Tuesday, July 16, 2013

MADRID YAIPIGA KIKUMBO MAN UNITED KATIKA ORODHA YA VILABU TAJIRI DUNIANI.

KLABU ya Real Madrid ya Hispania imetajwa kuwa klabu yenye thamani zaidi katika orodha ya timu za michezo 50 zenye thamani zaidi duniani iliyotolewa na jarida Forbes la nchini Marekani. Katika orodha hizo timu za Ligi Kuu ya Mpira wa Kimarekani-NFL ndizo zilizoonekana kutawala kwa kiasi kikubwa. Kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa na jarida hilo Madrid ambao ni mabingwa mara tisa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya wana utajiri unaofikia dola bilioni 3.3, utajiri huo ukiwa umeongezeka kwa dola bilioni 1.88 kulinganisha na mwaka uliopita baada ya kuongeza mapato yao kwa kuingia mikataba na kampuni za Adidas na Shirika la Ndege la Emirates. Manchester United wamepigwa kikumbo na Madrid na kushuka mpaka nafasi ya pili wakiwa na utajiri wa dola bilioni 3.17 wakati mabingwa wa Hispania Barcelona wao wamekwea kutoka nafasi ya tano mpaka ya tatu wakiwa na utajiri unaofikia dola bilioni 2.6. Nafasi ya nne inashikiliwa na timu ya Baseball ya Marekani ya New York Yankees ambao wana dola bilioni 2.3, wakifuatiwa na Dallas Cowboys ya NFL dola bilioni 2.1 na New England Patriots dola bilioni 1.6. Nyingine ni Los Angeles Dodgers ya baseball dola bilioni 1.6, timu za NFL Washington Redskins na New York Giant pamoja na klabu ya soka ya Arsenal ya Uingereza ambazo zote hizo zina utajiri wa dola bilioni 1.3.

No comments:

Post a Comment