Friday, January 31, 2014

CITY YAINGIA SOKONI KWA FUJO, YAWATAKA WAWILI KWA MPIGO.

WAKATI pilikapilika za usajili wa dirisha dogo barani zikielekea ukingoni, vinara wa Ligi Kuu nchini Uingereza klabu ya Manchester City imepanga kusajili nyota wawili Eliaquim Mangala na Fernando kutoka klabu ya FC Porto ya Ureno. Pamoja na ushindi mnono wa mabao 5-1 waliopata dhidi ya Tottenham Hotspurs, meneja wa City Manuel Pellegrini bado anaonyesha hajaridhishwa na safu ya ulinzi ya kikosi chake ndio maana anataka kuongeza nguvu mpya kabla ya muda wa mwisho wa usajili leo usiku. City wanatarajiwa kutoa kitita cha paundi milioni 35 kwa ajili ya Mangala mwenye umri wa miaka 22 huku Mbrazil Fernando mwenye umri wa miaka 26 naye akitarajiwa kuongeza nguvu katika safu ya kiungo. Mbali na City, Mangala ambaye ni raia wa Ufaransa amekuwa akizivutia timu kama Manchester United na Paris Saint-Germain ya Ufaransa. Kama Mangala akifanikiwa kutua City, itafungua milango kwa beki mahiri wa kimataifa wa Uingereza Joleon Lescott kuondoka klabuni hapo kwa mkopo.

No comments:

Post a Comment