Thursday, June 12, 2014

KOMBE LA DUNIA HILOOO.....

MICHUANO ya Kombe la Dunia inatarajiwa kuanza kutimua vumbi rasmi leo jioni kwa wenyeji Brazil kuanza kupepetana na Croatia. Michuano hiyo itakayodumu kwa muda wa mwezi mmoja, itashuhudia mataifa 32 yakichuana katika kugombea nafasi ya kucheza fainali itakayofanyika Julai 13 jijini Rio de Janeiro. Mchezo huo wa ufunguzi utakaochezwa katika Uwanja wa Corinthians uliopo jijini Sao Paulo utatanguliwa na sherehe fupi ambazo zitakuwa na maonesho mbalimbali kuelezea uhalisia wa watu wa nchi hiyo na soka. Akihojiwa jana kocha wa timu ya taifa ya Brazil, Luis Felipe Scolari aliwaambia wapenzi wote wa soka kwamba muda umefika, wanatakiwa kwenda pamoja kwasababu hilo ni Kombe lao la Dunia. Pamoja na shamrashamra za kuanza michuano hiyo, mwaka jana zaidi ya watu milioni moja waliingia mtaani katika miji mikubwa kwa ajili ya kuandamana kupinga kile walichokiita gharama kubwa za maandalizi ya michuano hiyo. Hata hivyo safari hii, rais wa Brazil Dilma Rousseff amesema hataruhusu maandamano kwa ajili ya kufuruga michuano hiyo ambapo maelfu ya polisi na wanajeshi wamepangwa ili kuhakikisha michuano hiyo inakwenda vyema.

No comments:

Post a Comment