Wednesday, May 30, 2012

WAZIRI MKUU WA ITALIA ASHAMBULIWA KWA KAULI YAKE.

Maurizio Zamparini.
WAZO lililotolewa na Waziri Mkuu wa Italia, Mario Monti la kusimamisha Ligi Kuu ya nchi hiyo kwa miaka kadhaa kutokana na sakata ya rushwa linaloikabili limepingwa vikali na viongozi wa vilabu pamoja na viongozi wa Shirikisho la Soka nchini humo. Vyombo vya habari nchini humo vilimnukuu rais wa klabu ya Palermo, Maurizio Zamparini akimshambulia Monti kuwa natakiwa kuona haya kwa kauli yake alitoa. Zamparini ambaye alikataa kuingia katika masuala ya kisiasa baada ya kuombwa kufanya hivyo ni mmoja wa waanzilishi wa chama cha kulinda haki za raia nchini humo. Kauli hiyo ya Zamparini imekuja kufuatia Monti kukaririwa akisema kuwa ligi hiyo inastahili kusimamishwa kwa muda wa miaka miwili au mitatu kutokana na tuhuma za rushwa na masuala ya upangaji matokeo unaoiandama ligi hiyo toka mwaka jana. Mamia ya wachezaji na viongozi wa vilabu wamekamatwa katika awamu ya tatu ya msako wa watu wanaotuhumiwa na masuala ya rushwa na upangaji matokeo shughuli ambayo imefanyika wiki hii. Zamparini amesema kuwa kauli ya Monti ni upuuzi na anaonekana kama anatapatapa kutokana na kuingilia mambo yasiyomhusu akisahau suala muhimu la kushughulikia mdororo wa kiuchumi unaolikabili taifa hilo hivi sasa.

No comments:

Post a Comment