Friday, June 13, 2014

FIFA INAPASWA KUIGA NBA ILI KUTOKOMEZA UBAGUZI - WEBB.

OFISA mkuu wa kikosi kazi cha kupambana na ubaguzi cha Shirikisho la Soka Duniani-FIFA, amesema timu zinapaswa kuondolewa katika michuano ya Kombe la Dunia kama mashabiki wake au wachezaji watakutwa na hatia ya kufanya vitendo vya ubaguzi wa rangi. Jeffrey Webb ambaye pia ni makamu wa rais wa FIFA amesema wanatakiwa kufuata mfano wa Ligi ya Mpira wa Kikapu nchini Marekani-NBA baada ya mmiliki wa timu ya Los Angeles Clippers Donaldo Sterling kulazimishwa kuiuza timu hiyo kwa kutoa kauli za kibaguzi. Webb amesema NBA wameweka sheria mpya na anaziunga mkono kwani kama wanataka kutokomeza masuala hayo inabidi wafanye kama hivyo. Sterling alifungiwa maisha kujishughulisha na masuala ya mchezo wa kikapu na kutozwa faini ya paundi milioni 1.5 baada ya kurekodiwa akimwambia mwanamke mmoja kutomhusisha na masuala ya watu weusi au kuwaleta uwanjani. Webb aliendelea kudai kuwa ana matumaini ya wazi kuwa FIFA italisimamia hilo na kamati zao za nidhamu kuweka adhabu kali na kuacha mazungumzo badala yake kufanya kwa vitendo.

No comments:

Post a Comment