Wednesday, December 21, 2016

VARDY KUTUMIKI ADHABU YA MECHI TATU.



MSHAMBULIAJI wa Leicester City, Jamie Vardy anatarajiwa kukosa mechi tatu baada ya rufani yake kupinga kadi nyekundu aliyopewa Jumamosi iliyopita katika mchezo dhidi ya Stoke City kukataliwa. Chama cha Soka cha Uingereza-FA kilitupilia mbali rufani hiyo, hivyo sasa Vardy anatarajiwa kukosa mechi dhidi ya Everton, West Ham United na Middlesbrough. Nyota huyo wa kimataifa wa Uingereza alitolewa nje na mwamuzi Graig Pawson katika dakika ya 28 kwa kumkwatua Mame Diouf wa Stoke. Baada ya mchezo huo meneja wa Leicester Claudio Ranieri alimtetea Vardy akidai alikuwa amefuata mpira na sio kucheza rafu hivyo alidhani pengine mwamuzi angempa kadi ya njano badala ya nyekundu kama alivyofanya. Baada ya kukosa mechi zote za msimu wa sikukuu, Vardy anatarajiwa kurejea uwanjani Januari 7 mwakani wakati Leicester itakapochuana na Everton tena katika mzunguko wa tatu wa michuano ya Kombe la FA.

No comments:

Post a Comment