Friday, June 26, 2015

FA YATETEA UAMUZI WAKE WA KUWAACHA BAADHI YA WACHEZAJI WA LIGI KUU KATIKA KIKOSI CHA UNDER21.

MKURUGENZI wa maendeleo wa Chama cha Soka cha Uingereza-FA Dan Ashworth amedai kuwa walifanya uamuzi sahihi wa kuwaondoa baadhi ya wachezaji wa Ligi Kuu katika kikosi cha timu ya taifa kilichoshiriki michuano ya Ulaya kwa vijana chini ya umri wa 21. Kikosi cha Uingereza kilichokuwa chini ya kocha Gareth Southgate kilishindwa kuvuka hatua ya makundi ya michuano hiyo inayoendelea huko Jamhuri ya Czech. Akihojiwa Ashworth alitetea uamuzi wao huo akidai kuwa timu za vijana zipo kusaidia kuwakuza wachezaji na kuwapa uzoefu kuingia katika timu ya wakubwa. Mshambuliaji wa Liverpool Raheem Sterling, kiungo wa Everton Ross Barkley, viungo wa Arsenal Alex Oxlade-Chamberlain na Jack Wilshere na mlinzi wa Manchester United Phil Jones ni miongoni mwa wachezaji waliokuwa wakihitajika katika timu hiyo, lakini hawakuitwa. Baadhi ya wachezaji wa Ligi Kuu waliochukuliwa kwa ajili ya michuano hiyo ni pamoja na mshambuliaji wa Tottenham Harry Kane, mlinzi wa Everton John Stones na mshambuliaji mpya wa Liverpool Danny Ings. Katika michuano hiyo Uingereza, ilipoteza kwa Ureno kwa kufungwa 1-0, lakini wakazinduka na kuifunga Sweden kwa idadi kama hiyo huku wakipoteza mchezo wao mwisho kwa kuchapwa mabao 3-1 na Italia.

No comments:

Post a Comment