Friday, January 20, 2017

FIFA YAAMRIWA KUMLIPA LASSANA DIARRA EURO MILIONI SITA.

MAHAKAMA nchini Ubelgiji imetoa hukumu kuwa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA na lile la Uholanzi-KBVB kulaumiwa kwa kushindikana kufanyika usajili wa Lassana Diarra kwenda Charleroi mwaka 2015 na sasa lazima wamlipe kiungo huyo euro milioni sita. Mahakama ya Charleroi iliamua kuwa FIFA walikiuka sheria ya Umoja wa Ulaya-EU kwa kuingilia uhuru wa kuhama baada ya kudai kuwa klabu yeyote itakayomsajili Diarra italazimika kulipa deni la euro milioni 10 anazodaiwa na klabu ya Lokomotiv Moscow. Kiungo huyo wa zamani wa Arsenal, Chelsea na Real Madrid alilimwa faini hiyo kubwa kwa kuvunja mkataba wake wa miaka minne na Lokomotiv, kwa kuondoka katika klabu hiyo ya Urusi baada ya kupita miezi 12 pekee. Kufuatia muongozo huo wa FIFA, klabu ya Charleroi ya Ubelgiji ilisitisha mazungumzo yake na Diarra Februari mwaka 2015 na baadae nyota huyo kujiunga na Marseille kufuatia kutocheza msimu mzima wa 2014-2015.

No comments:

Post a Comment