Wednesday, January 22, 2014

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF.

MZUNGUKO WA VPL KUANZA JUMAMOSI
Mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara unaanza Jumamosi (Januari 26 mwaka huu) kwa mechi tano katika miji ya Bukoba, Dar es Salaam, Tanga wakati mechi ya Tanzania Prisons na Ruvu Shooting inahamishiwa uwanja mwingine. Ashanti United itacheza na Yanga kwenye Uwanja wa Taifa, Coastal Union itacheza na Oljoro JKT katika Uwanja wa Mkwakwani, Tanga wakati Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Azam na Mtibwa Sugar. Jumapili (Januari 26 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya JKT Ruvu na Mgambo Shooting itakayofanyika Uwanja wa Azam Complex wakati Simba na Rhino Rangers zitaumana kwenye Uwanja wa Taifa. Mechi ya Tanzania Prisons na Ruvu Shooting iliyokuwa ichezwe Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine inahamishiwa uwanja mwingine kwa vile huo bado nyazi zake ambazo zimepangwa hivi karibuni hazijawa tayari kuhimili mechi hiyo. Hivyo Tanzania Prisons inatakiwa kutafuta uwanja mwingine unaokidhi viwango vinavyotakiwa kwa ajili ya mechi hiyo, na nyingine dhidi ya JKT Ruvu itakayochezwa Januari 29 mwaka huu. Pia matumizi ya tiketi za elektroniki yanaanza katika mzunguko huu kwa vile viwanja nane ambavyo tayari vimefungwa vifaa vya tiketi hizo. Vilevile tunakumbusha washabiki wa mpira wa miguu kuwa tiketi za elektroniki haziuzwi viwanjani.



TWIGA STARS KUIVAA ZAMBIA FEB 15 LUSAKA
Tanzania (Twiga Stars) itaivaa Zambia katika mechi ya kwanza ya raundi ya kwanza ya michuano ya mchujo ya Afrika kwa Wanawake (AWC) itakayofanyika Februari 15 mwaka huu jijini Lusaka. Mechi hiyo itafanyika kwenye Uwanja wa Nkoloma kuanzia saa 9 kamili kwa saa za Zambia na itachezeshwa na mwamuzi Salma Mukansanga kutoka Rwanda. Mukansanga atasaidiwa na Wanyarwanda wenzake; Francine Ingabire, Sandrine Murangwa na Angelique Tuyishime. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Jackey Gertse kutoka Namibia.



KISHONGOLE, KESSY KUSIMAMIA MECHI ZA CAF
Shrikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua Watanzania Alfred Rwiza Kishongole na Lina Kessy kuwa makamishna wa mechi za shirikisho hilo zitakazochezwa wikiendi ya Februari 14 mwaka huu. Kishongole ameteuliwa kusimamia mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Cote d’Or ya Shelisheli na Kabuscorp de Palanca ya Angola. Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya mchujo itafanyika Shelisheli na itachezeshwa na waamuzi kutoka Madagascar wakiongozwa na Abdoul Ohabee Kanoso. Waamuzi wengine ni Basile Alain Rambeloson, Augustin Gabriel Herinirina na Andofetra Avombitana Rakotojaona. Naye Kessy atakuwa kamishna wa mechi ya kwanza ya raundi ya kwanza ya Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) kati ya Rwanda na Kenya itakayochezwa jijini Kigali. Waamuzi wa mechi hiyo wanatoka Cameroon. Mwamuzi wa kati ni Sylvie Abou wakati wasaidizi wake ni Winnie li Koudangbe, Lum Rochelle na Jeanne Ekoumou.

No comments:

Post a Comment