Monday, June 20, 2016

CAVALIERS WAWEKA HISTORIA NBA.



TIMU ya Cleveland Cavaliers imekuwa ya kwanza kubadili matokeo wakitokea nyuma kwa kufungwa 3-1 na kushinda taji la Ligi ya Mpira wa Kikapu nchini Marekani NBA kwa kuichapa Golden State Warriors. Nyota wa Cavaliers, LeBron James ndio aliyekuwa nyota katika mchezo huo wa saba wa fainali akifunga alama 27, kusaidia zingine 11 na kuokoa mara 11. Akihojiwa James ambaye aliahidi kuwakata kiu mashabiki wa Cavaliers ambao kwa kipindi kirefu walikuwa hawajatwaa taji hilo, amesema alijitoa kwa kila kitu na anashukuru ahadi yake aliyotoa miaka miwili iliyopita imetimia.  Naye kocha wa Cavaliers, Tyronn Lue ambaye alichukua mikoba ya kuinoa timu hiyo Januari baada ya kutimuliwa kwa David Blatt amesema wameweka historia ya kipekee kwa kupeleka taji hilo katika ardhi ya mji wa Cleveland baada ya kupita kipindi kirefu cha miaka 52. Katika mchezo huo ulioshuhudiwa na mamilioni ya watu duniani kote akiwemo rais wa Marekani Barack Obama, James aliteuliwa kuwa mchezaji bora wa fainali hizo ikiwa ni mara ya tatu kutwaa tuzo hiyo baada ya kuitwaa mara mbili akiwa na timu ya Miami Heat. Obama aliutizama mchezo huo akiwa katika ndege yake ya Air Force One na ilimbidi asubiri mchezo umalizike ndio ashuke na kuendelea na shughuli nyingine pindi walipowasili jijini Calfornia akiwa na familia yake.

No comments:

Post a Comment