambapo klabu hiyo imesema upandikizaji huo umekuja toka alipoanza matibabu mwaka mmoja uliopita. Beki huyo wa kimataifa kutoka Ufaransa aliondolewa uvimbe katika ini lake Machi 17 mwaka 2011 na kurejea uwanjani mwishoni mwa msimu huo na kuonyesha athari chache kupotea toka kipindi hicho. Abidal mwenye umri wa miaka 32 alichaguliwa kunyanyua Kombe la Klabu Bingwa Ulaya katika Uwanja wa Wembley msimu uliopita baada ya kuisaidia Barcelona kuisambaratisha Manchester United kwa mabao 3-1 katika mchezo wa fainali. Mchezaji huyo amekuwa mchezaji tegemeo wa Barcelona toka alipojiunga na klabu hiyo akitokea klabu ya Lyon mwaka 2007 ambapo kwasasa nafasi yake ya kucheza michuano ya Ulaya iko mashakani kutokani kutokana na tatizo lake hilo.

VURUGU ZAJERUHI 11 COLOMBIA.

POLISI imesema inashikilia watu 135 baada ya vurugu zilizosababisha watu 11 kujeruhiwa nchini Colombia. Mamlaka imesema leo kwamba watu watatu walikuwa wana hali mbaya sana baada ya mashabiki wa Amerika na Deportivo Cali kugombana kabla na wakati wa mchezo katika vurugu zilizoendelea hata baada ya mechi hiyo ya Copa Colombia jana mjini Cali. Mashabiki hao walizipiga licha ya kwamba pande zote mbili za mashabiki wa timu hiyo zilikubaliana amani kuelekea kwenye mchezo huo. Maofisa walisema askari Polisi mmoja alipoteza kidole chake katika mapambano hayo. Jumapili iliyopita, mtu alipigwa risasi na kufariki na wengine tisa walijeruhiwa kwa visu, baada ya mashabiki wa wapinzani wa jadi wa Medellin, Atletico Nacional na Independiente kupigana. Polisi ilisema watu 315 walikamatwa na kukamata visu zaidi ya 450 wakati huo

PIQUE AFUTIWA MASHTAKA.

MAMLAKA ya Soka nchini Hispania imeamua kufunga mjadala wa malalamiko ya kamati ya waamuzi dhidi ya beki wa Barcelona Gerrard Pique wakimtuhumu kumshambulia mwamuzi baada ya kumpa kadi nyekundu. Taarifa iliyotolewa na mmoja wa viongozi wa shirikisho hilo imesema kuwa Kamati ya Mashindano imeamua kufunga mjadala huo wa kamati wa waamuzi dhidi ya Pique. Shirikisho hilo tayari limemfungia mchezaji huyo mchezo mmoja na faini ya euro 600 baada yak umjia juu mwamuzi katika mchezo baina ya timu yake na Sporting Gijon uliochezwa Machi 13 mwaka huu. Kamati hiyo inayowakilisha waamuzi ilitoa malalamiko yao kuhusu kauli ya Pique akimlenga mwamuzi Velasco Carballo ambaye alichezesha mchezo huo ambapo timu yake Barcelona ilituma barua ya kumtete mchezaji huyo kupinga kuwa mchezaji huyo alimdhalilisha mwamuzi. Pique alitolewa nje baada ya kumchezea vibaya Miguel De Las Cuevas dakika ya 47 mchezo ambao Barcelona ilishinda kwa mabao 3-1 dhidi Gijon.

Manchester City vs Sporting Lisbon 3-2 All Goals Highlights Full Match 1...

Athletic Bilbao vs Manchester United 2-1 - All Goals and Highlights 15....

Thursday, March 15, 2012

DAVE RICHARDS SORRY FOR COMMENTS ABOUT UEFA AND FIFA.

MWENYEKITI wa Ligi Kuu nchini Uingereza Sir Dave Richards amelituhumu Shirikisho la Soka Duniani-FIFA na Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA kuwaibia haki yao ya kuwa nchi ambayo soka liligunduliwa kwa mara ya kwanza. Katika mkutano uliofanyika Qatar Richards ambaye baadae alijiumiza mwenyewe baada yakuteleza kwenye ngazi amesema kuwa dunia inabidi iishukuru nchi ya Uingereza kwa kuanzisha mchezo huo. Richards aliendelea kusema kuwa nchi ndio iliwapa dunia mchezo wa mpira lakini miaka 50 baadae mtu anakuja kusema kuwa ni uongo na kutunyang’anya haki hiyo ambapo alidai mtu huyo ni FIFA. Richards ambaye ni mjumbe wa bodi ya Chama cha Soka nchini Uingereza-FA alizungumza hayo mbele ya Makamu wa Rais wa FIFA Ali Bin Hussein wa Jordan na Ofisa Mkuu wa Baraza la Kimatifa la Kriketi Haroon Lorgat. Kauli ya Richards imekuja wakati wa mapendekezo yaliyotolewa kuwa mchezo wa soka umeanzia nchini China. Richards amesema kuwa mchezo wa soka umeanzia katika kitongoji cha Shiffield miaka 150 iliyopita na Uingereza ndio iliyoandika sheria na kuzitoa duniani kote hivyo hadhani kama ni halali China kupewa haki hiyo. Kauli ambayo baadae aliomba msamaha kutokana na kauli yake hiyo.

PELE KUWEPO MKUTANO WA USULUHISHI, FIFA NA SERIKALI YA BRAZIL.

NGULI wa soka wa zamani wa Brazil Pele anatarajiwa kujiunga na Rais wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA Sepp Blatter pamoja na rais wa nchi hiyo Dilma Rousseff katika mkutano wa usuluhishi unaotarajiwa kufanyika kesho. Blatter anatarajiwa kusafiri kuelekea Brasilia ambao ndio mji mkuu wa Brazil kujaribu kurekebisha tofauti baada ya Katibu Mkuu wa FIFA Jerome Valcke kuchafua hali ya hewa baada ya kutoa kauli kuhusu maandalizi ya nchi hiyo ya Kombe la Dunia ambayo iliwaudhi. Katika taarifa yake Blatter amesema kuwa anafurahishwa kuwepo kwa nguli huyo wa soka katika mkutano huo ambapo wanatarajia kuzungumzia pia sula la maandalizi na kitu gani kinahitajika kufanywa katika miezi hii michache ya maandalizi iliyobakia. Taarifa hiyo imekuja ikiwa ni siku mbili tu toka aliyekuwa rais wa Shirikisho la Soka la nchi hiyo Ricardo Teixeira kujiuzulu kutokana na matatizo ya kiafya, Pele alikuwa na uhusiano usiokuwa mzuri na Teixeira ambaye alishindwa hata kumualika katika droo ya kupanga timu zitakazowania tiketi ya kushiriki michuano ya Kombe la Dunia. Hatahivyo baadae Rousseff alimteua Pele kuwa balozi wa Kombe la Dunia wa nchi hiyo.

CASILLAS KUFUNGA NDOA NA CARBONERO.

GOLIKIPA wa klabu ya Real Madrid Iker Casillas anatarajiwa kufunga ndoa na rafiki yake wa kike wa muda mrefu Sara Carbonero Julai mwaka huu baada ya michuano ya Kombe la Ulaya. Casillas mwenye umri wa miaka 30 na Carbonero ambaye ana miaka 28 wamekuwa pamoja katika kipindi ccha miaka mitatu sasa ambapo nahodha huyo wa klabu ya Madrid ameshamchumbia rafiki yake huyo zaidi ya mara moja. Gazeti moja la habari za udaku nchini humo lilidai katika kipindi chote ambacho Casillas amekuwa akimchumbia binti huyo amekuwa akikataa lakini mwishoni sasa amekubali ingawa hakuna taarifa zaidi kuhusiana na suala hilo. Wawili hao wote wanatarajiwa kuwepo nchini Poland na Ukraine kuanzia June 8 mpaka Julai 1 ambapo kutafanyika michuano hiyo ambayo Casillas anatarajiwa kuwepo langoni ili kukiongoza kikosi chake kutetea ubingwa huo ambao waliutwaa mwaka 2008, huku Carbonero yeye atakuwa akitangaza michuano hiyo katika moja ya televisheni za binafsi nchini Hispania.

Chelsea 4-1 Napoli All Goals And Highights 14/03/2012

Real Madrid vs CSKA Moscow 4-1 - All Goals & Highlights - 14/3/2012

Wednesday, March 14, 2012

NEW HEAD OF BRAZILIAN FOOTBALL WANTS FEW CHANGES.

Jose Maria Marin
KIONGOZI mpya wa Shrikisho la Soka la Brazil aliyechukua madaraka hayo jana ameahidi kufanya mabadiliko machache licha ya mara nyingi utawala wa aliyemtangulia Ricardo Teixeira kukumbwa na utata. Jose Maria Marin ambaye ni mwanasiasa ndiye aliyechukua nafasi ya Teixeira ambaye alijiuzulu Jumatatu kutokana na matatizo ya kiafya aliyonayo baada ya kuongoza shirikisho hilo kwa miaka 23. Akizungumza mara baada ya kuchukua wadhifa huo Marin amesema kuwa uongozi wa Teixeira ni wa kuigwa kwakuwa amefanya soka la nchi hiyo kutambuliwa duniani kutokana na juhudi zake. Teixeira alifufua shirikisho hilo katika kipindi chake lakini pia alikuwa akituhumiwa na rushwa na ukiukwaji wa wa taratibu katika uongozi wake. Marin ambaye ana umri wa miaka 79 ataliongoza shirikisho hilo mpaka mwishoni mwa 2014 baada ya Kombe la Dunia ambalo nchi hiyo ndio itakuwa mwenyeji ambapo ameajidi kuwa tayari kwa mazungumzo na serikali ili kuhakikisha maandalizi ya michuano hiyo yanakwenda kama yalivyopangwa.