Tuesday, November 20, 2012

KESI YA PARK KUSIKILIZWA LEO.

Kesi ya mchezaji soka wa kimataifa wa Korea Kusini ambaye aliyeleta msuguano wa kidiplomasia na Japan baada ya kupeperusha bango lenye maandishi ya kisiasa katika michuano ya Olimpiki iliyofanyika London, Uingereza inatarajiwa kusikilizwa tena na Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Duniani-FIFA. Kamati hiyo ambayo itaamua kama mchezaji huyo aitwaye PARK JONG-WOO atakabiliwa na adhabu ya kufungiwa kutokana na kitendo chake hicho alichokifanya mwishoni mwa mchezo wa kugombea nafasi ya tatu dhidi ya Japan, imekuwa ikishindwa kutoa uamuzi wakati ilipokutana Octoba kusikiliza kesi hiyo. Msemaji wa FIFA amesema kuwa hata kama uamuzi utafikiwa hii leo hautatangazwa kwa siku kadhaa mpaka ripoti kamili iweze kuandikwa na kutafsiriwa kabla ya kutolewa kwa wandishi wa habari. Kiungo huyo alishika bango lenye ujumbe ambao unaokumbushia tofauti za mipaka kati Korea Kusini na Japan wakati akishangilia ushindi wa mabao 2-0 waliopata dhidi ya mahasimu wao hao. PARK alizuiwa kuhudhuria sherehe za kukabidhiwa medali ya shaba waliyopata lakini Chama cha Soka cha Korea-KFA mwezi uliopita kilitoa taarifa kuwa wametumiwa ujumbe kupitia kamati ya nchi iliyoandaa michuano ya olimpiki ikithibitisha kuwa mchezaji huyo atapokea medali yake.

No comments:

Post a Comment