Thursday, March 28, 2013

FIFA KUCHUNGUZA TUKIO LA SUAREZ.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA linaangalia tukio la ugomvi lililomhusisha mshambuliaji nyota wa Liverpool Luis Suarez katika mchezo baina ya timu yake ya taifa ya Uruguay na Chile Jumanne iliyopita. Tukio hilo lilitokea wakati mchezaji wa Chile Gonzalo Jara alipokuwa amekabana na Suarez na baadhi picha zinamuonyesha mchezaji huyo akimpiga ngumi kwa makusudi Jara ambaye anacheza katika klabu ya Nottingham Forest. Wawili hao walionekana kujibizana maneno baada ya tukio hilo lakini mwamuzi Nestor Pitana aliyechezesha pambano hilo hakuchukua hatua yoyote. Katika taarifa yake FIFA wamedai kuwa bado wanakusanya taarifa za mchezo huo huku wakisubiri nyingine kutoka kwa waamuzi ambazo zitawasilishwa katika muda wa saa 24. Suarez na Jara ambaye ancheza kwa mkopo Forest akitokea klabu ya West Bromwich walikuwa wakigombea nafasi katika eneo la hatari katika mchezo huo huo wa kufuzu michuano ya Kombe la Dunia ambao Chile ilishinda kwa mabao 2-0.

No comments:

Post a Comment