Monday, March 31, 2014

VALDES NJE MIEZI SABA.

KLABU ya Barcelona, imethibitisha kuwa Victor Valdes amefanyiwa upasuaji wa goti wenye mafanikio na anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa muda wa miezi saba akijiuguza. Valdes amefanyiwa upasuaji huo leo baada ya kuchanika msuli wa katikati ya goti lake la kulia katika ushindi wa mabao 3-0 waliopata Barcelona dhidi ya Celta Vigo wiki moja iliyopita. Katika taarifa iliyotumwa katika mtandao wa klabu hiyo imedai kuwa golikipa huyo alifanyiwa upasuaji wenye mafanikio chini madaktari bingwa Ulrich Boenisch na Ricard Pruna huko Augsburg. Kutokana na majeraha hayo ya Valdes ambaye yatamuweka nje katika michuano ya Kombe la Dunia kipindi cha kiangazi, kinafanya kikosi cha Barcelona kinachonolewa na Gerardo Martino kubakiwa na Jose Pinto huku wakiingia katika wakati muhimu wa msimu wa 2013-2014.

No comments:

Post a Comment