Friday, June 27, 2014

KOMBE LA DUNIA 2014: MARADONA AIPONDA TENA FIFA KWA ADHABU YA SUAREZ WALIYOTOA.

NGULI wa soka wa Argentina, Diego Maradona ameendeleza vita na Shirikisho la Soka Dunia-FIFA kwa kuponda adhabu waliyotoa dhidi ya Luis Suarez baada ya kukutwa na hatia ya kumng’ata Giorgio Chiellini wa Italia. Nyota huyo wa kimataifa wa Uruguay na klabu ya Liverpool, amefungiwa miezi minne kujishughulisha na amsuala ya soka pamoja na kufungiwa mechi tisa za kimataifa kwa kutenda tukio hilo kwa mara ya tatu ndani ya miaka minne. Maradona ambaye alivaa fulana iliyokuwa na maandishi ya kumuunga mkono Suarez yaliyosomeka Luis tuko pamoja ameiponda FIFA na kudai kuwa wanamhukumu kama vile amefanya kosa kubwa sana. Maradona amesema uamuzi huo ni mkubwa na haelewi ni kwani kwani Suarez hajaua mpaka apewe adhabu kali kama hiyo. Maradona alihoji kuwa kama FIFA wanaona amefanya kosa kubwa sana kwanini wasimfunge pingu na kumpeleka katika gereza la wafungwa kigaidi la Marekani la Guantanamo Bay. Nguli huyo aliendelea kudai kuwa anakumbuka tukio la Zinedine Zidane alilofanya katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2006 lakini FIFA badala ya kutoa adhabu kali waliishia kumpa tuzo ya mpira wa dhahabu. Maradona amesema amesikitishwa na jinsi Suarez anavyochukuliwa kama muhalifu kwa kusindikizwa kuondoka kambini akiwa chini ya ulinzi wa polisi ndio maana ameamua kumtetea katika vyombo vya habari kwani adhabu aliyopewa imekuwa kali sana.

No comments:

Post a Comment