Saturday, December 21, 2013

SINA MATUMAINI YA KUITWA KOMBE LA DUNIA - TEVEZ.

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Argentina amedai kuwa hana matumaini ya kuitwa katika kikosi cha nchi hiyo kitakachoshiriki michuano ya Kombe la Dunia mwakani. Tevez mwenye umri wa miaka 29 ambae amekuwa katika kiwango kizuri msimu huu ambapo ameifungiwa timu yake ya Juventus mabao 10, amekuwa akiachwa katika kikosi cha nchi yake toka Alejandro Sabella alipotwaa mikoba ya kuinoa Argentina Agosti mwaka 2011. Akihojiwa Tevez amesema kama Sabella hatamwita katika kikosi chake, hana mpango wa kumpigia simu na kumhoji kwanini hajamwita kwasababu anataka aifanye kazi yake kwa weledi. Nyota huyo wa zamani wa vilabu vya Manchester City, Manchester United na West Ham United amesema ana mahusiano mazuri na wachezaji wote wa Argentina pamoja na nahodha wao Lionel Messi, hivyo suala la yeye kuitwa au kutokuitwa ni juu ya kocha mwenyewe. Argentina ambao ni mabingwa wa Kombe la Dunia mwaka 1978 na 1986 wamepangwa kundi F sambamba na timu za Bosnia, Iran na Nigeria.

No comments:

Post a Comment