Tuesday, February 19, 2013

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

FIFA YASITISHA MCHAKATO WA UCHAGUZI TFF
SHIRIKISHO la Kimaifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limeahirisha uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kutokana na mkanganyiko uliojitokeza katika mchakato wa uchaguzi huo. Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za TFF jijini Dar es Salaam leo mchana (Februari 19 mwaka huu), Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema FIFA imetuma barua ikiagiza mchakato wa uchaguzi usimame baada ya kupata malalamiko. Amesema kutokana na mkanganyiko huo, FIFA katika barua yake ya leo (Februari 19 mwaka huu- imeambatanishwa) imeagiza mkutano wa uchaguzi wa TFF ambao awali ulipangwa kufanyika Februari 24 mwaka huu uahirishwe hadi hapo itakapotuma ujumbe wake nchini. Ujumbe huo wa FIFA unatarajiwa kufika nchini katikati ya mwezi ujao (Machi) ambapo utafanya tathimini ya hali hivyo, kutuma ripoti yake katika shirikisho hilo na baadaye kutoa mwongozo wa nini kifanyike. Rais Tenga amewaomba radhi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na uamuzi huo wa FIFA, hivyo kwa sasa hakutakuwa tena na mkutano huo mpaka hapo watakapopewa taarifa nyingi. Amesema TFF inakaribisha kwa mikono miwili uamuzi huo wa FIFA kwa sababu ni chombo ambacho cha juu kimpira duniani, na hatua hiyo ina lengo la kuhakikisha kuwa kila mhusika katika mchakato huo wa uchaguzi anapata haki yake. “Nia yetu ni kuona watu wanatendewa haki, na nia ya FIFA ni kutafuta ukweli. Hivyo wahusika (waathirika) wajiandae, watumie wakati huu kuandaa hoja zao ili FIFA wakifika wawasikilize, wapate maelezo ya kina kuhusu utaratibu na malalamiko yaliyotolewa,” alisema Tenga. Rais Tenga amesema timu hiyo ya FIFA itakapofika yenyewe ndiyo itakayopanga izungumze na nani kwa wakati gani, hivyo ni vizuri waathirika na vyombo vyote vilivyohusika na mchakato wa uchaguzi wakajiandaa. Amesema ilikuwa ni muhimu suala hili likatatuliwa katika ngazi ya FIFA kwa lengo la kuhakikisha uchaguzi utakapofanyika TFF inaendelea kuwa chombo kimoja badala ya kurudi katika migogoro iliyokuwepo huko nyuma. “Nataka tubakie kama tulivyokuwa. Malumbano yaishe. Pangeni hoja, wakija hao waheshimiwa (FIFA) muwaambie. FIFA ni chombo cha juu, nafurahi wamekubali kuingia katika hili, kwani wana shughuli nyingi wangeweza kukataa,” amesema.Kuhusu fursa ya kufanya marejeo (review) kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi inayoongozwa na Idd Mtiginjola ambayo aliielezea Jumamosi, Rais Tenga amesema kwa vile hicho ndicho chombo cha mwisho nchini katika masuala ya uchaguzi alishauriwa kuwa kingeweza kufanya review. “Kwa vile hakuna chombo kingine, nikashauriwa kuwa kinaweza kufanya review. Katika utaratibu wa kutoa haki, uamuzi ni lazima uwe wa wazi kwa kutoa sababu. Nilidhani hilo linawezekana, kwani Mahakama Kuu hufanya hivyo. Kwa hili uamuzi wa Mtiginjola ni sahihi,” amesema Rais Tenga. Kamati ya Mtiginjola iliyokutana jana (Februari 18 mwaka huu) ilitupa maombi ya review yaliyowasilishwa mbele yake na waombaji uongozi watano kwa vile hakuna kipengele chochote kwenye Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi kinachotoa fursa hiyo. Waombaji hao walikuwa Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board). Wengine ni walioomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na Kanda zao kwenye mabano; Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).

NI KIBARUA PRISONS, SIMBA JIJINI MBEYA
BAADA ya sare mbili mfululizo, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Simba kesho (Februari 20 mwaka huu) wanashuka Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya wakiwa wageni wa Tanzania Prisons. Katika mechi zake mbili zilizopita, Simba iliondoka pointi mbili tu kati ya sita ilizokuwa ikizipigania. Ilitoka sare na timu za JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baadaye sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Oljoro JKT. Hiyo itakuwa mechi ya nne kwa Mfaransa Patrick Liewig tangu aanze kuinoa Simba huku akifanikiwa kuondoka na ushindi katika mechi moja dhidi ya African Lyon inayokamata mkia kwenye ligi hiyo. Simba iliilaza Lyon mabao 3-1. Kwa upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9 mwaka huu. Hekaheka nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha timu 14. Mwamuzi Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa timu zote mbili. Nayo JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15. Iwapo itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina pointi 33.

No comments:

Post a Comment