Tuesday, September 25, 2012

TAARIFA KUTOKA TFF LEO.

LIGI KUU VODACOM KUENDELEA KESHO
Michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Septemba 26 mwaka huu) kwa mechi mbili zitakazochezwa katika miji ya Tanga na Morogoro. Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Polisi Morogoro na Toto Africans ya Mwanza. Polisi Morogoro ambayo imepanda daraja msimu huu imeshacheza mechi tatu na kufanikiwa kupata pointi moja tu baada ya kutoka suluhu na Mtibwa Sugar katika mechi ya kwanza. Nayo Toto Africans ambayo katika mechi iliyopita ugenini ililazimisha suluhu dhidi ya Coastal Union, yenyewe ina pointi tatu baada ya kutoka sare katika mechi zote tatu ilizocheza chini ya kocha John Tegete. Mechi nyingine ya ligi hiyo itakuwa kati ya Coastal Union ambayo itaikaribisha Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Kagera Sugar inayofundishwa na Abdallah Kibaden, wikiendi iliyopita iliondoka na pointi zote tatu kwenye uwanja huo baada ya kuifunga Mgambo Shooting bao 1-0. Ligi hiyo itaingia kwenye Super Weekend kuanzia Ijumaa (Septemba 28 mwaka huu) kwa mechi kati ya Azam na JKT Ruvu itakayochezwa Uwanja wa Taifa itaoneshwa moja kwa moja (live) na kituo cha SuperSport kuanzia saa 1 kamili usiku.

No comments:

Post a Comment