Thursday, August 25, 2016

SAMATTA NJIANI KUANDIKA HISTORIA NA GENK.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta leo anatarajiwa kuingoza klabu yake ya KRC Genk ya Ubelgiji katika mchezo wa marudiano wa mwisho kuwania nafasi ya kufuzu hatua ya makundi ya michuano ya Europa League dhidi ya Lokomotiva Zagreb ya Croatia. Katika mchezo huo Genk watakuwa katika Uwanja wao wa nyumbani wa Luminus Arena wakijaribu kutafuta matokeo ya kusonga mbele baada ya sare ya mabao 2-2 katika mchezo wao wa mkondo wa kwanza uliochezwa katika Uwanja wa Maksimir jijini Zagreb. Katika mchezo uliopita Samatta ambaye pia ni nahodha wa Taifa Stars, alifunga bao katika sare hiyo iliyopatikana na wanakwenda katika mchezo huo wakiwa wametoka kushinda mchezo wao ligi ya Ubelgiji kwa mabao 3-0 Jumapili iliyopita huku Samatta akifunga mabao mawili kati ya hayo. Kama Genk wakifanikiwa kupata sare ya bila mabao au ushindi mwembamba kuanzia 1-0 moja kwa moja watakuwa wametinga hatua inayofuata ya makundi ambayo ratiba yake inatarajiwa kupangwa kesho.

No comments:

Post a Comment