Thursday, March 26, 2015

FA KUMUONGEZA MKATABA HODGSON MWAKANI.

MWENYEKITI wa Chama cha Soka cha Uingereza-FA Greg Dyke anapanga kuzungumza na kocha wa timu ya taifa ya nchi hiyo Roy Hodgson kuhusu mkataba mpya mapema mwaka ujao. Hodgson mwenye umri wa miaka 67 alichukua mikoba ya Fabio Capello Mei mwaka 2012 lakini kikosi chake kilijikuta kiking’olewa katika hatua ya makundi ya Kombe la Dunia mwaka jana. Hata hivyo, Uingereza ndio wanaoongoza kundi lao katika mechi za kufuzu michuano ya Ulaya mwakani baada ya kushinda mechi zao nne za kwanza. Mkataba wa sasa wa Hodgson unamalizika baada ya michuano ya Ulaya itakayofanyika nchini Ufaransa na Dyke amesema mapema mwakani watajadiliana kuhusiana na mustakabali wa kocha huyo. Hodgson ambaye amewahi kuinoa Switzerland kuanzia mwaka 1992 mpaka 1995, aliiwezesha Uingereza kutinga hatua ya robo fainali ya michuano ya Ulaya mwaka 2012 ambapo walitolewa kwa changamoto ya mikwaju ya penati na Italia.

No comments:

Post a Comment