Thursday, January 19, 2017

SENEGAL YAWA YA KWANZA KUTINGA ROBO FAINALI AFCON, TUNISIA YAZINDUKA.

TIMU ya taifa ya Senegal imekuwa timu ya kwanza kutinga hatua ya robo fainali ya michuano ya Mataifa ya Afrika baada ya kuishindilia Zimbabwe kwa mabao 2-0 katika mchezo wa kundi B uliochezwa jijini Franceville. Mabao ya Sadio Mane katika dakika ya tisa na lingine la mpira wa adhabu lilifungwa na Henry Saivet katika dakika ya 13 yalitosha kuwahakikishia nafasi ya kutinga hatua ya mtoano baada ya pia kushinda mabao 2-1 dhidi ya Tunisia katika mchezo wao wa kwanza. Katika mchezo wa awali Tunisia nao walifanikiwa kurekebisha makosa yao ya kupoteza mchezo wao wa kwanza kwa kuichapa Algeria mabao 2-1 na kufufua matumaini yao ya kusonga mbele. Timu hizo zinatarajia kucheza mechi zao za mwisho za kundi B Jumatatu ijayo ambapo Senegal watapepetana na Algeria jijini Franceville wakati Zimbabwe wakitafuta ushindi wao wa kwanza katika michuano hii kwa kuchuana na Tunisia huko Libreville.

No comments:

Post a Comment